Search This Blog

Sunday, January 20, 2013

Halmashauri ya Jiji la Mwanza yadaiwa kuitapeli fedha NSSF

HALMASHAURI ya Jiji la Mwanza chini ya Mkurugenzi wake Willson Kabwe, imeingia katika kashfa baada ya kulipwa Sh1.6 bilioni na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), kwa lengo wa kununua viwanja 692 katika eneo la Bugarika na Kiseke, lakini haikufanya hivyo.
Kashfa hiyo iliibuliwa juzi wakati Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, ilipofanya ziara ya  kukagua miradi ya maendeleo.
Kamati hiyo iliwakutanisha maofisa wa  NSSF na uongozi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza ili kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo lililodumu kwa miaka mitano.
Akitoa maelezo kwa wabunge hao, Kaimu Mkurungenzi wa NSSF, Ludovick Mroso, alisema mfuko wake uliingia mkataba na halmashauri hiyo  chini ya Mkurugenzi Kabwe na kwamba hiyo ilikuwa  mwaka 2008.
Alisema mkataba huo ulikuwa ni  kwa ajili ya kununua jumla ya viwanja 692 ili kujenga nyumba za kuuza, lakini licha ya kuwalipa, bado hawajatoa viwanja kwa NSSF.
Kwa mujibu wa nyaraka za makubaliano baina ya NSSF na Halmashauri ya Jiji la Mwanza wa Agosti 18, 2008, NSSF iliingia mkataba wa jumla ya Sh1.8 bilioni kwa ajili ya kupewa viwanja.
Katika mkataba huo uliosainiwa na Kabwe na mwanasheria wa Jiji John Wanga (wakati huo), utaratibu wa malipo ulikuwa ni katika awamu tatu.
Awamu ya kwanza ilihusisha fedha Sh943 milioni sawa na asilimia 50 mara baada ya mkataba kusainiwa zikiwa ni kwa ajili ya kulipa fidia.
Awamu ya pili ya malipo ilikuwa ni Sh755 milioni sawa na asilimia 30 zikiwa ni fedha zilizopaswa kulipwa baada ya ujenzi wa barabara katika viwanja na malipo ya awamu ya tatu na ya mwisho ilikuwa ni asilimia 20.
Kwa upande wa NSSF waliweza kukamilisha asilimia 80 ya malipo kwa awamu ya kwanza na ya pili kwa kulipia jumla ya Sh1.6 bilioni hadi kufikia Juni 2011, lakini Halamshauri ya Jiji hakuweza kuwakabidhi viwanja hadi jana.
Kaimu Mkurugenzi wa Jiji alidai kuwa mpango huo wa viwanja 300 vya NSSF huko Bugarika ulikwama kutokana na eneo hilo kuibuka vurugu baada ya wananchi wamiliki wa mashamba kuhamasishwa na Mbunge wa Nyamagana Ezekiel Wenje (Chadema) kuanza vurugu. Nkamia akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kikao hicho alisema maelezo ya Jiji yamekataliwa na wabunge na kwamba sababu za kudai walikwamishwa na mbunge wa Chadema ni za uzushi na kuwaomba kuandaa maelezo zaidi ili wawasilishe katika kikao maalumu mjini Dodoma mbele ya waziri wao.

“Hapa tumebaini kuna uhuni mwingi sana. Tumekataa upuuzi huu, Jiji walilipwa fedha ili kutoa viwanja kwa NSSF lakini viwanja hivi wameviuza kwa watu wengine huku wakidai kisa ni Mbunge.
Sasa tumewaita mjini Dodoma mwezi ujao wakati wa vikao vyetu vya Bunge ili waje waeleze mbele ya waziri wao,” alieleza Nkamia na kubainisha hata hivyo alisikitishwa na kukosekana kwa mkurugenzi mwenyewe.
Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/-/1597570/1670262/-/xl8quy/-/index.html

No comments:

Post a Comment