Search This Blog

Friday, November 2, 2012

Serikali isipokunjua makucha uhaba wa mafuta utadumu

Maoni ya mhariri-Gazeti la Mwananchi

Share bookmark Print Email Rating
 


Imetuwa  Alhamisi,Novemba1  2012  saa 22:53 PM
Kwa ufupi
Pasipo kwanza kutafuta kiini cha uhaba wa mafuta, Serikali juzi ilikurupuka na kuagiza kusitisha kusafirisha mafuta nje ya nchi. Wakati PIC ikisema mafuta yako ya kutosha na kwamba siyo jukumu lake kusambaza mafuta hayo, Ewura nayo imenawa mikono na kusema kampuni za mafuta ndizo zinazopaswa kulaumiwa kwa uhaba huo wa mafuta. Hapa tunaona wazi kwamba kutokuwapo uwajibikaji wa moja kwa moja kwa mamlaka ni sehemu ya tatizo.
SAKATA la uhaba wa mafuta nchini sasa limekuwa kama mchezo wa kuigiza. Wakati kampuni  inayoratibu uagizaji wa mafuta kwa pamoja (PIC) ikiwa inalumbana na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), kuhusu uhaba mkubwa wa mafuta uliopo nchini, Serikali imebakia tu kutoa maagizo ambayo yanaonekana kutotiliwa maanani na wafanyabiashara ya mafuta.
   Pasipo kwanza kutafuta kiini cha uhaba wa mafuta, Serikali juzi ilikurupuka na kuagiza kusitisha kusafirisha mafuta nje ya nchi. Wakati PIC ikisema mafuta yako ya kutosha na kwamba siyo jukumu lake kusambaza mafuta hayo, Ewura nayo imenawa mikono na kusema kampuni za mafuta ndizo zinazopaswa kulaumiwa kwa uhaba huo wa mafuta. Hapa tunaona wazi kwamba kutokuwapo uwajibikaji wa moja kwa moja kwa mamlaka ni sehemu ya tatizo.
  
Takwimu zilizotolewa juzi na Ewura zilionyesha kwamba kipo kiasi cha kutosha cha mafuta ya taa, dizeli na petroli, hivyo wakosoaji wanasema Serikali haikupaswa kuagiza zichukuliwe hatua za dharura kabla ya kufanya tathmini na uchambuzi wa tatizo hilo. Licha ya kuagiza usitishaji wa kusafirisha mafuta nje ya nchi, Serikali pia ilitoa maagizo mengine mengi ya kuchukuliwa hatua za dharura, ikiwa ni pamoja na kuharakisha meli za mafuta kuingia bandarini, Ewura kuhakikisha siyo tu inasimamia usambazaji wa mafuta, bali pia kuhakikisha nusu ya mafuta yote yaliyokuwa yasafirishwe kwenda nje ya nchi yanapelekwa mikoani.
  
Inastaajabisha kuona kuwa, pamoja na ukweli kwamba tatizo la uhaba wa mafuta limekuwa likitokea mara kwa mara, Serikali haijafanya uchunguzi kwa lengo la kutambua chanzo cha tatizo, kwani ingefanya hivyo ingegundua kwamba baadhi ya viongozi wa juu serikalini wanafanya biashara ya mafuta, hivyo wana maslahi binafsi na ndiyo maana wanapata kigugumizi kuchukua hatua stahiki.
    Ingefanya hivyo, Serikali pia ingegundua kwamba uhaba huo wa mafuta siyo uhaba halisi isipokuwa ni uhaba bandia unaosababishwa na baadhi ya makampuni ya mafuta na baadhi ya wamiliki wa vituo vya kuuzia mafuta ambao wanaficha mafuta kila mara Ewura inapotangaza kuteremka kwa bei ya mafuta. Pia zipo tetesi kwamba ndani ya Ewura wapo baadhi ya maofisa wanaowadokeza wafanyabiashara hao mapema kabla ya Ewura haijatangaza kupanda au kushuka kwa bei za mafuta.
  
Serikali ingefanya uchunguzi pia ingegundua kwamba tatizo hilo linachangiwa na sababu za udhaifu wa kisera, kiutendaji, kimaamuzi na kiusimamizi kwa baadhi ya viongozi na watendaji. Tunashuhudia viongozi na watendaji wakiwa watazamaji tu kabla na baada ya tatizo hilo kutokea, pamoja na ukweli kwamba zipo sheria zinazowapa mamlaka ya kudhibiti na kutoa adhabu kwa wanaokiuka sheria hizo.
   Hivi sasa imejitokeza biashara ya kuuza mafuta kwa kutumia madumu kwa bei ya juu mno. Tungetegemea Serikali na vyombo vyake viendeshe operesheni katika makampuni ya mafuta na vituo vya kuuzia mafuta kupata uhakika wa kuwapo au kutokuwapo mafuta. Msako huo ukiendeshwa kiadilifu bila shaka utawanasa wafanyabiashara wengi waovu wanaosababisha uhaba huo bandia.
   Serikali inayo vyombo vya dola na inashangaza kuona haivisimamii kikamilifu ili vifanye kazi yake kwa ufanisi, licha ya ukweli kwamba inatambua fika athari za uhaba huo wa mafuta kwa uchumi na usalama wa nchi. Kwa mfano, Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), juzi ilikanusha habari zilizodai kwamba kuna matatizo ya kupakua mafuta bandarini na kusema meli zimekuwa zikiendelea kushusha nishati hiyo kama kawaida.
 
Tunaitaka Serikali itambue kwamba vitendo vya kuficha mafuta ni hujuma kwa uchumi wetu na Idara ya Usalama wa Taifa inapaswa kuwajibika kwa kufichua hujuma hizo, vinginevyo iwe tayari kuwajibishwa. Wananchi wamechoka kuona Serikali waliyoiweka madarakani inazidiwa nguvu na kundi dogo la wafanyabiashara wanaotamba mitaani kwamba wameiweka Serikali mfukoni. Tunadhani huu sasa ni wakati mwafaka wa Serikali kukunjua makucha yake na kuwatia adabu wafanyabiashara hawa waovu.

No comments:

Post a Comment