Shehena ya kwanza ya mabomba ya mradi wa gesi Mtwara imepokelewa bandarini leo na Waziri Mkuu Mizengo Pinda. Waziri Mkuu amesema kuwa anashangaa kuona baadhi ya watu kwa makusudi kabisa wanapotosha ukweli wa mambo kuhusu mradi wa gesi Mtwara. Amesema lengo la serikali ni kuhamasisha uchumi wa gesi ili kuboresha maisha ya wananchi kwa kupunguza umaskini.

Aidha Waziri Mkuu ameishukuru serikali ya watu wa China kwa kuiwezesha serikali ya Tanzania kupata mkopo wa riba nafuu kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa gesi Mtwara. Ametoa wito kwa wananchi, wanasiasa, wanahabari na mashirika ya dini na yale yasiyo ya kiserikali na wanaharakati wote kuungana na serikali katika kufanikisha kukamilika kwa mradi huu.

Awali akizungumza kuhusu mradi huo Waziri wa Nidhati na Madini Sospeter Muhongo amesema kuwa sasa serikali imeanza safari ya maendeleo. Alisema sehemu ya kwanza ilikuwa ni kugundua rasilimali zilizopo kwenye ardhi yetu na kwamba sehemu ya pili ni kuanza kuzivuna hizo rasilimali.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC amesema shehena hiyo ni awamu ya kwanza tuu na kwamba zitakuja jumla ya meli nyingine kumi na mbili zenye shehena kama hiyo. Meli iliyowasili ina mabomba karibia 3,400.