Search This Blog

Friday, December 28, 2012

Dawa za CCM, Zimegeuka Sumu!

Iwapo unaumwa, njia pekee ili upate kupona lazima upate matibabu. Na kwa wale wa imani za kileo matibabu yao ni kwa njia ya uponywaji. Lakini pia, wakati mwingine si mpaka uumwe. Unaweza kutumia dawa ili kujikinga na maradhi kabla hata hayajakufika. Kinga ni bora kuliko tiba, na pia ni vema kuswali kabla hujaswaliwa!

Naamu! CCM inayoongoza Serikali isiyokuwa na dini, nayo toka kale inazo dawa na sindazo zake za kinga na matibabu. Miongoni mwa dawa na sindano hizo ni UMOJA wa Kitaifa, UADILIFU wa Viongozi, CHEO kama DHAMANA, na UONGOZI Bora wa Watu Kujiletea Maendeleo yao Wenyewe. Vifuko vya dawa hizi, vingi vilijumuhiswa na kufanywa kifurushi kimoja cha dawa iitwayo AZIMIO la Arusha.

Taifa chini ya CCM lilipougua ukabila na udini, viongozi wa CCM walifanya utabibu haraka wakitumia dawa iitwayo UMOJA wa Kitaifa, rushwa na ubadhilifu wa mali ya umma punde tu ulipoibuka, wale wote waliobainika mara moja walidungwa sindano ya UADILIFU. Na mwenendo wa Serikali katika kupambana na maadui (Ujinga, Umaskini, na Maradhi) wa Taifa ilikuwa si kutembeza bakuli la kuomba misaada toka Ulaya na Amerika bali kuwatumia VIONGOZI Bora kuwaunganisha wananchi katika kuchangia vipawa, ujuzi, na mali katika kujiletea maendeleo yao kwa kutumia rasilimali za nchi yao. Na hii ndiyo ilikuwa dhana kuu ya UJAMAA na KUJITEGEMEA.

Lakini la ajabu, leo hii, CCM ndiyo kinara wa kuchua dawa ya kubomoa UMOJA wa Kitaifa kwa kuendekeza Udini na Ukabila. Tumelishuhudia hili wakati wa Uchaguzi Mkuu na limejirudia tena katika Chaguzi Ndogo za Igunga na Arumeru. Tumeona jinsi CCM ya leo inavyoshangilia wasio-WAADILIFU kuwadunga sindano za mauti Wanaopinga RUSHWA na UBADHILIFU wa Mali za Umma. Na kubwa zaidi sote tu mashahidi, kwa CCM ya leo Cheo si DHAMANA bali BIDHAA inayonunuliwa na Matajiri ili wafanikishe mambo yao kupitia migongo ya Wapiga kura.

CCM imefanikiwa kwa muda kugeuza matumizi ya dawa zake bila kudhurika. Habari njema ni kwamba, dawa zote sasa zimefikia ukomo wa matumizi na zimegeuka sumu tena kali. Kwa sasa, UMOJA unaanzishwa na Wananchi wenyewe kuikabili CCM. Wananchi hawakubali tena kugawanywa katika makundi ya kidini wala kikabila ili CCM ipenye kuwatawala tena. Wananchi wanawataka na wanawajua watu waadilifu. Na wanapojitokeza wanaogawa RUSHWA, wananchi wanaipokea na kuila lakini haibatilishi maamuzi yao yaliyo sahihi moyoni. Au wanaitumia hiyo pesa ya RUSHWA kumchangia mtu muadilifu wampendaye ili afikie hatma ya kuwa kiongozi wao. Hili limethibitika katika Uchaguzi Mkuu na limejirudia tena hivi karibuni huko Arumeru Mashariki. Kiongozi ambaye Wananchi wanamhitaji ni yule atakaye waongoza katika kutetea HAKI zao na kuwaunganisha KUJILETEA maendeleo. Kitendo alichokifanya Kilema mmoja huko Mwanza, cha kutoa Kuku wake wa Pasaka anadishwe katika Harambee ya kuchangia madawati iliyoongozwa na Mbunge Wenje ili naye achangie watoto kupata mazingira mazuri ya kusomea ni fundisho tosha kwa CCM na watoa RUSHWA.

Ili CCM ipone na dhahama ya sumu inayoendelea kuenea mwilini mwake, lazima kwanza itapishwe na kukamuliwa sumu zote (Ubaguzi, Rushwa, Ubadhilifu, Viongozi Uchwara/wafanyabiashara, n.k) na kisha ianze upya matumizi ya dawa zake za awali (UMOJA, UADILIFU, UONGOZI BORA, CHEO kama DHAMANA). Ni makosa ya makadirio ya kisiasa kwa CCM kufikiria jinsi itakavyobaki madarakani hapo 2015. Hili jambo haliwezekani bila matumizi makubwa yaliyopitiliza ya dola yatakaambatana na umwagaji wa damu isiyo na hatia. Kadirio sahihi kwa CCM ni kufikiri nini itakuwa “Fall-Back Position” hapo 2015 na nini kiandaliwe ili baada ya hapo warudi tena madarakani ndani ya miaka mitano (5). Ni rahisi kwa CCM kurudi ndani ya muda mfupi namna hii kwa sababu, pamoja na maandalizi yanayoendelea kwenye vyama vya upinzani kushika dola, bado ni yatima wa mipango na rasilimali watu makini wa kutekeleza na kukidhi matumaini ya Wananchi ndani ya kipindi kifupi cha miaka mitano (5). Vyama vya Upinzani vimefanya na vinaendelea kufanya makosa makubwa sana kwa kuacha wananchi kuweka matumaini makubwa kupitiliza juu ya nini watakifanya wakiingia madarakani. Wamewaaminisha wanancnhi kwamba kile walichoshindwa CCM kwa miaka 54 (hapo 2015) wao watakifanikisha ndani ya miaka mitano! Kwa kosa hili, wategemee kuchukiwa haraka sana na kupingwa na wananchi hao hao watakaokuwa wamewapa ushindi. Ebu nisitoke ndani ya mada maana hii tayari ni mada nyingine kabisa.

Nakutakia tafakuri njema.
Source:  http://www.jamiiforums.com/jukwaa-la-siasa/252439-zilizokuwa-dawa-za-ccm-ndizo-sumu-zinazoiua-ccm.html

No comments:

Post a Comment