Search This Blog

Wednesday, January 9, 2013

MAMBO YAZIDI KUIBUKA MAUAJI YA POLISI KARAGWE

Taarifa za kuuawa kwa askari polisi wawili zimezidi kuchukua sura mpya wilayani Karagwe baada ya wananchi kuanza kutoboa unaodaiwa kuwa ukweli wa tukio hilo ambao wanadai umefichwa kwa makusudi na badala yake kuwatolea lawama wananchi.

Ukweli unaoelezwa ni huu: Mtu mmoja (Raymond) wa kijiji cha Rugu (iko wilayani karagwe) alikuwa na meno ya tembo; aliamua kwenda maeneo ya Benaco (iko wilayani Ngara) kutafuta wanunuzi wa Meno ya Tembo na huko aliwapata watu wawili (Abubakari na Geofrey).
Baada ya makubaliano ya kulipwa shs 12 milioni wale wanunuzi walimweleza kuwa kwa kuwa watakwenda usiku na njiani kuna pori la Kimisi watakwenda na mtu wao mwenye bunduki ambaye huwa anawalinda mara kwa mara. Walipofika Rugu wakauona mzigo, wakaupima na kukuta kilo walizokubaliana ndivyo zilivyo.
Mzigo ulipakiwa kwenye gari lao; jamaa hao wakataka kuondoka bila kulipa. Mwenye mali alipouliza mbona hawampi hela yake alijibiwa kuwa 'sisi ni polisi na haya meno ya tembo ni nyara za serilkali, ukileta fujo tutakukamata!'
Kwa kuwa walikuwa na bunduki jamaa aliogopa lakini alijitahidi kupambana na kuvunja kioo cha mbele cha gari hilo. Gari lilipoondoka na mzigo jamaa akapiga simu kwa watu walio kwenye stesheni ndogo ambayo ilikuwa lazima gari hilo lipitie akiwaeleza kuwa wamevamiwa na majambazi lakini wamepambana nao na kupasua kioo cha gari, hivyo wajitahidi kulizuia lisipite.
Raia hao walipanga mawe makubwa barabarani na mara gari hilo likaja - kioo kimepasuliwa na halina namba. Gari liliposimama raia wakaanza kuwahoji wanakotoka na wanakokwenda na walifuata nini.
Ikabidi kichapo kitembee kidogo. Jamaa kuona kichapo kinazidi ikabidi waseme kuwa wao no polisi na kuna mhalifu walikuwa wamnamfuatilia. Lakini raia wakaona hao polisi mbona hawawahamu?
Raia waliamua kupiga simu kwa OCS wa kituo cha karibu (Chanyamisa) akawajibu kuwa hana taarifa zozote na watu hao; wakapiga simu kituo cha Omukaliro, OCS akawajibu kuwa hana taarifa;. Walipiga simu polisi wilayani lakini jibu likiuwa ni hilohilo!
Hao Polisi -majambazi kuona hivyo yule aliyekuwa na bunduki akafyatua risasi hewani raia hawakuogopa wakataka wamkamate, akapiga risasi nyingine ikampiga kijana mmoja kwenye mkono!. Hapo ndipo raia waliona kuwa kumbe hawa tukiwalegezea watatuua. Kichapo kikaendelea lakini aliyekuwa na bunduki alikimbia baada ya kufyatua risasi nyingine. Hao wawili waliobaki walipigwa hadi kufa!
Raia waliamua kulitia gari moto, wakati likiendelea kuuungua walifungua kwenye boot na kukuta meno ya tembo baadhi yakiwa yameanza kuungua kidogo.
Huo ndio unaelezwa kama ukweli baada ya TBC kutangaza wakimkariri msemaji wa jeshi la Polisi kuwa hao polisi walikuwa wanataka kumkamata mhalifu na raia wakawaua ili wasimkamate, raia wamechukizwa sana uongo huo.
Ukweli huu umetobolewa na wananchi katika kipindi cha Radio Jana majira ya saa 3 hadi saa 4:30 Usiku na kituo cha Radio ya kijamii (Radio Fadeco) iliyoendesha kipindi kwa kuruhusu wananchi kupiga simu kueleza nani alaumiwe kwa mauaji ya hao polisi?

No comments:

Post a Comment