Search This Blog

Sunday, July 14, 2013

Waziri mkuu apokea shehena ya mabomba ya gesi.

Shehena ya kwanza ya mabomba ya mradi wa gesi Mtwara imepokelewa bandarini leo na Waziri Mkuu Mizengo Pinda. Waziri Mkuu amesema kuwa anashangaa kuona baadhi ya watu kwa makusudi kabisa wanapotosha ukweli wa mambo kuhusu mradi wa gesi Mtwara. Amesema lengo la serikali ni kuhamasisha uchumi wa gesi ili kuboresha maisha ya wananchi kwa kupunguza umaskini.

Aidha Waziri Mkuu ameishukuru serikali ya watu wa China kwa kuiwezesha serikali ya Tanzania kupata mkopo wa riba nafuu kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa gesi Mtwara. Ametoa wito kwa wananchi, wanasiasa, wanahabari na mashirika ya dini na yale yasiyo ya kiserikali na wanaharakati wote kuungana na serikali katika kufanikisha kukamilika kwa mradi huu.

Awali akizungumza kuhusu mradi huo Waziri wa Nidhati na Madini Sospeter Muhongo amesema kuwa sasa serikali imeanza safari ya maendeleo. Alisema sehemu ya kwanza ilikuwa ni kugundua rasilimali zilizopo kwenye ardhi yetu na kwamba sehemu ya pili ni kuanza kuzivuna hizo rasilimali.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC amesema shehena hiyo ni awamu ya kwanza tuu na kwamba zitakuja jumla ya meli nyingine kumi na mbili zenye shehena kama hiyo. Meli iliyowasili ina mabomba karibia 3,400.

Wanajeshi saba Watanzania wauawa Dafur

Wanajeshi saba wa Tanzania, ambao ni miongoni mwa kikosi cha Umoja wa Mataifa, cha kulinda amani katika jimbo la Darfur nchini Sudan, wanadaiwa kuwa wameuawa.
Taarifa zilizolifikia gazeti hili jana zilisema kwamba wanajeshi hao wa Tanzania, wamekufa kutokana na mashambulizi yaliyofanywa na waasi wanaopigana na Serikali.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, miili yao wanajeshi hao bado ipo nchini Sudan ikisubiri taratibu za kusafirishwa kuletwa nchini.
Hii ni mara ya kwanza kuripotiwa kwa idadi kubwa ya wanajeshi wa Tanzania wanaolinda amani katika nchi mbalimbali kufa kwa wakati mmoja.
Agosti mwaka jana wanajeshi watatu wa Tanzania huko Darfur waliripotiwa kuuawa kwenye tukio kama hilo.
Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) , Kanali Kapambala Mgawe alipoulizwa kwa njia ya simu kuhusu vifo vya wanajeshi wa Tanzania huko Darfur, alisema kuwa naye amesikia, lakini hana taarifa rasmi kwa mujibu wa taratibu za kiofisi.
Hii ni mara ya pili kwa wanajeshi wa Tanzania kuuawa katika Jimbo la Darfur, ambapo Agosti mwaka jana, Kanali Mgawe alinukuliwa na vyombo vya habari akithibitisha kutokea kwa vifo vya askari watatu ambao gari lao lilizolewa na maji walipokuwa wakivuka mto uliokuwa umefurika maji.
Kanali Mgawe aliwataja askari hao kuwa ni Sajini Julius Chacha, Sajini Anthony Daniel na Koplo Yusuph Said na kwamba askari wengine walinusurika baada ya kuogolea.
Tanzania ina askari 850 kwenye kikosi cha Umoja wa Mataifa cha Kulinda Amani jimbo la Darfur, ambao ni sehemu ya askari 1,081 wa kulinda amani katika jimbo la Darfur.
Wanajeshi hao wa Tanzania wametawanywa kwenye miji ya Khor Abeche na Muhajeria kusini mwa Darfur.
Aprili mwaka huu Tanzania ilipeleka wanajeshi wa kulinda amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kupambana na kikundi cha waasi wa nchi hiyo M23 kinachopigana kuiangusha serikali ya DRC.
Majeshi ya Tanzania yalipelekwa kulinda amani chini ya Umoja wa Mataifa. Tanzania inaungana na nchi za Afrika Kusini na Malawi kukamilisha kikosi cha wanajeshi 3,000. Tanzania imepeleka wanajeshi 850.

“Tanzania imekuwa ikijihusisha na misheni za amani, mafunzo na ushauri kwa nchi nyingi,” alinukuliwa Kanali Mgawe, na kueleza kuwa majeshi ya Tanzania yamekuweko katika vikosi vya kulinda amani huko Lebanon, Darfur, Sudan Kusini, Visiwa vya Comoro na Liberia. Liberia waliuawa wanajeshi wa Tanzania 11.
“Tanzania daima haiendi kwa nchi yeyote bila ya kuombwa na nchi hiyo au kutoka Umoja wa Mataifa,” alisema.
Source:  http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/-/1597296/1914214/-/13b8bno/-/index.html

Sheikh wa wilaya Arusha amwagiwa Tindikali

Wakati vumbi la matukio ya kigaidi ya milipuko ya bomu kanisani na kwenye mkutano wa kampeni za Chadema halijatulia, tukio lingine linalohusishwa na ugaidi limetokea wilayani Arumeru kwa Sheikh wa wilaya hiyo, Said Juma Makamba aliyejeruhiwa kwa kumwagiwa usoni kimiminika kinachoaminika kuwa tindikali.
Sheikh Makamba anayekaimu nafasi hiyo alikutwa na hayo kati ya Saa 4:00 hadi 5:00 usiku wa kuamkia juzi akitoka kusali Tarawei na alilazwa wodi namba nne katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwa matibabu.
IGP Said Mwema
Jicho la kushoto la Sheikh huyo limeathirika, huku akiwa amebabuka na kuvimba usoni, kifuani, mkono wa kushoto na mgongoni.
Akizungumza kwa taabu kitandani kwake alikolazwa, Sheikh Makamba ambaye pia ni Imamu wa Msikiti wa Sekei wilayani Arumeru alisema alimwagiwa tindikali muda mfupi baada ya kurejea nyumbani kwake akitoka kuswali.
“Nilipotoka Msikitini, nilisindikizwa hadi nyumbani na vijana wawili nilioongozana nao kutoka msikitini ambao walihakikisha nimeingia ndani salama. Lakini kabla ya kulala nilitoka nje kwa ajili ya kujisaidia kwenye choo cha nje ndipo nilimwona mtu amesimama pembeni ya nyumba nikiwa najitahidi kumwangalia ili nimtambue, ghafla alinimwagia kitu cha majimaji usoni,” alisema Sheikh Makamba.
Ingawa hataki kuingia kwa undani kuhusu anaowatuhumu na sababu za kumwagiwa tindikali, Sheikh Makamba alisema anadhani jambo hilo linatoakana na ugomvi wa madaraka msikitini hapo.
Katibu wa Bakwata Wilaya ya Arumeru, Sheikh Yahaya Husein Mwangela aliwaomba polisi kuchunguza tukio hilo ili kuondoa hofu miongoni mwa viongozi wa Bakwata.
Hili ni tukio la pili kwa viongozi wa Bakwata Arusha kumwagiwa tindikali baada ya Oktoba mwaka jana, Katibu wa Baraza hilo Mkoa wa Arusha, Abdukarim Njonjo kulipuliwa na kitu kinachosadikiwa kuwa ni bomu. Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa hadi jana kulikuwa hakuna mtu aliyekamatwa.
Source: http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Sheikh-wa-wilaya-arushiwa-tindikali/-/1597296/1914272/-/xxpuox/-/index.html

Saturday, July 13, 2013

Polisi Dar wamvamia Mbowe usiku wa manane

KUNDI la polisi wenye silaha za moto jana usiku walivamia nyumbani kwa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, kwa nia ya kumkamata.

Askari hao wanaokisiwa kufikia saba, wakiwa na silaha nzito katika gari la wazi waliwasili nyumbani kwa Mbowe majira ya saa saba na nusu usiku na kuwaamuru askari wanaolinda nyumbani kwake kumtoa Mbowe nje ili waonane naye.
Mbowe


Walinzi wa Mbowe walihoji uhalali wa ukamataji huo na kuwataka polisi wawaoneshe hati ya kumkamata, lakini hawakuweza kuionesha, hali iliyozusha wasiwasi kwa walinzi wa kiongozi huyo.

Hata hivyo walinzi hao waliwaambia polisi hao kuwa Mbowe ambaye pia ni kiongozi mkuu wa kambi ya upinzani bungeni alikuwa safarini, jibu ambalo lilipokewa kwa shingo upande na askari hao.

Polisi hao baada ya kuona wameshindwa kukamilisha kazi hiyo, waliwaachia walinzi hao namba ya simu 0754-085600 ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Ernest Kimola, wakiwaagiza kuhakikisha wanamwambia Mbowe awasiliane na kamanda huyo.

RCO amsukumia RPC, akana
Hata hivyo, alipohojiwa na Tanzania Daima Jumapili kwa njia ya simu, Mkuu wa Upelelezi Kimola aligoma kuzunguzia suala hilo na kumtaka mwandishi kuwasiliana na mkuu wake wa kazi, ambaye ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Kamilius Wambura, akidai ndiye mwenye haki ya kutoa ufafanuzi wa jambo hilo.

“Unajua mimi si msemaji wa polisi, wasiliana na kamanda wa mkoa, maana ndiye mwenye uwezo wa kutoa maelezo,” alisema Kimola na kukata simu. Lakini alipopigiwa simu Kamanda Wambura aliruka kimanga, kwa mshangao, akidai kutojua lolote kuhusiana na polisi kuvamia nyumbani kwa Mbowe.
“Kwa kweli ndiyo napata taarifa hizo kutoka kwako, kuwa kiongozi huyo alifuatwa na polisi, maana silijui suala hilo hata kidogo,” alisema Wambura, naye kama alivyofanya Kimola akakata simu.

Kauli ya CHADEMA
Lakini wakati Kimola akikataa kusema chochote, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alisema kuwa alizungumza kwa njia ya simu na Kimola kuhusiana na kitendo cha polisi kuvamia nyumbani kwa kiongozi huyo wa juu wa kisiasa, na kudai kupewa majibu ya kushangaza.

Akizungumza jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika Manzese, Wilaya ya Kinondoni, Dk. Slaa alisema Kimola alijitetea akidai kwanza kukana kufika nyumbani kwa Mbowe usiku wa manane. Pili, alisema kuwa hawakwenda kumkamata Mbowe, isipokuwa kufanya naye mazungumzo na kisha wangemwacha.

Slaa alisema kitendo hicho kimewashitua na ni cha kinyama na kilichokiuka sheria za nchi na haki za binadamu. Aliongeza kwamba, daima wamekuwa wakilishutumu Jeshi la Polisi kwa kutumika vibaya kukandamiza wapinzani, lakini mara zote CHADEMA kimepuuzwa na sasa jeshi hilo limeamua kuvamia makazi ya viongozi wa kisiasa kwa madhumuni yasiyoeleweka.

Alisema haijulikani nini kingetokea ikiwa Mbowe angekuwa ndani, ikiwa walinzi wangeamua kugoma kumwachia kiongozi wao. “Tuna hofu kubwa na usalama wetu, maana pale wangeweza kufanya lolote, hata kumuua na kisha kutoa matamshi kuwa walikuwa wanajibishana kwa risasi, kama ambavyo imekuwa jadi ya askari polisi kutoa taarifa za uongo na upotoshaji wanapoua watu,” alisema Slaa.

Alisema ikiwa polisi walikuwa na shida ya kweli, wangemwita kwa njia sahihi na si kumvamia na kuingilia uhuru wake na wa familia yake kama wanakamata gaidi ama jambazi hatari.

Dk. Slaa alisema Mbowe anayo ofisi inayojulikana, na kama kweli hakukuwa na jambo baya lililopangwa na polisi hao wasingeweza kufanya uhuni kama walioufanya.

“Kama wanaweza kuvamia nyumbani kwa kiongozi mkubwa kama Mbowe wakiwa na silaha nzito, itakuwaje kwa viongozi wa kawaida na raia?” alihoji Slaa.

Kutokana na tukio hilo la kuogofya, CHADEMA imemtaka Rais Jakaya Kikwete kuwaeleza Watanzania maana ya matukio haya ambayo yamedhamiria kuleta vurugu kubwa nchini. Kadhalika, wamemtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Said Mwema, kuueleza umma kile kilichokusudiwa na askari wake kuvamia nyumbani kwa Mbowe mithiri ya jambazi.

Itakumbukwa pia kuwa hivi karibuni askari polisi wa Mkoa wa Arusha walivamia nyumbani kwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, wakiwa na silaha nzito na mbwa, na kumkamata, kisha kumtupa rumande kwa siku nzima.

KAULI YA WAZIRI WA FEDHA KUHUSU KODI YA LINE ZA SIMU NI KIELELEZO CHA UDHAIFU WA SERIKALI NA UZEMBE WA BUNGE; NIANDIKIE SASA KUHUSU HATUA ZA KUCHUKUA JUU YA SUALA HILI KUPUNGUZA MZIGO WA GHARAMA ZA MAISHA KWA WANANCHI



Katika kipindi cha Hot Mix cha EATV muda mfupi uliopita Waziri wa Fedha amesema kwamba mawazo ya kutoza elfu moja kwa mwezi kwenye kila laini ya simu ni ya wabunge. 

Kauli inayokaribiana na hiyo imewahi kuandikwa pia na Naibu Waziri wa Wizara yenye dhamana na sekta mawasiliano kwenye mitandao ya kijamii katika siku za karibuni. Baadaye alifuata Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha na sasa waziri mwenyewe. Mwaka 2012 nilitahadharisha kuhusu udhaifu wa Rais (na Serikali) na uzembe wa Bunge katika masuala yanayohusu maandalizi ya bajeti, hususan kutozingatiwa kwa mpango wa taifa wa maendeleo na ongezeko la mara kwa mara la gharama za maisha kwa wananchi. Kwa kauli hizi za Serikali udhaifu na uzembe huo unaendelea kujihidhirisha.

Kauli hizi za Serikali ni za kujivua mzigo wa lawama baada ya malalamiko ya wananchi kuhusu kodi hii na nyinginezo kwa kuhamisha mzigo huo kwa wabunge.

Ni muhimu badala ya kutoa kauli za ujumla za kulaumu wabunge, Serikali ijitokeze itaje kwa majina na wabunge gani hasa walitoa mawazo hayo. Mimi sijawahi kutoa wazo hilo wala kuliridhia. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwenye Hotuba yake juu ya Muswada wa Sheria ya Fedha ilipinga pendekezo hilo lililokuwepo katika jedwali la marekebisho lililowasilishwa na Wizara ya Fedha. Katika kuhakikisha kwamba kifungu hicho hakipitishwi, niliwasilisha jedwali la marekebisho ya sheria kutaka kifungu hicho kiondolewe katika muswada wa sheria ya fedha na marekebisho yake yaliyowasilishwa na Serikali.

Hata kama ikiwa ni ukweli kwamba wazo hilo ni la baadhi ya Wabunge (ambao ni muhimu wakatajwa kwa majina), Serikali inayokwepa kutetea maamuzi ambayo Serikali yenyewe imeyaunga mkono inadhihirisha kwamba imechoka na imepoteza uhalali kwa kimaadili kwa kushindwa kukubalika mbele ya wananchi wake yenyewe (illegitimate government) . 

Mamlaka na madaraka ya Bunge kwa mujibu wa katiba ibara ya 63 ni kuishauri na kuisimamia Serikali. Katika kutekeleza mamlaka hayo, Bunge ni chombo cha uwakilishi wa wananchi na chenye mamlaka pia ya kutunga sheria na kupitisha bajeti ya nchi. Hata hivyo, ibara ya 99 ya Katiba imeweka mipaka kwa mamlaka hayo ya Bunge inapokuja suala la kutunga sheria ya fedha kama hii iliyoongeza mzigo wa kodi kwa wananchi. Mamlaka hayo yamewekwa kwa kiwango kikubwa mikononi mwa Rais kupitia Waziri wake mwenye dhamana.

Ninachofahamu mimi ni kwamba kodi hiyo ya simu iliingizwa kwa mara ya kwanza ndani ya ukumbi wa Bunge na Rais kupitia kwa Waziri wa Fedha aliposoma bajeti ya Serikali. Ilikuwepo kwenye Hotuba ya maandishi ya Waziri lakini wakati wa kusoma akaruka sehemu hiyo na kutangaza kwamba imefutwa.

Waziri wa Fedha aeleze katika hatua hiyo, wazo hilo lilitoka kwa nani mpaka likaingia katika kitabu cha hotuba yake na nini maamuzi ya Baraza la Mawaziri kwenye kikao kilichofanyika siku moja kabla ya yeye kusoma hotuba yake kilichojadili hatua za kikodi (tax measures).

Kifungu hiki kilirejeshwa kwa mara nyingine tena kwenye Muswada wa Sheria ya Fedha kupitia jedwali la Marekebisho lililowasilishwa na Waziri wa Fedha mwenyewe. Hivyo, ajitokeze na kueleza katika hatua hiyo, ni wabunge gani waliotaka kodi hiyo iingizwe katika muswada huo na sababu za Wizara ya Fedha kukubaliana nao.

Uzembe wa Bunge usitumike kama kisingizio cha kuficha udhaifu wa Serikali katika suala hili na mengine. Ni wazi, kuna uzembe pia kwa upande wa Bunge kwa kuacha mapendekezo ya wabunge wachache yageuzwe kinyemela kuwa ni msimamo wa wabunge wote bila ya kuwa na azimio la Bunge kuhusu mapendekezo hayo.

Katika mchango wangu bungeni kuhusu muswada huo, nilifanya rejea ya inayoitwa Kamati Ndogo ya Spika ya kupanua wigo wa mapato iliyoundwa kabla ya kuundwa kwa Kamati ya Bajeti; zote mbili zikiongozwa na Mh. Andrew Chenge (Mb).

Kamati hii ambayo haijawahi kuwasilisha ripoti yake Bungeni bali kwa Spika mwenyewe na hatimaye sasa ripoti kuwekwa kwenye maktaba ya Bunge, bila ya ripoti hiyo kuwasilishwa na kujadiliwa bungeni kama taarifa ya kamati au walau kuwekwa mezani kama hati rasmi ya Bunge; sasa inatumika kusukuma mzigo wa lawama kwa Bunge na wabunge.

Baada ya kamati hii, majadiliano kati ya Serikali na Kamati ya Bajeti yaliyofanyika kwa nyakati mbalimbali yanatumika kuhalalisha maamuzi ya Serikali yenye kuongeza mzigo wa gharama za maisha kwa wananchi katika hali yenye kudhihirisha uzembe wa Bunge wa kuachia mamlaka na madaraka yake kutumiwa visivyo.

Katika muktadha huu, kulaumiana kati ya Serikali na Wabunge au kulalamika kwa wananchi pekee hakutoshelezi kuwezesha uwajibikaji au mabadiliko yanayokusudiwa. Lawama ziendelee kwa kuwa zinasaidia kuendeleza mjadala na kufanya ukweli uoendelee kutolewa na pande zote. Malalamiko ya wananchi yaendelee kwa kuwa inawezesha Serikali na wabunge kutambua athari za maamuzi hayo kwa wananchi.

Tunapaswa kwenda mbele zaidi kwa wewe, mimi na mwingine kuchukua hatua? Wewe unapendekeza hatua gani zichukuliwe? Nitatoa msimamo wangu kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa baada ya kupata maoni yenu kwa kuniandikia kupitia mbungeubungo@gmail.com. Maslahi ya umma kwanza.

John Mnyika (Mb)
11/07/2013

Kwa heri wasomaji wangu mie nimeamua kujinyonga

Na Nyaronyo Mwita Kicheere
Mambo mengi yamefanyika nchi hii nikayapuuzia lakini hili la juzi limezidi kipimo nami siwezi kulivumilia kwa hiyo nitajinyonga tu ili kuondoa udhia.
Siko tayari kuendelea kutazama upuuzi huu, ushenzi huu, upumbavu huu, uhuni huu, uhayawani huu, umbumbumbu huu na unyang’au huu uliopindukia wa askari wetu kwenda Mtwara kupiga Wamakonde na kazi ya ulinzi wa ikulu yetu wakawaachia maaskari wa Marekani.
Nazungumzia kitendo cha askari wa Marekani kumsimamisha Waziri wetu wa Uwezekezaji, Bibi Mary Nagu, na kumkagua kabla haijaingia ikulu yetu ya Tanzania anakofanyia kazi rais wetu mpendwa kitendo ambacho kimenifanya niamue kujinyonga siku yoyote kuanzia leo.
Rais Baraka Obama
Nasema siwezi kukivumilia kitendo cha kihayawani kama hiki cha maaskari wa mabeberu wa Marekani kuja Tanzania kusimamia ulinzi wa Kilimanjaro Hotel alikolala rais wao Barack Obama na kufunga barabara ya Kivukoni kuzuia wakazi wa Kigamboni kwenda au kurudi kutoka mjini.
Yaani watu nchini mwetu tusiende mjini kununua nyama, tule mlenda na kisamvu eti kwa sababu Obama kalala Kilimanjaro Hoteli? Tunazuiwa kutembea barabarani nchini mwetu eti kwa sababu Wamarekani hawataki tupite karibu na alipo Rais wao?
Kitendo cha askari wa Marekani tena ambaye hana hata cheo cha ukoplo kumkagua waziri wetu, nchini mwetu, karibu na ikulu yetu, mbele ya maaskari wetu hakivumiliki na ndiyo maana nimeamua kujinyonga kwishilia mbali.
Nimeambiwa mawaziri wetu waliokaguliwa na maaskari wa Marekani nchini kwetu, wengine wakati wanakwenda ikulu yetu, kuhudhuria dhifa ya taifa iliyoandaliwa na Rais wetu, Jakaya Kikwete, kwa heshima ya mgeni wake, Rais wa Marekani Barack Obama, ni wengi na kwamba hakuna hata mmoja aliyekasirikia jambo hilo!
Wewe utavumilia kuwaona askari wenu wanapokea amri kutoka kwa wageni ndani ya nchi yenu? Eti askari private wa Marekani anatoa amri kwa askari wa Tanzania wenye vyeo mabegani? Sivumilii mimi kitendo hiki, bora nife kwa kamba ya katani.
Nimeshanunua kamba ya ukonge nimeificha mbali ili mke wangu Maritina na wanangu Nyagone, Mwita, Matinde, Robi, Tumaini na Bhoke wasije wakaiona na kuitilia mashaka wakaikata au kuichoma na kunizuia kujinyonga.
Miaka 50 baada ya uhuru mawaziri wetu wanashikwashikwa na Wamarekani wasiokuwa na vyeo begani wala ukoplo tu eti kwa sababu hawatuamini na wana mashaka na usalama wa Rais wao nchini, kwani ni lazima Obama aje kwetu Tanzania?
Askari wa Marekani wanawalazimisha Watanzania Waislamu kufungua mabegi yao na wanayanusisha na mbwa eti kuona kama kuna mabomu ndani yake! Laanakum yeyote aliyetoa amri mbwa wa Marekani kunusa nguo za dada zetu wawe makatoliki au Waislamu.
Kwani Wakenya ambao hawakutembelewa na Obama wamepungua nini? Kwa nini in the first place ziara za kipuuzi kama hizi ziandaliwe?
Kwani ni lazima tukubali kudhalilika mbele ya dunia nzima? Eti Obama ni rais wa dunia? So what? Kwani ni sisi tuliowatuma Wamarekani kuongopea dunia kuwa Saddam Hussein wa Iraq ana silaha za maangamizi na kumvamia mpaka leo wamejitengenezea maadui kila mahali?
Eti Wamarekani wana pesa, ni matajiri na wana nguvu za kijeshi! Kwa hiyo? Tudhalilike tu mbele ya walimwengu wote ili kumlinda Obama? Ni nani hasa aliyekubali mambo yooooote haya ya kihuni yafanyike na kutuondolea utu wetu ili kumfurahisha Obama?
Wallahi mie jua la kesho sitaliona. Mimi nitajinyonga tu nipishilie mbali wapuuzi waendeleze upuuzi wao. Siwezi kukubali upuuzi huu tunaofanyiwa Watanzania eti kwa sababu ya umaskini wetu, unyonge wetu, udhaifu wetu na upole wetu wa kipuuzi wa kufurahia ziara za kutupuuza.
Nasema haya huku nikijua fika kwamba kuna amri ya Waziri Mkuu wetu, Mizengo Pinda, inayowataka Polisi kutupiga kama tukikaidi jambo, nami nakaidi waziwazi jambo hili la serikali yetu kuwapeleka askari wetu Kusini kuwapiga Wamakonde, Wamwera, Wamakua na Wayao na kuwaacha skari wa Marekani wanawakagua wananchi Dar.
Bwana Mizengo Pinda usijihangaishe kutuma Polisi kuja kunipiga kwa kukaidi uhuni huu, upuuzi huu na uhayawani huu kwa sababu Polisi wako hawatanikuta badala yake watakuta kaburi langu. Tumechoka sisi raia kuliko mlivyochoka nyie serikali hadi ulinzi wa nchi mnawaachia wageni.
Nimekereka sana na sasa nasema nisilotaka kusema. Askari wa Marekani kanishika matako mimi eti ananikagua. Kweli mie mzee wa Kikurya nashikwa matako na haya majitu yaliyozoea kulambana madume kwa madume na majike kwa majike! Kweli ninayo heshima ya kuishi mie? Hapana najinyonga kesho.
Na hili silo pekee linalonifanya niamue kujinyonga. Yapo mengi ikiwa pamoja na hili lililoandikwa kwenye mtandao na mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Zuberi Kabwe, kwamba kampuni maarufu nchini ya mawakili ya Rex Attorneys eti ilithibitisha mkataba wa Dowans ili kampuni hiyo ipewe mkopo.
 
Kwa mujibu wa maelezo ya Zitto mtandaoni ni kwamba Novemba 2007 kampuni ya Dowans ilikwenda kukopa benki ya Stanbic dola za Marekani milioni 20 na kwamba benki hiyo ilipotaka ushauri wa kisheria kutoka kampuni ya REX Attorneys iliambiwa kuwa mkataba kati ya Tanesco na Dowans ni mzuri na uko sawasawa kabisa wapeni mkopo.
Kwamba July/August 2008 Tanesco waliiendea kampuni hiyo ya mawakili ya REX Attorneys kuomba ushauri wa kisheria kuhusu mkataba wa Dowans na Tanesco safari hii REX Arttorneys wakasema mkataba huo ni mbovu na haufai kabisa uuvunjeni kwa sababu hauna uhalali wowote. Tanesco wakaitika wakauvunja mkataba wake na Dowans.
 
Eti Dowans walipokwenda mahakamani kupinga kuvunjwa mkataba wao na Tanesco ukatolewa uamuzi wa kuiajiri kampuni maarufu ileile ya REX Attorneys kuiwakilisha Tanesco kwenye kesi ambapo ilishindwa kesi zote katika hatua zote!
 
Sasa mimi nitavumilia namna gani, eti niendelee kuishi huku naendelea kuona eti mtu kutoka REX Attorneys anateuliwa kuwa balozi wetu nje ya nchi? Kwa uendaji gani bora? Kwa manufaa ya nani? Na kwa kutaka kumridhisha nani? Mke wangu, wanangu na majirani kwa herini siwezi kuvumilia upuuzi huu.
 
Kama nilivumilia ya EPA, Deep Green, Meremeta, Twin Tower na Alex Stewart Assayers sipo tayari kuvumilia kushikwa matako na wageni wakati tuna polisi hata kama wana tuhuma za kurushia wapinzani mabomu na askari jeshi hata kama ni mabingwa wa kupiga raia basi angalhinda kesi walipwe dolaau wangeachwa ha[a dar wachache watukague siyo FBI, CIA na wahini wengine wa kigeni.
 
Kwa maelezo ya Zitto REX walilipwa dola za Marekani milioni 8 na Dowans walipwe dola za Marekani milioni 94! Bora nikafe kwa kamba ya mkonge kuliko kushuhudia haya tena katika wakati ambao vyombo vyetu vya dola vinapiga raia kwa amri ya Waziri Mkuu nasi wa dar tusiopigika tunashikwa matako na wageni wanaotukagua!
 
Mwisho mambo haya ya kihuni ya mabomu kulipuka mara kwa mara, askari kupiga raia Mtwara wakiacha askari wa kigeni wakikagua raia wetu, nchini kwetu, yanafanyika miaka 50 baada ya uhuru na baada ya majenerali Serakikya, Twalipo, Musuguri, Kyaro, Mboma na Waitara waondoke jeshini. Kwa nini? Wangekuwapo wangeruhusu tushikwe matako na Wamarekani wakitukagua? Kwa herini, najinyonga kesho, tukutane ahera.

Friday, July 12, 2013

CHADEMA Wamechelewa Kuchukua Uamuzi wa Kujilinda; Lakini Wako Sahihi



Freeman Mbowe kushoto na Dr. Wilbrod Slaa



Humu duniani kuna mambo mengi sana yanayopingana. Yapo ya kushangaza, yapo ya kuchukiza, yapo yanayokera na kuchefua roho, yapo ya kufurahisha na kuburudisha na yapo mengine ya vioja na vituko. Haya ya vioja na vituko wakati mwingine ndiyo hayo hayo ya kuudhi, kushangaza na kuchukiza kama siyo ya kukera na kuchefua roho vile vile. Mwitikio wa serikali ya Rais Kikwete na Chama cha Mapinduzi kufuatia uamuzi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo kutoa mafunzo ya kujilinda kwa chombo chake cha ulinzi na usalama wa chama – Brigedia Nyekundu – unaangukia kwenye hilo la mwisho.


Uamuzi wa CHADEMA umechelewa
Uamuzi wa CHADEMA kutoa mafunzo na kuchukua uamuzi wa kujihakikishia ulinzi wake yenyewe umechelewa sana. Uamuzi huu ulitakiwa uje kabla hata ya uchaguzi mkuu wa 2010 ambapo tulishuhudia vitendo mbalimbali ambavyo vilionesha wazi kuwa Jeshi la Polisi na vyombo vya usalama havikuwa tayari kuhakikisha usalama kwa CHADEMA kama vinavyofanya kwa Chama cha Mapinduzi.


Na tunaweza kusema umechelewa kwelikweli kwa sababu baada ya matukio ya Igunga kwenye uchaguzi mdogo kufuatia kujiuzulu kwa kashfa kwa Mbunge wa muda mrefu wa jimbo lile Rostam Aziz CHADEMA ilipaswa mara moja kujiangalia mfumo wake wa ulinzi na usalama wa viongozi wake na wanachama wake. Matukio mengine yaliyofuatia baadaye – ya Arusha, Mbeya, Tukuyu, Songea, Iringa na sehemu nyingine yalipaswa kuwa kichocheo tu cha kuharakisha kujichunguza huku na kuchukua hatua.


Ni Uamuzi unaoteteeka Kikatiba
Baadhi ya watu – hasa mashabiki wa CCM na wale wa Serikali –wameitikia kwa kusema kuwa uamuzi huu wa CDM unalingana na kuunda jeshi kitu ambacho Kikatiba hakiruhusiwi isipokuwa kwa serikali tu. Wanafanya hivi kwa kunukuu Ibara ya 146 ya Katiba ambayo inasema katika kifungu chake cha kwanza kuwa “Ni marufuku kwa mtu yoyote au shirika lolote au kikundi chochote cha watu, isipokuwa Serikali kuunda au kuweka Tanzania jeshi la aina yoyote.”
Haiitaji uelewa mkubwa kutambua kuwa Ibara hiyo ya Katiba haikatazi kuundwa kwa makampuni ya ulinzi, vikundi vya ulinzi wa jadi, au hata vikundi vya ulinzi vya vyama vya siasa, makanisa, misikiti n.k. Kinachokatazwa ni kuundwa kwa jeshi (army) kwa maana ya chombo cha kivita. Kwa sababu tukikubali tafsiri finyu ya Ibara hiyo itabidi serikali itoe maelezo ya kutosha ya kwanini kuna makampuni mbalimbali ya ulinzi nchini ambayo yamesajiliwa na mengine yanabeba silaha za moto kabisa. Yapo makampuni makubwa kama KK Security, Knight Support, Bison Security, Dragon Security Services, Group 4 Security Ltd, Securex Tanzania, Aurora Security Tanzania, na Warrior Security –nikitaja machache – ambayo yote yanatoa huduma mbalimbali za ulinzi na usalama. Baadhi ya makampuni haya yameanzishwa na watu waliowahi kuwa wanajeshi na wengine wametumikia majeshi yetu katika ngazi mbalimbali.




Mkuu wa Kampuni ya Warrior Security akitembelea maafisa wake



Na tunaweza pia kuangalia kwa namna nyingine na kuona kwanini hoja ya serikali kupinga CHADEMA kujilinda haina mashiko, ya kipuuzi na yenye kuonesha kuchanganyikiwa kusiko na sababu tunaweza kuangalia eneo jingine ambalo tunaweza kulifananisha zaidi na CDHADEMA. Wengi wetu tumewahi kuhudhurudia hafla mbalimbali na burudani mbalimbali ambapo tunawakuta watu wanaoitwa “mabouncer” yaani walinzi wa milangoni. Iwe kwenye matamasha ya muziki, mikutano ya kidini au makusanyiko makubwa watu waliovaa tsheti za “Security” au “Staff” wanaonekana wakitoa ulinzi. Wote hawa wanafanya kile ambacho tunaweza kwa kabisa kukiita “kujilinda” yaani siyo tu wanalinda watu waliopo pale lakini pia wanalinda maslahi ya watu walioandaa tamasha au shughuli hiyo. Sasa je hawa nao wanavunja Katiba kwa kuamua “kujilinda”?


Na ukiangalia baadhi ya makampuni haya yamejipanga na yanafanya kama kama majeshi. Wanavaa sare na wengine wana nyenzo zinazokaribiana kabisa na zile za vyombo vya kijeshi; lakini hatujasikia serikali ikisema kuwa “vimeanzisha majeshi kinyume na Katiba”! Picha za hapa chini zinadokeza uwepo wa vikundi vya kujilinda (makampuni) ambavyo havijaanzishwa na serikali na hoja inaweza kujengwa kuwa vinakiuka Katiba.



Nafasi ya Polisi katika Kujilinda
Sasa, sote tunatambua kuwa uwepo wa makampuni mbalimbali ya ulinzi au vikundi mbalimbali vya kujilinda haina maana kuwa polisi hawawezi kuhusika au hawatakiwi kuwepo; na haina maana kabisa kuwa watu wanaofanya shughuli ya kujilinda wamejipa majukumu ya polisi. Ukweli rahisi kuona ni kuwa polisi kama chombo cha umma kina watumishi wachache, ambao hawawezi kuwepo mahali pote wakati wote kuhakikisha ulinzi na usalama. Hivyo katika kile ambacho kinatambulikana kama “ulinzi shirikishi” watu na makundi ya watu yanapofanya shughuli mbalimbali za kujilinda wanasaidia polisi kuhakikisha usalama na badala ya kuwakataza watu hao kufanya hivyo jeshi la polisi linatakiwa kuwapongeza na kuhakikisha kuwapatia msaada wakati unapohitajika.


Mazingira ya Sasa yanalazimisha CDM kujilinda
Kama nilivyodokeza hapo juu CHADEMA imechelewa kuchukua uamuzi wa kuanza kujilinda hasa katika mazingira ambayo vyombo vya dola viko dhidi yake. Katiba inampa kila Mtanzania haki ya “kulinda, kuhifadhi, na kudumisha uhuru, mamlaka, ardhi na umoja wa taifa”. Matukio ya mashambulizi dhidi ya CHADEMA na viongozi wake yanatishia umoja wa taifa na hivyo wana CHADEMA kama Watanzania wengine wanaitwa kulinda na kuhifadhi umoja huu kwa kuhakikisha kuwa matukio kama haya hayajirudii tena kwenye mikutano yao. Jukumu hili la kulinda halihitaji kibali cha Rais, Jaji Mkuu, Mwanasheria au Kiongozi wa juu wa CCM; ni jukumu ambalo kila Mtanzania analo na anapaswa kujitambua kuwa analo.
Mauaji ambayo yamekuwa yakitokea kwenye mikutano ya CHADEMA karibu yote hadi hivi sasa yamehusishwa na polisi – watu waliopaswa kutoa ulinzi. Na ushahidi wote unaonesha kuwa Jeshi la Polisi halijabadili mtazamo wake wa utendaji na linaendelea kuangalia CHADEMA kama chama cha waleta vurugu na hivyo limejiandaa mara zote kuingilia kati kuleta usalama. Na uamuzi wa Rais Kikwete kuwapongeza na kuwapandisha vyeo baadhi ya maofisa ambao wanatajwa kuhusika na mitazamo hii hasi ndani ya jeshi la polisi ni uthibitisho dhahiri kuwa CHADEMA hawawezi – na watakuwa wapumbavu – kutegemea ulinzi wa polisi. Maana kama polisi wanapotoa ulinzi ndio yanatokea mauaji itakuwaje kama hawatoi!?


CDM Iandae mpango mzuri wa kujilinda
Kwa vile CHADEMA wamesema wanataka kutoa mafunzo ya ukakamavu kwa vijana ili kusaidia kujilinda kwa kupitia makambi nchini pote hatari ya hili ni kuwa kama CCM na makambi yake. Tayari wananchi wanajua kile kinachozalishwa kutoka makambi ya CCM, CHADEMA haipaswi kuiga hilo. Kwa vile lengo la CHADEMA ni kuhakikisha kuwa inajilinda na kulinda wanachama, mali na viongozi wake basi mpango wake wa kujilinda hauwezi na haupaswi kuwa kama wa CCM au unaoshabihiana na ule wa CCM kwa namna yoyote ile; hatutaki CHADEMA ifanane na CCM maana ikifanana na CCM haitakuwa tofauti na CCM na watu wanachotaka ni tofauti na hasa kama ni tofauti nzuri na bora.



Hivyo, CHADEMA wasiwe kama wana –beep – tu na kutishia bali wajipange vizuri na wawaeleze wanachama na Watanzania mpango huu na utekelezaji wake; hakuna kambi za siri au mafunzo ambayo yataweza kutafsiriwa kama kujiandaa kulipa kisasi.


Jeshi la Polisi na Serikali Wajiulize Wametufikisha Vipi Hapa?
Badala ya kuipiga mikwara CHADEMA na kuwatishia viongozi wake uongozi wa jeshi la polisi na Ikulu inapaswa wawe na ujasiri wa kusimama mbele ya vioo na kujiuliza maswali ambayo majibu yake yagonge visogo vyao. Maswali hayo baadhi yake ni haya:
a. Kwanini CHADEMA imefikia mahali pa kutaka kujilinda?
b. Vyombo vya usalama vimepungukiwa nini kiasi kwamba chama kikuu cha upinzani nchini haiviamini?
c. Je, uongozi wa vyombo vya usalama una mahusiano gani ya kikazi na viongozi wa CHADEMA?
d. Je, ni kwanini matukio yaliyotokea na kugusa CHADEMA hayachunguzwi kwa kasi ile ile kama matukio mengine – mfano mauaji ya Padre Mushi kule Zanzibar yamepewa uzito wa uchunguzi (Hadi Rais kaingilia kati) kuliko mauaji ya mtoto mdogo Arusha?
e. Je vyombo vya usalama vinaweza kuchukua hatua gani kurudisha imani ya CHADEMA na wanachama wake kuwa vinafanya kazi kwa weledi na siyo kama sasa ambavyo vimebatizwa majina ya CCM kama PoliCCM (badala ya Polisi), na TICCM (Badala ya TISS) n.k?
f. Rais Kikwete ajiulize kwanini wale aliowakabidhi dhamana ya kusimamia usalama nchini wameifikisha nchi hapa – kuwalaumu CHADEMA kwa kujilinda ni kukosa umakini na kuwa na usahaulifu unaobagua (selective amnesia).


Cheo cha Kamisaa wa Polisi Kirejeshwe
Lakini kubwa zaidi naamini wakati umefika kwa Jeshi la Polisi kufikiria kurejesha cheo cha Kamisaa wa Polisi (Police Commissar) ambaye atashughulikia masuala ya vyama vya siasa kwenye mkoa au wilaya ya kipolisi. Afisa huyo wa ngazi za juu (Mkoani asiwe chini ya Mrakibu Mwandamizi wa Polisi na Wilayani si chini ya Mrakibu Msaidizi wa Polisi) ndiye atakuwa ni ni kiungo kati ya vyama vya siasa na jeshi la polisi katika eneo lake na ndio atawajibika kusimamia masuala ya ulinzi na usalama katika eneo lake hili na kwa kwa kushirikiana na Mkuu wa Polisi wa eneo atawajibika kwa yote yanayotokea au kupaswa kutokea kuhusiana na ulinzi na usalama wa mambo ya kisiasa mkoani.


Mwisho
Haki ya kujilinda ni miongoni mwa haki za msingi kabisa za binadamu ambazo zinatokana na mtu kuwa binadamu na haziwezi kuondolewa au kufutwa na chombo chochote. Ni haki ambayo mwanadamu anayo kwa kuzaliwa kwake. Haki hii kwa kadiri tunavyokua tunaiacha kwenye vyombo mbalimbali lakini mwisho wa siku bado ni haki yetu ya msingi kama binadamu. Mwanadamu anaposhambuliwa ana haki ya kujikinga kukinga maisha yake na mali yake; na kama ni familia yake inashambuliwa ana haki ya kulinda familia yake. Huwezi kumwambia mtu kuwa akipigwa ainame na kukubali kipigo bila kujilinda.


Haki hii ni tofauti na haki ya kujitetea au kulipiza kisasi – japo ni haki zinazoendana pamoja katika ile haki ya msingi ya kutokudhulumiwa. Haki ya kujilinda ni haki ambayo mtu si lazima alipe kisasi lakini ni haki ya kuzuia kutendewa vibaya. Hii ndiyo sababu watu wamejenga kuta kwenye nyumba zao, wameweka vyombo vya ulinzi na kuajiri walinzi. Wote hawa wanatumia haki yao ya kujilinda bila kulazimika kulipa kisasi. CHADEMA kama chama cha siasa ambacho tayari kimeshadhurika mara kadhaa sasa na kwa niaba ya wanachama wake kimeamua kutoa mafunzo ya ukakamavu na kujilinda; wanatumia haki hii ya msingi.


Jeshi la Polisi na vyombo vya usalama na wale wote wanaobeza wanahitaji kutafakari upya kama wao wangekuwa upande wa pili kama wasingetafuta mbinu ya kujilinda. Kama wale watu waliowekwa kutoa ulinzi ndio hao hao wanaoharibu ulinzi utakuwa ni ujinga wa hali ya juu kuwategemea. Bila mabadiliko ya msingi ya mfumo na utendaji wa jeshi la polisi katika mazingira ya vyama vingi vya siasa ni vigumu kwa chama cha upinzani kama CHADEMA kuweka maisha yake na maisha ya viongozi wake mikononi mwa chombo hicho. Ni wajibu na ni haki kwa wao kufikiri namna ya kujilinda na kulinda maslahi yake. Hili halihitaji baraka kutoka CCM, Ikulu, au Polisi.
Na kama nilivyosema, ni jambo ambalo limechelewa.


Niandikie: mwanakijiji@jamiiforums.com