Search This Blog

Sunday, July 21, 2013

NEMC KUBOMOA HOTELI YA MKURUGENZI WA JIJI LA DAR



Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingiza (NEMC) linakusudia kubomoa hoteli ya Royal Sunset Beach mali ya Mkurugenzi wa Jiji la Dar es salaam Willson Kabwe kutokana na kujenga ndani ya eneo la mita 60 kutoka Ziwa Victoria kinyume na sheria ya usimamizi wa Mazingira kifungu cha 57 pia kumtoza faini ya Sh10 milioni. 
Mbali na hatua hiyo pia NEMC inaweza kuwatia mbaroni watu wawili ambao ni Wakurugenzi wa Taasisi zisizo za Kiserikali (NGO) kutokana na kudaiwa kughushi mihuri, nyaraka mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutoa vyeti bandia vya Tathimini ya Mazingira (EIA) kwa makampuni ya mane ya Jijini Mwanza na kujipatia fedha kinyume cha sheria.
Mwanasheria wa NEMC Heche Suguta akieleza
Akizungumza na Waandishi wa habari jana Mwanasheria wa NEMC, Manchare Heche Suguta alisema watu hao wamekamatwa baada ya kuwekewa mtego na kutokana na kubainika kuwa walitoa vyeti vya Tathimini ya Mazingira kwa makampuni ya Bibiti Oil (T) ltd, Nyanza Road Works Ltd, Wang Hill Hotel pamoja na Brichand Oil Ltd kwa kutozwa kati kiasi cha Dola za Kimarekani 10,000.
Suguta alisema kwamba Vyeti hivyo ambavyo ni Bandia vilivyotolewa na Mwanza Environment and Conservation of Nature (MEC) pamoja na Mwanza Region Environment Conservation zote za jijini Mwanza na kubainisha kuwa wahusika wake wametiwa mbaroni baada ya kuwekewa mtego na maofisa wa NEMC kama wateja waliokuwa wakihitaji cheti na kukubaliana nao kutoa cheti kwa Sh5 milioni.
 “Kawaida vyeti hivi hutolewa na kusainiwa na waziri na wala siyo NGO, lakini wao wamekuwa wakijifanya ni maafisa wetu na kukagua viwanda ama Hetali zilizojengwa ndani ya maeneo ya Mito, Vyanzo vya maji na ndani ya eneo la Mita 60 kutoka ziwani na hivyo kujipatia fedha kwa udanganyifu,” alieleza na kuongeza kuwa NGO hizo mbili zimefungiwa kuendelea na shughuli zake..
Alisema ofisi yake kwa sasa ambao imeunda Kitengo cha Polisi wa Mazingira kinachosimamiwa na Afisa wa wanaoshughulika na Mazingira kutoka Jeshi la Polisi, ameanza msako na kwamba watawakamata wale wote wenye vyeti Bandia vya Usimamizi wa Mazingira ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua wale wote waliojenga kinyume cha sheria kwa kuwavunjia nyumba zao.
Alisema vyeti hivyo hutolewa na Waziri anayehusika na Mazingira na kusainiwa naye lakini hivyo vilikuwa vikitengenezwa na NGO hizo na kutolewa kwa Makampuni hayo jambo ambalo alisema ni kosa na kuwataka wale wote wenye vyeti bandia kuvisalimisha katika ofisi zao ikiwa ni pamoja na wale wanaohitaji pia.
Aidha katika zoezi la kuwachukulia hatua waliojenga nyumba katika maeneo ya fuko za Ziwa Victoria, NEMC tayari inakusudia kubomoa Hoteli ya Royal Sunset Beach inayomilikiwa na aliyekuwa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza na sasa Jiji la Dar es salaam.
“Tayari tumeshamwangia Barua Julai 10, tukimtaka kubomoa mwenyewe eneo la Hoteli yake ambalo lipo ndani ya MIta 60 ikiwa ni pamoja na kulipa Faini ya Sh10 milioni kwa kutiririsha maji ndani ya ziwa Victoria,” alieleza na kubainisha kwamba iwapo atashindwa kubomoa NEMC itabomoa yenyewe na kumtoza gharama zake.
Akizungumza na Gazeti hili kwa njia ya Simu, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es salaam Wilison Kabwe alieleza kwamba  amejenga kwa mujibu wa Sheria na kubainisha kwamba inaruhusu kujenga vitu ambavyo ‘water related activity’ pamoja na Majengo ya Muda badala ya kudumu.
“Sheria ina niruhusu kujenga majengo ya muda, miundombinu yote pale Hotalini siyo ya kudumu ni ya muda. Ninavyo vibali vingine vinavyoniruhusu kujenga,” alieleza Kabwe.
Hata hivyo mwanasheria wa NEMC alisema sheria ipo wazi na kubainisha kwamba Hoteli hiyo imejenga Majengo ya Kudumu na kwamba walichomwagiza katika barua yao ni kumtaka avunge eneo la Mita 60 kutoka ndani ya Ziwa Victoria.

No comments:

Post a Comment