Search This Blog

Sunday, June 9, 2013

Ngono kwa njia ya mdomo husababisha saratani

Saratani imeendelea kuwa tishio hapa nchini huku hofu ikiendelea kuikumba jamii kutokana na wataalamu wa afya kushindwa kufahamu tiba halisi ya maradhi hayo hatari.
Takwimu kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road zinaonyesha ongezeko la saratani ya mdomo na koo kwa kiasi kikubwa kutoka kesi 167 mwaka 2006 hadi 277 mwaka 2012.
Mkurugenzi wa Idara ya Kinga Ocean road, Julius Mwaiselage anaeleza kuwa watanzania wasipende kuiga mambo ambayo si sahihi bila kujua madhara yake kama kufanya mapenzi kwa njia ya mdomo. “Saratani ya mdomo ipo, na nyingine zinasababishwa na zinaa “ anasema Dk Mwaiselage
Mdomo ukliwa umeathiriwa na bakteria kufuatia kutumiwa kama njia ya  kufanya mapenzi 
Tafiti mbalimbali zimewahi kufanyika nchini na kubaini kuwepo kwa ongezeko la saratani ya mdomo.Utafiti uliofanywa na Dk Innocent Mosha wa Kitengo cha Patholojia cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), umebaini aina za saratani 1,594, kati ya hizo 509 zikiwa ni za midomo kwa mwaka 2003 pekee.
Matokeo hayo yanaonyesha kuwa kati ya saratani 509 za mdomo, saratani 242 zilisababishwa na Virusi vya Human Papiloma ambavyo hutokana na zinaa.
“Ninachojua mimi ni kuwa Virusi vya HPV husababishwa na magonjwa ya zinaa, hivyo mtu anayeugua saratani ya aina hiyo, imetokana na zinaa,” anasema Dk Mosha.
Takwimu hizo ni zile zilizopatikana kwa watu waliokwenda kufanyiwa uchunguzi katika Mkoa wa Dar es Salaam pekee.
Dk Mosha anasema kuwa wanaume ndiyo huathiriwa zaidi na saratani ya mdomo ambapo kwa hapa nchini, asilimia 53 ya wanaume waliofika MNH kwa ajili ya vipimo, walibainika kuugua saratani hiyo, huku wanawake wakiwa ni asilimia 47.
Utafiti kama huo ulifanywa pia na Dk Amos Mwakigonja, mkuu wa Idara ya Patholojia katika Chuo Kikuu cha Tiba cha Muhimbili (MUHAS).
Dk Mwakigonja alifanya utafiti wa saratani ya mdomo aina ya Kaposi’s Sarcoma ambapo wagonjwa 78 walibainika na saratani hiyo kuanzia mwaka 1990 hadi 2003. “Saratani za mdomo zipo za aina nyingi na zimetofautiana kulingana na visababishi vyake,” anasema Dk Mwakigonja.
Katika utafiti wake Dk Mwakigonja alibaini kuwa wanawake wengi walikuwa na saratani ya mdomo aina ya Kaposi’s Sarcoma kuliko wanaume.
Hata hivyo, utafiti huo ulionyesha kuwa asilimia 50 ya wanaume walikuwa na saratani ya mdomo hatari zaidi (systemic) kuliko wanawake ambao ni asilimia 37.

Mapenzi kwa mdomo husababisha maradhi
Dk Mwakigonja anasema kuwa mapenzi yoyote kwa njia ya mdomo lazima yasababishe maradhi ya zinaa iwapo mmoja ameambukizwa.
Pia anasema kwamba sampuli nyingi za wanaume wanaojihusisha na mapenzi na wanaume wenzao (mashoga) zilibainika na saratani ya mdomo.
Utafiti huo ni sehemu ya utafiti wa Shahada ya Uzamivu ambao ulionyesha kuwa wagonjwa wengi wa saratani ya mdomo walikuwa ni wanaume wenye umri wa miaka kati ya 38 na kuendelea na wanawake ni 31.
Ufatiti wa WHO Tanzania
Shirika la Afya Duniani (WHO) pia lilifanya utafiti mwaka 2010 nchini kwa kushirikiana na Kituo cha Taarifa za HPV, ambapo ilibainika kuwa asilimia 20 ya saratani za koo na mdomo nchini zinasababishwa na ufanyaji wa mapenzi kwa njia ya mdomo.
Taarifa hizo za WHO zinaeleza kuwa wanaume 747 hugundulika na saratani ya mdomo kila mwaka wakati wanawake 472 hubainika na saratani hiyo pia.
Wakati huohuo, wanaume wanaopoteza maisha kutokana na saratani hiyo ni 444, kwa mwaka na wanawake ni 270, kwa mwaka.
Utafiti wa WHO umebaini kuwa saratani ya mdomo inashika nafasi ya sita katika aina 24 za saratani 24 zinazoisumbua zaidi Tanzania.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa wanaume wanaoathirika zaidi ni wenye umri wa kati ya miaka 15 na 55, ambao tayari wameshaanza kujihusisha na ngono.
Kama maradhi mengine ya kuambukiza, Virusi vya HPV huambukizwa kwa urahisi zaidi kutoka kwa wanawake kwenda kwa wanaume kuliko kutoka kwa wanaume kwenda kwa wanawake.
Utafiti huo uliodhaminiwa na mfuko wa Bill na Melinda Gates na Kituo cha Saratani na Mpango wa Utafiti wa Taasisi ya ICO unaeleza kuwa mitandao ya kijamii na picha za ngono ndiyo chanzo cha watu wengi kuiga ufanyaji wa mapenzi ya aina hiyo.
Kwa mujibu wa gazeti la The New York Times, tafiti zimefanyika na kubaini kuwa asilimia 70 ya wagonjwa wanaobainika na saratani ya koo na mdomo duniani, husababishwa na Virusi vya Human Pappiloma vinavyotokana na magonjwa ya zinaa.
Tafiti hizo zinaonyesha kuwa wagonjwa wengi wanaogundulika na saratani hiyo ni wanaume wenye umri wa kati, wenye uwezo wa kifedha, wasiovuta sigara wala siyo walevi waliokubuhu.
Utafiti huo ulibaini kuwa wanaume wapo hatarini zaidi kupata saratani ya koo inayosababishwa na Virusi vya HPV.
Miaka ya 80, idadi ndogo ya watu waliougua saratani ya koo walihusishwa na maambukizi ya Virusi vya HPV. Kihistoria, watu waliobainika na ugonjwa huo, ni wenye umri wa miaka 70 kwenda juu ambao walikuwa ni wale walevi waliokubuhu na wavuta sigara.
Ilielezwa kuwa Virusi vya HPV vipo kwa wingi kiasi ambacho watu wazima wanaojihusisha na ngono ya aina yeyote ile, huweza kupata maambukizi ya zinaa hata kama siyo saratani.
Hata hivyo ilibainishwa kuwa saratani isababishwayo na virusi vya HPV ni rahisi kuitibu kuliko saratani ya koo isababishwayo na tumbaku au pombe kali.
Virusi vya HPV ni nini?
Kwa jina la jumla, saratani ya koo au mdomo huitwa saratani ya kichwa na shingo. (Neck and Head Cancer)
HPV ni miongoni mwa virusi hatari zaidi duniani visababishwavyo na magonjwa ya zinaa na vinaweza kuathiri sehemu mbalimbali za mwili.
Zipo aina zaidi ya 120 za HPV, baadhi huweza kuzalisha usugu (warts) ambazo si saratani katika sehemu za siri, mikononi na miguuni.
Maambukizi ya HPV hufanyika kwa urahisi, hata kwa kugusana ngozi au majimaji, huku maambukizi mengine yakisababishwa na ngono.

Virusi hatari na vinavyosababisha saratani ni HPV-16, HPV-18, HPV-31 na HPV 45.
Aina hii ya Virusi vya HPV husababisha saratani ambapo uvimbe waweza kujitokeza kwa ndani na unaweza usionekane ukilinganisha na vivimbe vingine vya saratani.
Wataalamu wanasema HPV-16 na HPV-18 inahusishwa zaidi na saratani ya shingo ya kizazi na endapo mapenzi kwa njia ya mdomo yatafanywa na mtu mwenye uambukizo huu ni rahisi kuambukizwa.
Source:  http://www.mwananchi.co.tz/habari/Ngono-kwa-njia-ya-mdomo-husababisha-saratani/-/1597578/1876252/-/y3laqcz/-/index.html

Mbunge CCM mbaroni vurugu za gesi Mtwara

Jeshi la Polisi mkoani Mtwara limemkamata mbunge wa Mtwara Mjini (CCM), Hasnain Murji likimtuhumu kuchochea vurugu za kupinga mradi wa bomba la gesi kutoka mkoani humo kwenda jijini Dar es Salaam.
Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Msemaji wa Jeshi la polisi nchini, Advera Senso zinaeleza kuwa Murji alikamatwa jana jioni nyumbani kwake maeneo ya Shangani mjini Mtwara.
Mbunge wa Mtwara Mjini (CCM) Hasnain Murji
Kukamatwa kwa mbunge huyo kunakuja ikiwa zimepita siku tano tangu viongozi wanne wa vyama vya upinzani mkoani Mtwara, kufikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Juni 4, mwaka huu wakikabiliwa na mashtaka matatu ikiwamo kula njama, kufanya uchochezi na kuamsha hisia mbaya kwa wakazi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Washtakiwa hao ni Katani Ahmed Katani (33) na Saidi Kulaga (45) wa CUF, Hassan Uledi (35) wa NCCR Mageuzi na Hamza Licheta (51) wa TLP, wote wakazi wa Mtwara. Taarifa zaidi zilieleza kuwa baada ya polisi kumkamata mbunge huyo, walifanya upekuzi katika nyumba yake kwa saa kadhaa na baada ya kujiridhisha walikwenda kupekua na ofisi yake.
“Amekamatwa kwenye saa 11:00 jioni, hata hati ya kukamatwa kwake imeeleza kuwa anatuhumiwa kuchochea vurugu za kupinga gesi inayopatikana mkoani Mtwara kwenda Dar es Salaam,” alisema Katibu wa Mbunge huyo, Meckland Millanzi.
Katika ufafanuzi wake Senso alisema kukamatwa kwa mbunge huyo ni jambo la kawaida na kwamba hivi sasa unaandaliwa utaratibu ili faili lake lipelekwe kwa Mwanasheria wa Serikali.
“Acheni polisi ifanye kazi yake kama kutakuwa na la ziada tutawaeleza ila kwa sasa tunaandaa utaratibu wa suala hili kwenda kwa mwanasheria wa Serikali,” alisema Senso. Murji amekamatwa ikiwa zimepita siku 16 tangu kutokea vurugu kubwa mkoani Mtwara zilizodumu kwa siku mbili, ambapo polisi walipambana na makundi ya vijana wanaopinga mradi wa bomba la gesi kujengwa.
Vurugu hizo zilizosababisha baadhi ya watu kupoteza maisha huku wengine wakiachwa majeruhi na mali nyingi kuharibiwa, ziliibuka baada ya hotuba ya bajeti ya wizara ya nishati na madini kusomwa bungeni .
Mvutano kuhusu mradi wa bomba la gesi ulianza Novemba 16, mwaka jana baada ya Serikali kutuma kamati inayoratibu maoni ya sera ya gesi “The Natural Gas Policy of Tanzania -2013” ambayo ilifika mkoani Mtwara kukusanya maoni ya wananchi.
Katika mikutano yake mjini Mtwara, wananchi wengi hawakukubaliana na wazo la kusafirishwa gesi nje ya Mtwara kwa njia ya bomba. Hali hiyo ndiyo iliyowasukuma viongozi wa vyama kuhamasisha wananchi kuhusu suala hilo.
Source:  http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Mbunge-CCM-mbaroni-vurugu-za-gesi-Mtwara/-/1597296/1876684/-/r4t0bbz/-/index.html

Wednesday, June 5, 2013

HIVI NDIVYO WANAVYONG'OA MENO KWA KOLEO: ANGALIA VIDEO

Kwa kipindi sasa nchi yetu imekuwa ikigubikwa na matukio ya vitendo vya Kialifu kama vile vya ung'oaji wa Kucha na Meno bila ya kutumia Sindano ya Ganzi. Vitendo hivi vimewakuta baadhi ya watu hapa nchini akiwemo Dk. Stepehen Ulimboka, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Absalom Kibanda.
Video hii unaonyesha moja ya njia ambazo zinatumika KUNG'OA MENO bila ya ganzi.

MUHIMU: Hii ni picha ya Video yenye kusikitisha na kuumiza sana, tafadhari tunaomba kama una roho nyepesi usiangalie Video hii.


Saturday, June 1, 2013

UTATA KIFO CHA AFISA USALAMA KIJITONYAMA

Utata umeibuka kuhusiana na kifo cha Ofisa Usalama wa Taifa, Peter Tyenyi, ambaye mwili wake umekutwa ndani ya kisima cha maji kilichopo eneo la ofisi za idara zilizopo Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kwa njia ya simu, msemaji wa familia ambaye ni kaka wa marehemu, John Tyenyi alisema mwili wa Peter (53) ulikutwa juzi ukiwa ndani ya kisima cha maji kilicho ndani ya eneo la Ofisi za Usalama wa Taifa, Kijitonyama baada ya kutoweka tangu Jumatatu ya Mei 27, alipoaga kwenda kazini.
“Peter alitoweka tangu Jumatatu alipoaga kwenda kazini. Mimi nimepigiwa simu jana saa tano asubuhi nikiwa Mombasa nchini Kenya kwamba amepatikana akiwa ndani ya shimo la maji,” alisema John.
Baadhi ya ndugu zake waliozungumza kwa sharti la kutotajwa majina wakiwa msibani Kigamboni jijini Dar es Salaam, walisema kuwa baada ya ndugu yao kutoweka mkewe Joyce Mwakilama aliwataarifu na kuwasiliana na ofisi yake, lakini aliambiwa kuwa hata huko hayupo.
“Tuliwajulisha Usalama wa Taifa wakasema hata wao hawajui. Lakini jana (juzi) wakatupigia simu kuwa amekutwa kwenye kisima cha maji baada ya kutokea shida ya maji,” alisema mmoja wa wanafamilia kwa sharti la kutotajwa jina na kuongeza:
“Walisema kuwa kisima hicho huwa kinalindwa, lakini tunashangaa ndugu yetu aliingiaje humo.”
Ndugu mwingine alisema: “Awali tuliambiwa kuwa ndugu yetu yuko Muhimbili, tukaenda kuulizia tukamkosa. Baadaye tukaambiwa yuko hospitali ya Lugalo, huko tukamkuta ameshaandaliwa kwa mazishi. Tulipouliza tukaambiwa kibali cha kuzika kiko tayari na usafiri wa ndege uko tayari tujiandae kusafirisha.”
Hata hivyo, msemaji wa familia John Tyeni alisema kuwa ndugu hao walipinga kuusafirisha mwili huo, hadi ufanyiwe uchunguzi (post mortem).
Mkurugenzi Usalama wa Taifa katikakati
“Tulipokwenda hospitali tukakuta maofisa usalama wamemchukua OCD wa Wilaya ya Kinondoni Wilbrod Mutangungwa na askari wawili na kwenda kufanya post mortem. Yaani kulikuwa na ujanja ujanja unafanyika. Sisi tukamchukua Ofisa Upelelezi Mkoa wa Kinondoni, RCO Kimola na askari wawili na wapigapicha ndiyo tukafanya post mortem,” alisema John.
Akizungumzia matokeo ya uchunguzi huo, John alisema kuwa watapewa matokeo hayo baada ya kutoka kwenye mazishi yatakayofanyika Musoma mjini mkoani Mara, baada ya kusafirishwa leo.
Hata hivyo alisema kuwa macho yake yalikuwa yametoka nje kwa sababu ya kujaa maji.
Baadhi ya ndugu wa marehemu walidai kuwa mwili wake ulikutwa ukiwa umetumbuliwa macho huku nguo na viatu vikiwa bado mwilini.
Akizungumzia kifo hicho, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela alikiri kutokea tukio hilo na kusema kuwa bado uchunguzi unaendelea.
“Ni kweli kuna ofisa usalama amefariki ndani ya kisima, lakini bado tunachunguza. Kwa sababu itabidi tupate taarifa ya daktari ndiyo tuunganishe na uchunguzi wetu,” alisema Kenyela.
SOURCE: http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kifo-cha-Ofisa-Usalama-chazua-utata/-/1597578/1868848/-/ahqc99/-/index.html