Search This Blog

Thursday, May 30, 2013

TAARIFA YA UCHUGUZI JUU YA KUTEKWA NA KUUMIZWA KWA ABSALOM KIBANDA

IMEWASILISHWA NYUMBANI HOTEL - TANGA MEI 30, 2013

UTANGULIZI:

Usiku wa Jumanne ya Machi 5 kuamkia Machi 6, 2013, Mhariri Mtendaji wa New Habari (2006) Ltd, ambaye pia Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda alivamiwa na kujeruhiwa vibaya akiwa nje ya lango la kuingilia nyumbani kwake Mbezi Juu, Dar es Salaam.

Tukio hilo liliishtua na kutikisa taifa kwa kiwango kikubwa si tu katika tasnia ya habari nchini, bali pia jamii kwa ujumla hasa baada ya aina ya utekaji, utesaji na usiri uliotumika katika kufanikisha uhalifu huu kufanana kwa karibu na tukio lilomkuta Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madkatari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka lililotokea karibu miezi tisa kabla ya tukio la Kibanda yaani, usiku wa Juni 26, 2012.Ukiacha matukio hayo, miezi sita kabla ya Kibanda kutekwa na kuteswa Mwandishi Daudi Mwangosi, aliuawa akiwa mikononi mwa vyombo vya dola Septemba 2, 2012 huko Nyololo, Iringa akiwa kazini.Tukio la Kibanda limekuwa na sura ya mwendelezo wa mauaji au utesaji wa wanahabari, hasa ikitiliwa maanani kuwa Mwandishi Issa Ngumba (45) wa Radio Kwizera aliyekuwa anafanyia kazi zake katika Wilaya ya Kakonko, Kigoma, Januari mwaka huu, alipigwa risasi na kuuawa katika mazingira ya kutatanisha. Kama hiyo haitoshi, tukio la kutekwa na kudhuriwa kwa Kibanda limetokea mwezi mmoja tu baada ya Mwandishi wa Gazeti la Tanzania Daima, Shaaban Matutu kupigwa risasi na polisi akiwa nyumbani kwake Dar es Salaam kwa maelezo kuwa kimakosa polisi walidhani Matutu ni jambazi.

Mazingira ya kutekwa na kuumizwa kwa Kibanda yalitia wasiwasi kuwa upo uwezekano, na dalili zilionyesha kwamba waliofanya kitendo hicho cha kinyama hawakuwa wezi wala majambazi kutokana na ukweli kwamba licha ya kuwa na fedha zipatazo shilingi milioni tatu taslimu ndani ya gari, laptop, simu tatu za gharama (ipad, iphone na Blackberry), watekaji hawa hawakuchukua chochote baada ya kukamilisha uhalifu wao.

Kibanda aliumizwa kwa kiwango kikubwa. Alitobolewa jicho la kushoto, akaumizwa vibaya kichwani kiasi cha kusababisha kuvunjika kwa baadhi ya mifupa ya kichwa. Aling’olewa meno mawili na kucha mbili, tena bila gazi. Watekaji hawa, katika unyama wa ajabu kabisa, walimkata pingiri ya kidole cha pete chini ya kucha na kuondokana nayo.Hali hiyo iliibua maswali mengi, watu wengi wakajiuliza na kutafuta sababu za kutekwa na kuumizwa kwa Kibanda kiasi hiki. Kutokana na kuwapo kwa maelezo mengi yanayotofautiana kuhusu tukio hilo, ikabidi Jukwaa la Wahariri Tanzania lifanye uamuzi.Katika kikao cha Machi 8, 2013 Jukwaa la Wahariri Tanzania liliunda TIMU ya watu watano na kuipa hadidu rejea za kufanya uchunguzi wa kihabari juu ya shambulio hilo kubaini limetokana na nini.Timu hiyo iliundwa kufuatia uamuzi wa Jukwaa la Wahariri kufanya uchunguzi huo na baada ya kukubalika kwa ombi la ruzuku ya kufanya uchunguzi huo wa kihabari kutoka Mfuko wa Vyombo Vya Habari Tanzania (TMF). Ruzuku ya TMF ililenga kiujumla kutumia tukio la Kibanda kuwa chanzo cha kutengeneza mazingira salama zaidi kwa waandishi na wahariri na kwamba kiwango cha matukio ya kuteswa, kupigwa na kuuawa kwa waandishi yanapungua kila mwaka. Timu hii imefanya kazi usiku na mchana kwa kwa zaidi ya mwezi. Timu imezungumza na wadau 26. Kati ya hawa yumo Kibanda mwenyewe, mke wake, ndugu zake, wasaidizi wake, waajiri wake wa zamani na wa sasa, viongozi wa kisiasa na vyombo vya dola kutafuta ukweli wa jambo hili. Pia tumesoma matamko na habari zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii na magazeti ya kati ya Machi 5, 2012 na Aprili 5, 2012 kwa nia ya kufanya ulinganishi wa taarifa tulizozipata kutokana na uchunguzi na habari zilizochapishwa baada ya kutekwa kwake.Vyombo vya dola akiwamo Waziri mwenye dhamana walikataa kuhojiwa wakisema kuna tume ya serikali inayofanya kazi hiyo na kwamba kuhojiwa kungeonyesha kutokuwa na imani na tume hiyo.Leo tunawasilisha muhtasari wa ripoti hii. Ripoti kubwa pamoja na viambatanisho vyake, itachapishwa na kuwekwa katika kitabu kimoja. Utaratibu mwingine wa kuchapisha habari ambazo hazijachapishwa kuhusiana na tukio hili (untold stories) pia utaandaliwa kwa ushirikiano na Jukwaa la Wahariri kwa nia ya kuieleza jamii maajabu juu ya kadhia hii.Tulipewa Hadidu Rejea ziafuatazo:

HADIDU REJEA:1. Kuchunguza mazingira ya kabla na baada ya tukio la kushambuliwa kwake. Kabla ya kushambuliwa kwa maana ya kufahamu kama kulikuwa na viashiria vyovyote vinavyoelekea kuwapo kwa mipango ya mashambulizi dhidi yake.2. Kuchunguza mazingira ya tukio lenyewe kwa kujikitika katika mwenendo wake hasa siku nzima ya Jumanne Machi 5, 2013.3. Kuangalia mazingira ya kazi ndani ya Kampuni ya New Habari (2006), Ltd na nje ya kampuni hiyo kwa kumulika sababu za kuhama kwake kutoka Free Media mwishoni mwa mwaka jana na kuhamia New Habari.4. Kuchunguza jambo jingine lolote linaloweza kutoa mwanga wa sababu za kuvamiwa na kupigwa kwa Kibanda.5. Kuchunguza mazingira ya sasa ya kazi kwa wanahabari na kupendekeza hatua za kuchukua kutokana na kile kitakachobainika

YALIYOJIRI KATIKA UCHUNGUZI:1.0. Kuchunguza mazingira ya kabla na baada ya tukio la kushambuliwa kwake. Kabla ya kushambuliwa kwa maana ya kufahamu kama kulikuwa na viashiria vyovyote vinavyoelekea kuwapo kwa mipango ya mashambulizi dhidi yake.Timu ya uchunguzi ilitumia muda mwingi katika eneo hili, kubaini iwapo kulikuwapo viashiria, sababu au matukio ya wazi yenye mwelekeo wa kujitokeza kwa shambulio hili. Tuliangalia pia iwapo wapo watu au makundi yaliyokwishapata kuonyesha ishara kwa matendo au kwa kauli juu ya uwapo wa nia hii. Uchunguzi umebaini kuwa kuliwapo viashiria vingi, isipokuwa Kibanda au watu wake wa karibu hawakupata kufikiri kuwa huenda vingeweza kuleta madhara makubwa kiasi hiki kama ifuatayo:-

1.1. Wiki tatu kabla ya Kibanda kuvamiwa, kutekwa na kuumizwa, gari la polisi aina ya gofu Na PT 180 liliwafuatilia kwa muda mrefu Absalom Kibanda na Ofisa Mtendaji Mkuu wa New Habari (2006) Ltd, Hussein Bashe likiwa limeegeshwa nje ya ofisi zao Sinza Kijiweni na baadaye likawafuatilia hadi Sinza Makaburini, ambapo walisimamisha magari yao na kuzungumza na polisi hao waliosema walikuwa wanatilia shaka magari yao. Baada ya kuzungumza kwa muda polisi waliondoka.

1.2. Usiku wa Februari 25, mwaka huu majira ya saa 09:00 usiku, Kibanda walivamiwa na watu walioingia kwenye uzio wa nyumba yao wakavunja kioo cha gari analotumia, lakini kioo kilipovunjwa ‘alarm’ ilipiga kelele, Kibanda akatoka nje na watu hao wakakimbia.

1.3. Kutokana na uvamizi huo, Kibanda na wapangaji wengine katika nyumba zilizopo kwenye uzio mmoja, waliona hatari ya kuvamiwa hivyo wakaanza mazungumzo na kampuni ya Ulinzi ya Kiwango, iliyowataka kufunga kamera za usalama na kuweka walinzi watano. Hadi Kibanda anatekwa, walikuwa hawajahitimisha mazungumzo na kampuni hii ya Kiwango.

1.4. Kuna askari anayefanya kazi Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) miezi minane kabla alipata kumpa Kibanda taarifa za kinteligensia, kuwa kulikuwapo mpango wa kumteka na kumuumiza. Taarifa kama hizo pia alipewa na wasamaria wanaofanya kazi katika Jeshi la Polisi. Kwa maneno yake Kibanda alisema:“Kuna rafiki yangu askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), kama miezi minane au tisa hivi aliwahi kuniambia ‘unaandika sana usidhani kama watu wanakupenda. Chukua tahadhari hasa unapofika getini nyumbani kwako’. Tangu wakati huo nimekuwa nikichukua tahadhari sana.“Wiki mbili kabla ya tukio, niliwahi kuhisi kitu kama hicho [cha kuvamiwa] nikiwa getini. Nilipiga honi wakachelewa kuja kunifungulia, niliogopa sana. Hata nilipoingia ndani nilikuwa nimekosa raha kabisa.“Pia kuna rafiki zangu polisi waliwahi kuniambia kwamba ninatafutwa na kwamba watu wananifuatilia na ikibidi wanitengenezee ajali au kunifanyia kama Ulimboka au Kubenea.”

1.5. Ndani ya miezi mitatu mbele ya mlango wa ofisi yake Kibanda (Free Media Limited) ilikuwa mara kwa mara muda wa asubuhi anapofika ofisini anakuta damu. Haikufahamika kama damu hiyo ilikuwa ni ya binadamu, kuku, ng’ombe, kunguru au mbuzi, bali waliipuuza wakidhani ni masuala ya ushirikina. Mhariri Mtendaji wa sasa, Ansbert Ngurumo, amethibitisha kuwapo kwa tukio hilo.1.6. Mfanyakazi mwandamizi wa Kampuni ya New Habari anakofanya kazi sasa Kibanda ndani ya wiki mbili kabla ya kutekwa na kuumizwa kwake alipata kumwabia Kibanda maneno mazito mara tatu, na hapa tunamnukuhu Kibanda:“Aliniambia Danny Mwakiteleko [aliyekuwa Naibu Mhariri Mtendaji wa New Habari] hakufa kwa ajali, bali alikufa kutokana na blood clotting (kuganda kwa damu). Hivyo ikitokea mtu ukapata ajali au ukapigwa na kuumizwa sana sehemu za kichwa hivi au tumbo, ni lazima madaktari wadhibiti sana blood clotting.“Na kweli, nilivyoletwa hapa Milpark hospitalini, madaktari walikuwa wananidunga sindano sita kila siku kwenye kitovu kuzuia blood clotting. .... (jina linahifadhiwa) aliniambia maneno haya mara tatu, katika mazingira yasiliyotarajiwa na kwa msisitizo ambao sikujua maana yake. Nasema .... (jina linahifadhiwa) naye achunguzwe kwa kina. Inawezekana kuna jambo analijua.”Ofisa huyu, alipishana dakika chache na Kibanda muda wa kutoka ofisini baada ya kipindi cha kwanza cha mechi kati ya Real Madrid na Manchester united kumaliza nusu ya kwanza (half time). Dakika ishirini baadaye Kibanda alishambuliwa.

2.0. Kuchunguza mazingira ya tukio lenyewe kwa kujikitika katika mwenendo wake hasa siku nzima ya Jumanne Machi 5, 2013.2.1. Familia ya Kibanda na Kibanda Mwenyewe hawakuwa na wasiwasi wowote siku hiyo kwani hawakuwa na hisia wala wazo kuwa ungetokea uvamizi huo.

2.2. Kibanda alipopiga honi, mlinzi alisogea langoni kumfungulia. Ghafla akasikia kishindo kikubwa. Akasikia kelele za Kibanda akiomba msaada. Kijana huyu Baraka Ibrahim mwenye umri wa miaka 27, aliogopa. Aliogopa kwa mana hakuwa na silaha yoyote mkononi. Hakuwa na panga, kisu, rungu, wala filimbi. Kwa maneno yake anasema:“Nilivyoona ningefungua geti hata mimi ningekufa, nilikimbia kuwaamsha majirani. Sikuwa hata na namba ya simu ya mtu yeyote kati ya mabosi wangu ninaowalinda. Nilikuwa mimi tu, imani yangu na Mungu wangu.... kutokana na maisha naifanya hivyo hivyo tu. Vinginevyo milele nisingefanya kazi hii ya ulinzi.”Mlinzi huyo alikimbilia kwa majirani katika nyumba aliyoamini yumo mwanaume, lakini akaanza kumwamsha House Girl, ili house girl amwamshe baba mwenyenyumba. Kitendo cha kuamshana na kuwapa taarifa kilichukua dakika tano hadi saba, na ndani ya muda huo, Mlinzi anasema watekaji wa Kibanda walifanyafanya unyama na uasi huo na kuondoka ndani ya muda mfupi kiasi hicho. “Watu hawa wana mafunzo maalumu,” anahitimisha.

2.3. Mke wake alikwenda kazini asubuhi na kurejea nyumbani jioni, lakini tofauti na utaratibu wake wa kawaida ambapo huwa anaangalia televisheni sebuleni hadi Kibanda anaporejea nyumbani, siku hiyo alikwenda kuangalia televisheni akiwa chumbani na usingizi ukampitia. Anasema hakusikia honi wala tukio la Kibanda kutekwa. “Hii inanitesa sana moyoni. Najiuliza kwa nini siku hiyo tu sikukaa sebuleni? Kwa nini siku hiyo tu nimelala mapema kabla Baba Joshua hajarudi (machozi yanamlengalenga). Najiuliza sipati jibu.”2.4. Mmoja kati ya wasaidizi wawili wa nyumbani kwa Kibanda, alisikia kelele za Kibanda akiomba msaada. Alimwamsha mwenzake na kumwambia. “Nasikia Baba Joshua anapiga kelele kama amevamiwa hivi.” Mwenzake alimwambia “Unaota maana kuna kelele za mpira.” Siku hiyo kulikuwa na mechi kati ya Real Madrid na Manchester United.Ni kweli zilikuwapo pia kelele za wanaoshangilia mpira siku hiyo, hivyo Kibanda alipoomba msaada, hata waliosikia walidhani watu wanashangilia mpira. Binti aliwaamsha Angela na mwenzake, wakaenda sebuleni, wakakaa na kuchungulia dirishani, wakaona mwanga wa gari getini, lakini baada ya kutosikia kelele yoyote wakarejea kulala wakidhani siye. Lakini binti mmoja alibaki sebuleni. Baada ya muda jirani mmoja akampigia simu Angela kumweleza kuwa mumewe ameshambuliwa.2.5. Kibanda kwa upande wake, anasema alipofika getini, alipiga honi, ghafla akaona watu wawili wamesimama pembeni mwa gari lake na mtu wa tatu akiwa kwa mbali. Kisha akasikia kishindo kikubwa, akidhani wanataka kuiba gari, aliatokea mlango wa abiria na kuanza kukimbia huku akiita. “Mama Joshua nisaidieeeeee.”Katika kukimbia, aliteleza akaanguka. Huku watesaji wake wakisema mara tatu “Afande piga risasi.” Kibanda alijaribu kupambana, akashika rungu, akawahoji amewakosea nini hadi wampige kiasi hicho, lakini hawakumjibu lolote. Waliendelea kumpiga, hadi akapoteza fahamu. Hakujua jicho limetobolewa saa ngapi, meno yameng’olewaje na wala pingiri ya kidole chake imekatawaje. Ifuatayo ni sauti ya Kibanda mwenyewe. Inasikitisha ila tuwe wavumilivu na tuisikilize.

3.0. Kuangalia mazingira ya kazi ndani ya Kampuni ya New Habari (2006) Ltd na nje ya kampuni hiyo kwa kumulika sababu za kuhama kwake kutoka Free Media mwishoni mwa mwaka jana na kuhamia New Habari.

3.1. Mazingira ya kazi ndani ya New Habari (2006) Limited na Freemedia Limited, yanaacha maswali kadhaa yenye kustahili majibu. Kama ilivyoelezwa kwenye Hadidu Rejea Na: 1, ndani ya kampuni ya New Habari imekuwapo misuguano isiyo na afya kwa kazi ya Kibanda kama mwandishi na tasnia ya habari kwa ujumla.

3.2.Mazingira ya kazi ndani ya Kampuni ya New Habari (2006) Ltd ni utata. Uhusiano katika chumba cha habari si mzuri. Ndani ya kampuni hawaaminiani na imefikia hatua wanatuhumiana kuwa huenda baadhi ya viongozi ndani ya New Habari wamehusika kumteka na kumuumiza Kibanda. Haya yameandikwa ndani ya mitandao ya kijamii, ikidai kwamba kiongozi mmoja ndani ya kampuni hiyo alihusika na utekaji wa Kibanda. Mkurugenzi wa Uhariri, Prince Bagenda anasema waliohusika kusambaza taarifa chafu dhidi ya kiongozi huyo wa New Habari wanatoka ndani ya kampuni hiyo.

3.3. Timu ya uchunguzi ilibaini kuwapo mgawanyiko mkubwa ndani ya New Habari (2006) Ltd kwa kuwapo kundi la ‘Habari Wazawa’ na ‘Habari wa Kuja’. Malalamiko mengi yanajikita katika msingi kuwa ajira hazitangazwi na watu wanaajiriwa bila kuzingatia sifa za kitaaluma.

3.4. Kibanda hakuhama Free Media kwa amani. Uchunguzi unaonyesha kuwa miezi kadhaa kabla ya kuondoka kwake alianza kupoteza mamlaka. Mwenyekiti wa Kampuni ya Free Media Ltd, Freeman Mbowe alianza kumsikiliza zaidi msaidizi wake ambaye alikuwa Naibu Mhariri Mtendaji, Ansbert Ngurumo kuliko yeye Kibanda. Kwa maneno yake, anasema:“Nilihofu kuwa Mbowe anaweza kutugombanisha. Nikaona ni bora niondoke nisije nikagombana na Mbowe au Ngurumo.”Anasema alianza kupoteza mamlaka yake na kutoaminika kwa mwajiri wake baada ya kuandika makala kuhusu Abdulrahman Kinana ambayo kabla ya kuiandika hakuwa na wazo la kuondoka. Yaliyofuata baada ya makala hiyo, yalimshukuma aondoke.

4.0. Kuchunguza jambo jingine lolote linaloweza kutoa mwanga wa sababu za kuvamiwa na kupigwa kwa Kibanda.

4.1. Uchunguzi ulifuatilia masuala mbalimbali ikiwamo miendendo ya watu waliotajwa kwa njia moja au nyingine kuhusinaa na tukio hili. Hata hivyo, karibu watu wote waliohojiwa, akiwamo Kibanda mwenyewe aliyeumizwa walimtaja kwa kutilia shaka mwenendo wa kijana Joseph Ludovick. Hofu yao, iliongezwa nguvu na maandishi aliyoyachapisha Ludovick kwenye mitandano ya kijamii siku ya Machi 6, 2013.

4.2. Usiku aliotekwa na kuumizwa Kibanda, Ludovick katika naye alidai kuwa ametekwa katika eneo la Shekilango na kupelekwa hadi Kigogo. Baada ya kutekwa aliibiwa kila kitu, ikiwamo begi, laptop, simu mbili, fedha taslimu Sh 35,000, akavuliwa nguo na kubaki na chupi tu. Pia alieleza kuwa alitoa taarifa hizo kituo cha polisi Mabibo.

4.3. Maelezo ya Ludovick yalitiliwa shaka na watu wengi hasa baada ya kuleeza kuwa watekaji walitumia muda wa saa mbili kumtoa Shekilango hadi Mabibo, umbali ambao kwa kiwaida mwendo wake hauwezi kuzidi dakika 10. 4.4. Daniel Chongolo aliiambia timu kuwa alfajiri ya Machi 6, siku anayodai kutekwa Ludovick yeye alimuona eneo la Mabibo wakati anatoka Muhimbili. Chongolo alikwenda kituo cha polisi Mabibo na kupewa taarifa kuwa Ludovick alitoa taarifa polisi kuwa alikuwa ametekwa ila akarudishiwa mali zake zote. “Alipouliza amefuata nini polisi, akawambia kama raia mwema amefika kuandikisha kumbukumbu kwa nia ya kuonyesha kiwango cha uhalifu kinavyoongezeka nchini,” anasema Chongolo. Timu ya uchunguzi ilikataliwa kupitia leja ya polisi kama itakavyoelezwa hapa chini.

4.5. Pia taarifa za uchunguzi wa timu hii zinathibitisha kuwapo kwa utata juu ya madai ya kuibwa kwa simu za Joseph Ludovick, kwani simu yake ya tigo (inayodaiwa kuibwa) ilitumika saa 01:21 asubuhi siku ya Machi 6, 2013. Muda huu ofisi za Serikali na Kampuni ya Tigo zilikuwa hazijafunguliwa

5.0. Kuchunguza mazingira ya sasa ya kazi kwa wanahabari na kupendekeza hatua za kuchukua kutokana na kile kitakachobainika.

5.1. Uchunguzi umebaini kuwa maisha ya wanahabari yapo hatarini. Hatari hii inatokana na makundi mengi yenye masilahi kuwaona wanahabari wanaosimamia ukweli kuwa maadui wa masilahi yao haramu. Kuna hatari kubwa inayowakabili waandishi wakati nchi inapoelekea kwenye uchaguzi wa mwaka 2015.

5.2. Uchunguzi umebaini kuwa usiri umepungua katika vyombo vya habari. Tofauti na zamani ambapo habari nyeti ziliandikwa kwa kuhifadhi majina ya waandishi wakitumia jina la MWANDISHI WETU. Simu hizi hata habari za kutisha waandishi wanaweka majina yao na hata wasipoweka, ndani ya vyumba vya habari vingi waandishi wapo tayari kutaja nani ameandika habari fulani.

5.3. Usaliti miongoni mwa waandishi wenyewe ndani ya vyumba vya habari unazidi kuongezeka na usipodhibitiwa hali itazidi kuwa mbaya zaidi. Mwenyekiti wa MOAT, Dk. Reginald Mengi anasema: “Hili ni jambo muhimu sana. Tuache usaliti vinginevyo wengi wataumia.”

5.4. Pia alishauri waandishi wa habari kurejea katika msingi wa taaluma, ambayo inawataka wao kuwa ndio wenye kuendesha vyombo vya habari badala ya kutegemea matakwa ya wamiliki au makundi yenye masilahi binafsi.

6.0. KILICHOBAINIKA:
6.1. Uchambuzi uliofanywa ni timu hii umebaini kuwa hoja nne zinazungumzwa kuhusiana na kutekwa na kuumizwa kwa Kibanda. Hoja hizi ni:-(i) Kazi yake ya uandishi wa habari(ii) Uhusiano wa kisiasa na vyama au wanasiasa mbalimbali(iii)Uhusiano wa kijamii ikiwamo mapenzi(iv) Vitendo vya rushwa.

6.2. Timu imejiridhisha kutokana na majibu ya wengi kuwa dhana ya mapenzi na rushwa, havina nafasi yoyote katika tukio hili. Wote waliohojiwa walieleza pasi na shaka kwamba suala hili la kushambuliwa na kuumizwa kwa kiwango kikubwa kwa Kibanda, halina uhusiano wowote na rushwa au mapenzi.

6.3. Kutokana na yaliyotajwa hapo juu kazi yake na siasa vikiunganishwa vimechangia kwa kiasi kikubwa kuvamiwa kwa Kibanda. Timu imebaini kuwa kuna kutupiana mpira kati ya vyombo vya dola na vyama vya siasa. Mchezo huu mchafu unaweza ukawa mwanzo wa kuumizwa kwa Kibanda na waandishin wengine.

6.4. Baadhi ya waliohojiwa walidai kuwa utekaji huu umefanywa na vyombo vya dola ukiwa sehemu ya mpango mkakati wa vyombo hivi kukihusisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na vitendo vya ugaidi.6.5. Wanayataja matukio ya Uchaguzi Mdogo wa Igunga, maandamano ya Morogoro na Mkanda anaodaiwa kurekodiwa Mkurugenzi wa Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare kuwa vililenga kukifanya CHADEMA kichukiwe na Watanzania kwa kukitaja kama chama cha kigaidi ambacho kinateka watu na kinawaumiza.

6.6. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe anadai kwamba mpango kama huo vyombo vya dola viliutumia kwa NCCR Mageuzi vikakisambaratisha, Chama cha Wananchi (CUF) kilisingiziwa udini kikapoteza mwelekeo na sasa vyombo hivyo vililenga kukifanya CHADEMA kionekane cha kigaidi mbele ya macho ya jamii ndiyo maana imerekodiwa mikanda kwa nia ya kuitumia kujenga hoja hiyo.

6.7. Wakati Mbowe akisema hayo, baadhi ya watu waliohojiwa wanadai kuwa CHADEMA kimepewa mafunzo na ushauri kutoka nje ya nchi kuwa kikitumia baadhi ya watumishi wa vyombo vya dola wasiokuwa waaminifu kuteka, kuumiza na hata kuua baadhi ya watu maarufu nchini wakiwamo waandishi na wanasiasa, basi wananchi wataamini kuwa Chama Cha Mapinduzi na Serikali yake kimeshindwa uongozi na sasa kimeanza kazi ya kuua wanaowapinga.

6.8. Kwa njia hiyo, inaelezwa kuwa hesabu za Chadema ni kuwa wananchi wataichukia CCM na Serikali yake na kukipa nafasi ya kuingia madarakani. Hapa kauli ya Chadema kuwa NCHI HAITATAWALIKA itakuwa imetimia.

6.9. Dhana nyingine iliyojitokeza ni kuwa wapo wafanyabiashara ambao wana vita binafsi, hivyo wanaamua kuumiza watu wasiowaunga mkono katika mipango yao na hilo ndilo limemkumba Kibanda, baada ya kuwa ameepusha mauaji ya mwandishi mmoja na aliyekuwa ameandaa mpango wa kuua mwandishi huyo hakuridhika hivyo akaamua amshughulikie Kibanda.

7.0. MAPENDEKEZO:Baada ya Timu kupata taarifa hizi na nyingine nyingi, inapendekeza yafuatayo:-

7.1. Taarifa hii ichukuliwe kama chanzo cha uchunguzi zaidi wa vyombo husika.7.2.

Yanahitajika marekebisho makubwa na ya haraka katika mifumo ya uendeshaji wa vyumba vya habari kwa nia ya kurejesha misingi ya uandishi wa habari inayokubalika.

7.3. Usalama wa wanahabari unapaswa kupewa kipaumbele na wamiliki, wanahabari wenyewe na jamii kwa ujumla. Hapa Timu inapendekeza yawepo mafunzo ya kuwawezesha wanahabari kutambua viashiria vya hatari na kuchukua hatua mara moja.

7.4. Kwa kiwango alichoumizwa Kibanda iwapo mwajiri wake asingejitolea kugharamia matibabu, hatujui hatima yake ingekuwaje leo hii. Tunapendekeza taasisi na mifuko mbalimbali inayojihusisha na masuala ya wanahabari kama Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) , Baraza la Habari Tanzania (MCT), Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF) na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) kuanzisha mfuko wa pamoja utakaotumika kugharamia matibabu ya waandishi watakaoumia wakiwa kazini.

7.5. Tukio la kutekwa kwa Kibanda limeonyesha mwanga kuwa wahariri tumegawanyika mno. Habari zilizochapishwa katika magazeti mbalimbali na mitandao ya kijamii zimeonyesha haja ya kuwafanya wahariri kuwa kitu kimoja kwa kuondoa tofauti zao zisizo na masilahi kwa tasnia ya habari.

7.6. Kuna viashiria vingi kuwa kuelekea mwaka 2015 matukio ya waandishi kuumizwa au kutekwa yanaweza kuongezeka kutokana na wanasiasa na vyama kuwania madaraka huku wakitumia baadhi ya watumishi katika vyombo vya dola. Kwa mantiki hiyo, vyombo vya habari na waandishi wa habari wachukue tahadhari kuanzia sasa.

7.7. Taasisi za habari zifanye juhudi za makusudi kukutana na vyama viwili vya siasa vya CCM na CHADEMA haraka iwezekanavyo, kuzungumzia viashiria hivi vya hatari vinavyoelekea kuvuruga amani ya Tanzania.

8.0. HITIMISHO:Ni dhahiri kuwa kupigwa na kuteswa kwa Kibanda kumejiegemeza katika siasa na kazi yake, hali inayofanya makundi muhimu kuchukua wajibu wa msingi. Kwa upande wa Serikali ni muhimu kufuatilia viashiria katika taarifa hii kwa nia ya kupata ukweli zaidi na kuchukua hatua stahiki za kisheria dhidi ya wahusika.Na kwa upande wa vyombo vya habari na taasisi za kihabari zinapaswa kutambua viashiria vinavyohatarisha usalama wa waandishi wa habari na wahariri na kutengeneza mazingira yatayokuwa salama zaidi kwa waandishi kufanya kazi zao.

9.0. SHUKRANI:

9.1. Tunapenda kulishukuru Jukwaa la Wahariri Tanzania, kwa kufanya uamuzi sahihi wa kuwezesha kufanyika kwa uchunguzi huu ulioanza kuonyesha mwanga wa nini kilitokea.

9.2. Tunapenda kulishukuru Baraza la Habari Tanzania (MCT) kwa kushiriki kikamilifu na kuiwezesha timu hii kwa Rasilimali Watu na Mali kufanikisha kazi hii.

9.3. Tunapenda kuwashukuru Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF) kwa uwezeshaji wa ruzuku, uliofanikisha kufanya uchunguzi wa kihabari uliohusisha kwenda nchini Afrika Kusini kufanya mahojiano na Kibanda. Uwezeshaji huo pia unahusisha kutengeneza mwongozo kwa waandishi wenye lengo la kuwaepusha na hatari za kiusalama.

9.4. Tunawashukuru Kibanda, mkewe Angela, wanafamilia, ndugu na jamaa wa Kibanda na wanahabari wote waliohojiwa kwa ushirikiano mkubwa walioutoa kwa Timu hii.

9.5. Tunawashukuru wahariri wote kila mtu kwa nafasi yake, kutokana na ushauri wa mara kwa mara mliotupatia katika kufanikisha uchunguzi huu.

10.0. WAJUMBE WA TIMU:Timu hii iliundwa na wajumbe watano ambalo ni:1. Deodatus Balile – Mwenyekiti2. Pili Mtambalike – Mjumbe3. Jane Mihanji – Mjumbe4. Tumaini Mwailenge – Mjumbe5. Rashid Kejo – Katibu

Mwisho.

Rais Kikwete awasili Japan, kukutana na Waziri Mkuu

Rais Jakaya Kikwete
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amewasili nchini Japan jioni ya leo, Jumatano, Mei 29, 2013, kuhudhuria Mkutano wa Tano wa Kuzungumzia Maendeleo ya Afrika
ujulikanao kama Tokyo International Conference on African Development (TICAD - V) unaoanza Yokohama, mji mkubwa wa pili katika Japan, Jumamosi,  Juni  Mosi hadi 3, mwaka huu, 2013.

Kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Narita mjini  Tokyo, Rais Kikwete ambaye anafuatana na Mama Salma Kikwete amepokewa na Balozi wa Tanzania katika Japan Mheshimiwa Mama Salome Sijaona na maofisa wengine wa Ubalozi wa Tanzania katika Japan.

Rais Kikwete amewahi kuwasili nchini  Japan kabla ya Mkutano wa TICAD V kwa vile ni mmoja wa viongozi wawili wa Afrika waliopangwa kuonana na Waziri Mkuu wa Japan Mheshimiwa Shinzo Abe kabla ya kuanza kwa Mkutano wenyewe wa TICAD V.

Mheshimiwa Abe ambaye ndiye amemwalika Rais Kikwete kufanya ziara ya kikazi ya wiki moja katika Japan wakati huu anakutana na Rais Kikwete mapema ili kuweza kupata maoni, msimamo na matarajio ya Afrika kabla ya kuanza kwa Mkutano wa TICAD V.

Mkutano wa mwaka huu utakwenda sambamba na sherehe za kumbukumbu ya miaka 20 ya Mkutano wa TICAD ambao ulifanyika kwa mara ya kwanza mjini Tokyo mwaka 1993.

Mkutano huo – TICAD V utawashirikisha viongozi wa Afrika, viongozi wa Japan na washirika wa maendeleo ya Afrika ikiwamo Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU) na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) na utafunguliwa na Waziri Mkuu wa Japan mwenyewe, Mheshimiwa Abe.

Wengine waliopangwa kuzungumza kwenye sherehe hiyo ya ufunguzi wa Mkutano huo mkubwa ni Waziri Mkuu wa Ethiopia Mheshimiwa Hailemariam Desalegn ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika (AU), Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mheshimiwa Ban Ki Moon na Mwenyekiti wa Kamisheni ya Afrika Mheshimiwa Dkt. Nkosazana Dlamini Zuma.

Mbali na kukutana kwa mazungumzo na Waziri Mkuu Abe, Rais Kikwete pia atakuwa miongoni mwa kundi la viongozi wa Afrika watakaokutana na Mfalme wa Japan, H.M. Akihito.

Katika mkutano kati ya viongozi hao wawili, Waziri Mkuu wa Japan anatarajiwa kuwa atatangaza kuwa Japan inaifutia Tanzania deni la dola za Marekani milioni 220 likiwa ni deni la mchele ambao Tanzania
iliupata kutoka Japan chini ya mikataba iliyotiwa saini kati ya mwaka 1980 na 1983 kati ya Mamlaka ya Chakula ya Japan na Serikali ya Tanzania.

Aidha, inatarajiwa kuwa Mheshimiwa Abe atatangaza rasmi kuwa Japan itagharimia ujenzi wa barabara ya juu kwa juu (fly-over) katika eneo la Ubungo, Dar es Salaam, kama moja ya hatua za kupunguza msongamano wa magari katika jiji hilo.

Kabla ya kuanza TICAD V, Rais Kikwete pia atakutana na kuzungumza na wakuu wa mashirika makubwa na kimataifa ya kibiashara na uchumi ya Japan ambayo yanaendesha shughuli zake katika Afrika ama yanapenda kuanzisha shughuli katika Tanzania.

Kesho, Alhamisi, baada ya kuwa amekutana na Mheshimiwa Abe, Rais Kikwete atakwenda Kawasaki ambako atakutana na viongozi wa Kampuni ya Natori Holding Management ambayo imeamua kuwekeza katika sekta ya nguo na kilimo cha pamba katika Tanzania.

Baadaye kesho, Mheshimiwa Rais atatembea Jumba la Makumbusho la Sayansi la Kampuni ya Toshiba, maarufu duniani kwa utengenezaji wa kompyuta za aina ya Toshiba na vifaa vingine vya elektroniki. Baadaye,
Rais atatembelea na kuzungumza na wanafunzi wa Shule ya WASEDA kuhusu nafasi na mchango wa Tanzania katika uhusiano wake na Japan.

Keshokutwa, Ijumaa, Rais Kikwete atatembelea Shirika la Sumitomo ambalo limewekeza katika ujenzi wa kituo cha umeme cha Kinyerezi cha Dar Es Salaam ambacho kitatoa megawati  220 na linataka kuwekeza
katika miradi ya miundombinu kwa kushirikiana na sekta binafsi katika Tanzania.

Akiwa Sumitomo, Rais Kikwete atashuhudia utiaji saini wa ujenzi wa mradi wa umeme wa Kinyerezi baina ya Sumitomo Corporation yenyewe, Benki ya Maendeleo ya Japan – JBIC na Wizara ya Fedha ya Tanzania. Mchana wa keshokutwa, Rais Kikwete atakuwa miongoni mwa viongozi wachache wa Afrika walioalikwa na Waziri Mkuu Mheshimiwa Abe kuzungumzia hali ya Somalia.

Katika mkutano huo, Mheshimiwa Abe anataka kupata mawazo ya viongozi hao wachache wa Afrika ambayo yatawasilishwa kwenye Mkutano wa 39 wa wakuu wa  Nchi Tajiri na Zenye Viwanda Vingi Duniani – G-8 uliopangwa kufanyika Lough Erne, Uingereza mwezi ujao, Juni 17-18, 2013.

Aidha, Rais Kikwete siku hiyo hiyo, atakutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Kampuni ya Marubeni, moja ya makampuni makubwa zaidi ya biashara katika Japan ambayo imeonyesha nia ya kujenga Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia na Kuzalisha Umeme katika Tanzania.

Jioni ya siku hiyo, Rais Kikwete atahudhuria hafla maalum ya kitaifa inayoandaliwa na Mheshimiwa Abe kwa ajili ya viongozi wote watakaohudhuria Mkutano wa TICAD V.

Mkutano wa TICAD V miongoni mwa mambo mengine utajadili mchango wa sekta binafsi, biashara na uwekezaji kama injini za maendeleo, jinsi gani Afrika inavyoweza kuimarisha sekta ambazo zimejithibitisha kuwa misingi ya kukua kwa uchumi wa Bara la Afrika, Ajenda ya Maendeleo baada ya mwaka 2015 ambao ni mwisho wa utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDG’s). Hatimaye, mkutano huo utatoa Azimio ya Yokohama 2013 na Mpango wa Utekelezaji wa Yokohama kwa miaka 2013 hadi
2017.

Mikutano ya TICAD (TICAD Policy Forum and Conference) ilianzishwa mwaka 1993 na Japan kwa kushirikiana na UN, UNDP na Benki ya Dunia kwa njia ya kujadili na kuendeleza ajenda ya maendeleo ya Bara la Afrika.

Chini ya mchakato huo wa TICAD, Japan hujenga mazingira ya  kuunga mkono ajenda ya maendeleo ya Bara la Afrika ambalo nalo ndilo linamiliki na kuongoza jukumu la kimsingi la kujiendeleza kwa kushirikiana na Bara la Asia na Jumuia ya Kimataifa.

Tokea ulipofanyika mkutano wa kwanza – TICAD 1 mjini Tokyo Oktoba 5-6, mwaka 1993, imefanyika mikutano mingine mitatu na kujenga mazingira mazuri zaidi ya jinsi Japan na Jumuia ya Kimataifa inavyoweza
kuchangia maendeleo ya Afrika.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu. Dar es Salaam.
29 Mei, 2013

Ethiopia kujenga bwawa kwenye Blue Nile

Ethiopia imeanza kuelekeza kwingine mkondo wa maji ya mto Blue Nile ili kujenga bwawa kubwa, hatua ambayo imezua mzozo mkubwa na nchi zinazotegemea maji ya mto huo.

Bwawa hilo litakalogharimu Ethiopia dola bilioni 4.7 ni sehemu ya mradi unaolenga kuigeuza Ethiopia kuwa muuzaji mkuu wa nishati ya umeme inayotengenezwa kutokana na maji. Misri na Sudan zinasema mradi huo unakiuka makubaliano ya miongo kadhaa kuhusu matumizi ya pamoja ya maji ya mto Nile.

Mradi huo umesababisha mgogoro kati ya Ethiopia na nchi zinazotumia maji ya mto Nile. Bwana hilo lijulikanalo kama Great Ethiopian Renaissance, ambalo tayari limeanza kujengwa ni sehemu ya mradi wa uekezaji wa dola bilioni 12 ili kuimarisha ununuzi wa kawi ya nchi hiyo.

Mto wa Blue Nile ni moja ya vyanzo vya maji ya mto Nile, moja ya mito mirefu zaidi duniani. Misri na Sudan zinapinga ujenzi wa bwawa hilo. Wanasema Bwawa hilo linakiuka mkataba wa enzi za kikoloni ambao unawapa 90% umiliki wa maji ya mto huo.

Bwawa la The Grand Renaissance , ambalo linajengwa katika eneo la Benishangul-Gumuz linalopakana na Sudan, hatimaye litaweza kuzalisha megawati 6,000 za umeme kulingana na serikali ya Ethiopia.Kiwango hiki ni karibu mara ya sita ya umeme unaozalishwa na mitambo sita ya nuklia.
Source:  http://www.bbc.co.uk/swahili/habari/2013/05/130529_blue_nile.shtml

Thursday, May 23, 2013

Marehemu Chinua Achebe kuzikwa leo Nigeria


Mwili wa mwandishi mashuhuri wa vitabu barani Afrika Chinua Achebe umewasili nyumbani kwake katika jimbo la Anambra nchini Nigeria. Mwandishi huyo mashuhuri alifariki mjini Boston,Marekani, akiwa na umri wa miaka 82 baada ya kuugua kwa muda mfupi.
 
Jamaa na maafisa wa serikali walikuwa katika uwanja wa ndege Kusini mwa Nigeria kumpokea marehemu. Hayati Achebe, anasifika sana kwa kuwa mwanzilishi wa fasihi ya kiafrika kwa kiingereza.

Kitabu chake alichokianda cha kwanza, mwaka 1958, Things Fall Apart, ambacho kilizungumzia sana athari za ukoloni barani Afrika, aliweza kuuza zaidi ya vitabu milioni kumi.

Mwandishi huyo na msomi, aliendelea na uandishi wake na kuandika vitabu vingine 20 baadhi vikikosoa sana wanasiasa na kile alichokitaja kama ukosefu wa uongozi nchini Nigeria. Alikuwa anaishi nchini Marekani tangu mwaka 1990 baada ya ajali ya barabarani kumjeruhi kiasi cha kumlemaza.

Makundi ya kitamaduni yalifanya tamasha mbali mbali nje ya uwanja wa ndege wa Enugu, huku ndege iliyokuwa inambeba marehemu Achebe ilipotua. Inaarifiwa kuwa licha ya kuwa watu wana majonzi tele, lakini pia wanasherehekea maisha ya mwandishi huyo. 
Achebe atazikwa karibu na nyumbani kwa familia yake mjini Ogidi, mji mdogo kwenye vilima vya jimbo la Anambra. Achebe aliandika sana vitabu vya kukosoa serikali ya Nigeria kwa uongozi duni

Tuesday, May 21, 2013

Polisi wavamia gazeti Daily Monitor kwa "kumfichua" ya Museveni

Polisi nchini Ugandan wamevamia ofisi za magazeti kufuatia taarifa kwamba Rais Yeweri Museveni anamuandaa mwanawe wa kiume kumrithi urais.
Vituo viwili vya Redio pia vamiwa na kuzimwa , hii ni kwa muujibu wa gazeti la serikali la New Vision. Wiki iliyopita magazeti ya Uganda yalidai kuwa kuna njama za kuwaua wale watakao pinga mpango wa Rais Museveni kumuandaa mwanawe kuchukua madaraka ya Uganda.
Magazeti hayo yalidai kuwa mipango hiyo ya mauaji yalitolewa na Mkuu fulani wa jeshi la Uganda. Rais Museveni, ambaye amekuwa madarakani tangu 1986, anatarajiwa kung'atuka uongozini mwaka 2016. Kwa muda mrefu kumekuwa na madai kwamba Museveni anamuandaa mwanawe Muhoozi Kainerugaba,ambaye ni brigadier jeshini kushikilia uongozi wa Uganda, lakini serikali ya Museveni imekanusha kwamba kuna mipango kama hiyo.
Mwanawe Museveni Brig. Kainerugaba.
Wiki iliyopita gazeti la, The Daily Monitor, na jingine la, Red Pepper, lilichapisha barua ya siri ikidai ilikuwa imeandikwa na Jeneral David Sejusa, ikitaka uchunguzi ufanywe kuthibitisha madai kwamba kuna mipango ya kuwauwa wote watakao piga mipango ya Rais Museveni kumpachika mwanawe uongozini. Uvamizi huo wa polisi umeidhinishwa na mahakama ya Uganda na ulikuwa unalengo la kutafuta barua hiyo inayodaiwa kuandikwa na mkuu huyo wa Jeshi akifichua njama za mauaji.
Vituo viwili vya Redio vinavyohusiana na Daily Monitor, Dembe FM na KFM, pia vilivamiwa na kuzimwa. Mkurugenzi Mkuu wa Daily Monitor Alex Assimwe aliambia BBC kwamba Chumba chao cha Habari kilivamiwa na polisi wapatao 50 waliojihami kwa silaha.
Lakini wachambuzi wa maswala ya kisiasa wanadai kuwa ikiwa barua ya Jenerali Sejusa ni ya kweli basi ni dalili kuwa kuna hali mvutano ndani ya jeshi huku ikidhaniwa kuwa wanajeshi wakongwe huenda wanapoteza uwezo kwa wanajeshi chipukizi wanaoongozwa na mwanawe Museveni Brigadia Kainerugaba.
Jenerali Sejusa ni mwanajeshi mkongwe aliyekuwa katika vita vya ukombozi uliyomuweka Rais Museveni madarakani mwaka1986.
Kwa muujibu wa taarifa za AP kamanda mmoja wa jeshi Jenerali Aronda Nyakairima amenukiliwa akisema kuwa Jenerali Sejusa kwa wakati huu anachunguzwa kutokana na barua anayodaiwa kuiandika.

Monday, May 20, 2013

SPIKA AZUIA HOTUBA YA MBILINYI WA KAMBI YA UPINZANI BUNGENI



HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MHESHIMIWA JOSEPH O. MBILINYI (MB) KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014
(Inatolewa chini ya Kanuni ya 99(9) ya kanuni za Bunge toleo la mwaka 2013)
1.   UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika,
Dira ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ni “kuwa na taifa lililohabarishwa vizuri, lina vijana wenye uwezo na malezi bora, linathamini utamaduni wake na linakuwa mahiri katika michezo ifikapo mwaka 2025.” Aidha, ‘dhamira’ ya wizara hii ni ‘kuendeleza utambulisho wa taifa kwa kuwezesha upatikanaji mzuri wa habari, kuwawezesha vijana kiuchumi na kukuza utamaduni na michezo kwa umma kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.’
Mheshimiwa Spika,
Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Serikali hii ya CCM imeshindwa kutekeleza dira na dhamira iliyotajwa katika maandiko ya kisera ya Wizara. Badala yake, chini ya usimamizi wa Wizara hii, Tanzania imegeuka kuwa taifa lisilotaka watu kuhabarishwa vizuri juu ya matendo ya watawala. Tanzania imegeuka kuwa taifa linalofungia magazeti yanayofichua ufisadi, uchafu na matumizi mabaya ya madaraka miongoni mwa viongozi, watendaji na watumishi wa Serikali hii ya CCM. Tanzania imegeuka, chini ya usimamizi wa Wizara na Serikali hii ya CCM, kuwa taifa linaloteka nyara wanahabari, kuwatesa kwa kuwang’oa kucha na meno, kuwatoboa macho, kuwamwagia tindikali na hata kuwaua. Tanzania sio nchi inayoandaa vijana wake tena. Haiwapi tena elimu bora wala kuwapatia maarifa, uwezo na malezi bora; ni nchi isiyowawezesha wala kuwathamini vijana wake; ni nchi inayoruhusu vijana wake kunyonywa na kutoendelezwa; na ni taifa ambalo limeachia utamaduni utambulisho wake kama taifa kupotea kabisa. Aidha, katika fani ya michezo ya aina zote, Tanzania imeporomoka kutoka taifa lililokuwa linaheshimika kimataifa katika miaka ya sabini na kuwa alichokiita rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi, ‘kichwa cha mwendawazimu’ ambacho kila kinyozi anajifunzia kunyolea!
2. UHURU WA UHARIRI NA USALAMA WA WANAHABARI
Mheshimiwa Spika,
Kwa masikitiko makubwa, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inalitaarifu Bunge lako tukufu kwamba sasa Tanzania imeingia rasmi katika orodha ya fedheha (The List of Shame) ya mataifa ambayo taaluma ya habari ni taaluma ya hatari kwa wale wote wanaoitumia kama sehemu ya wajibu wao kwa taifa na kama ajira yao. Kwa mujibu wa taarifa ya Kamati ya Kulinda Waandishi wa Habari Ulimwenguni (the Committee to Protect Journalists - CPJ) iliyotolewa mwaka huu 2013, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa CPJ mwaka 1992, Tanzania imeingizwa kwenye orodha ya nchi 20 ambazo ni hatari kwa waandishi wa habari kufanya kazi zao kutokana na hatari ya  kuuwawa kwa mwaka 2012 (20 Deadliest Countries in 2012). Kwa mujibu wa taarifa hiyo, ilishikilia nafasi ya 7 ulimwenguni kati ya nchi 20 zinazoongoza kwa kuhatarisha maisha ya waandishi wa habari.
Mheshimiwa Spika,
Kwa mujibu wa taarifa ya CPJ, tishio kubwa kwa waandishi wa habari duniani ni kuuwawa kwa kutekwa na kuteswa na/au kutishiwa maisha. Aidha, Serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama ni washiriki wakubwa wa mauaji ya waandishi wa habari. Kwa mujibu wa takwimu za CPJ, kati ya waandishi waliouwawa mwaka 2012, karibu ya 20% waliuwawa ama na maafisa wa serikali au na majeshi yake. Karibu idadi hiyo hiyo ya waandishi wa habari waliuawa kwa sababu ya kufuatilia taarifa za kiuchunguzi na za hatari. Taarifa hiyo inaonyesha kwamba hadi kufikia Aprili 2013, waandishi wa habari wapatao 30 tayari wamekwishauawa ulimwenguni wakati wakitimiza wajibu wao; wakati mwaka 2012 waandishi wa habari 103 waliuwawa ulimwenguni kote.
Mheshimiwa Spika,
Taarifa ya CPJ inaungwa mkono na ushahidi wa matukio mengi yanayodhihirisha kwamba maisha ya waandishi wa habari wa Tanzania yako hatarini kutokana na vitendo na vitisho kutoka kwa Serikali na watendaji wake ambao hawataki kusikia ukweli dhidi yao ukianikwa hadharani. Kudhihirisha kauli hii tunaomba kumnukuu mwanahabari mahiri na mmoja wa wahanga wa vita dhidi ya wanahabari na uhuru wa habari hapa nchini, Mzee Ndimara Tegambwage:
Mwaka 2006, waliojiita wananchi wakazi wa jiji la Mwanza, walikusanywa na wenye uwezo kufanya maandamano makubwa kwa walichoita ‘kupinga mwandishi Richard Mgamba kuandika uongo’ na kudai kwamba alikuwa Mkenya na ‘siyo raia wa Tanzania.’ Desemba 2009, mwandishi Frederick Katulanda wa Mwanza, alivamiwa nyumbani. Wavamizi walikuwa wakipaza sauti na kudai kuwa ana nyaraka za akaunti za benki za Halmashauri ya Jiji la Mwanza. Walikuwa na mapanga. Walikuwa wakichagizana kwa kusema, “Kata kichwa! Kata kichwa!” Waliondoka na mafaili. Walimwachia kilema mguuni na makovu mikononi.

“Mwezi Septemba, 2010 wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu, katika eneo la Nyambiti, Jimbo la Sumve wilayani Kwimba, mkoani Mwanza, mwandishi Frederick Katulanda alivamiwa na kupigwa na watu wapatao 15 waliojiita “Green Guard” – wa “chama cha kijani.” Katika “kumshughulikia,” Katulanda anasema, walikuwa wakionyesha kuwa na ujuzi mkubwa wa judo na karate huku wakidai kuwa anawaandika ‘vibaya’ Chama Cha Mapinduzi (CCM).

“Mwaka 2011 mwandishi Richard Massatu alikutwa amekufa katika eneo la Igoma, jijini Mwanza. Vyombo vya habari viliripoti kuwa macho yake yalikuwa yametobolewa na kuwekwa gundi aina ya super glue; mguu wa kushoto na mbavu vilikuwa vimevunjika. Vyombo vya habari viliripoti kuwa Massatu aliyekuwa mmiliki na mhariri mkuu wa gazeti la Kasi Mpya (sauti ya umma), alionekana mara ya mwisho usiku wa kifo chake akiwa na maofisa wa polisi na usalama katika baa iitwayo Cross Park katika eneo la Igoma.

“Tarehe 3 Januari, maiti ya mwandishi Issa Ngumba iliokotwa katika pori la mlima Kajuruheta, kijiji cha Mhange, wilayani Kakonko katika mkoa wa Kigoma.Ngumba alikuwa mwandishi wa habari wa Redio Kwizela. Tangu mwezi uliopita Machi, mwandishi wa habari Erick Kabendera anayeishi Dar es Salaam, anaishi kwa wasiwasi. Wazazi wake waishio Bukoba, wamehojiwa na ‘ofisa usalama’ kwa kile kilichoitwa ‘uhalali wa uraia wao.’

“Kuuwawa kwa aliyekuwa mwandishi wa habari wa Kituo cha Luninga cha ITV, John Lubungo ambaye alikuwa mfuatiliaji mahiri wa habari zinazohusu  wafanyabiashara au biashara haramu ya dawa za kulevya ambayo inadaiwa kufanywa na watu wakubwa nchini, wakiwemo vigogo serikalini. Kuna orodha ndefu ya waandishi wa habari waliotishwa na wanaoendelea kutishwa; waliopigwa na polisi na askari magereza (Ukonga, Dar es Salaama) kwa tuhuma mbalimbali; waliotishiwa maisha kwa simu na hata kwa kufuatiliwa na watu wasiowafahamu.”
Kwa sababu ya uadilifu na kutopenda kujikweza, Mzee Tegambwage hakutaja shambulio la tindikali na mapanga dhidi yake na mwandishi mwenzake Saed Kubenea wa gazeti la Mwanahalisi, ambalo baadae lilifungiwa na Serikali hii ya CCM.
Mheshimiwa Spika,
Katika Maoni yake wakati wa mjadala wa bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria ya tarehe 3 Mei mwaka huu, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilielezea kwa kirefu jinsi ambavyo Serikali hii ya CCM imekuwa tishio kwa maisha ya waandishi wa habari na kwa uhuru wa habari katika nchi yetu. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilirejeaRipoti ya Timu Maalum ya Uchunguzi Iliyoteuliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Kuchunguza Mazingira Yaliyopelekea Kuuawa kwa Mwandishi wa Habari Daudi Mwangosi Septemba 2, 2012 Katika Kijiji cha Nyololo, Wilaya ya Mufindi, Mkoani Iringa, iliyotolewa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), taasisi mbili huru zinazojihusisha na masuala ya habari Tanzania.
Kwa mujibu wa Ripoti ya MCT/TEF, matokeo ya uchunguzi wao “... yanadhihirisha bila wasi wasi kwamba polisi kwa makusudi waliwavurumisha waandishi waliotoka Iringa wakati wakikusanya habari za shughuli za CHADEMA katika kijiji cha Nyololo. Zaidi ya hapo, Daudi Mwangosi mwenyewe aliuawa akiwa mikononi mwa polisi huku wakisimamiwa moja kwa moja na Kamanda (wa Polisi wa Mkoa wa Iringa SACP Michael) Kamuhanda.” Ripoti hiyo inaelezea jinsi Marehemu Mwangosi alivyouawa: “Alipoangalia nyuma, Daudi Mwangosi aliona kikundi cha polisi wakimpiga mwandishi mkuu wa gazeti la Nipashe wa Iringa, Godfrey Mushi.... Wakati mwandishi Godfrey Mushi akiwa bado anapigwa na polisi, marehemu Mwangosi aliwakimbilia akiwaomba waache kumdhuru zaidi Mushi kwa kuwa alikuwa mwandishi tu. Polisi hawakumsikiliza. Badala yake wakamburuta mwandishi huyo ambaye tayari alikuwa amepoteza fahamu na kumweka kwenye gari lao na wakamgeukia Daudi Mwangosi mwenyewe, wakampiga kwa nguvu mpaka akapoteza fahamu.”
Hata amri ya Mkuu wa Kituo cha Polisi Mafinga Mwampamba kuwataka askari polisi waache kumpiga marehemu Mwangosi haikusikilizwa na askari hao. Ili kujiokoa, marehemu Mwangosi alimkumbatia OCS Mwampamba na “baadaye kumwangukia miguuni mwake kuepuka kipigo zaidi.” Kwa mujibu wa Ripoti ya MCT/TEF, “picha za mgando zinaonyesha polisi mmoja akipiga bomu la machozi tumboni mwa marehemu Mwangosi kwa karibu kabisa.” Bomu hilo liliusambaratisha mwili wa marehemu Mwangosi aliyekufa papo hapo. Kwa sababu marehemu Mwangosi alikuwa chini ya miguu ya OCS Mwampamba, “naye pia alijeruhiwa vibaya.”
Mheshimiwa Spika,
Sio MCT/TEF pekee zilizofanya uchunguzi wa mauaji ya Marehemu Mwangosi. Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora nayo ilitoa Taarifa ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ya Uchunguzi wa Tukio Lililopelekea Kifo cha Daudi Mwangosi Kilichotokea Septemba 2, 2012 Kijijini Nyololo, iliyobaini kwamba Marehemu Mwangosi “... alizingirwa na askari, aliteswa na hatimaye ... alipigwa bomu na kufa papo hapo.” Aidha, kwa mujibu wa Taarifa hiyo, “... Tume imejiridhisha kuwa tukio la lililopelekea kifo cha Daudi Mwangosi limegubikwa na uvunjwaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora.” Taarifa ya Tume inafafanua kuwa, “... Tume imejiridhisha kuwa Jeshi la Polisi limevunja  haki ... ya kuishi, haki ya kutoteswa na kupigwa, haki ya usawa mbele ya sheria na haki ya kukusanyika na kutoa maoni.”
Mheshimiwa Spika,
Siku moja baada ya mauaji ya Daudi Mwangosi, Jeshi la Polisi lilianza kampeni kubwa ya kujaribu kuficha ukweli juu ya kuhusika kwake, kwa kuhamishia lawama kwa watu wengine wasiohusika na mauaji hayo. Kwa mfano, Kamanda Kamuhanda alinukuliwa na vyombo vya habari akidai kwamba marehemu Mwangosi alifariki “kutokana na kitu kizito kilichotupwa na waandamanaji.” Aidha, siku iliyofuata Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Polisi Paul Chagonja alidai kwamba baada ya ghasia kudhibitiwa, marehemu Mwangosi alikimbilia walipokuwa polisi na “kitu kama bomu kikarushwa na kundi la watu wanaokimbia hovyo na kumlipua Mwangosi.”
Njama hizi za kuficha ukweli zimeumbuliwa na Ripoti ya MCT/TEF inayobainisha kwamba marehemu Mwangosi “aliuawa chini ya usimamizi wa moja kwa moja wa RPC Michael Kamuhanda.” Ripoti hiyo pia imeelezea kwa kirefu jinsi Jeshi la Polisi lilivyotoa taarifa zinazokinzana juu ya kuhusika kwake na mauaji ya Mwangosi. Hivyo, kwa mfano, wakati Waziri wa Mambo ya Ndani Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi alidai tarehe 4 Septemba 2012 kwamba marehemu aliuawa na bomu la machozi ambalo ‘halikulipuliwa kitaalamu na polisi’, Kamanda Kamuhanda alitokea kwenye televisheni siku iliyofuata “akitangaza habari za kuwatupia lawama wafuasi wa CHADEMA kwa kutupa kitu kizito kilicholipuka na kumuua Mwangosi....”
Mheshimiwa Spika,
Hata Taarifa ya Uchunguzi wa Kifo cha Mwandishi wa Habari wa Channel Ten Bw. Daudi Mwangosi, iliyoandaliwa na Kamati iliyoundwa na Mheshimiwa Nchimbi na kuongozwa na Jaji Stephen Ihema imethibitisha kuhusika kwa Jeshi la Polisi na mauaji ya Marehemu Mwangosi. Baada ya kuzunguka huku na huko ikijaribu kulisafisha Jeshi la Polisi kutoka kwenye lawama ya kumuua Marehemu Mwangosi, Taarifa ya Kamati hiyo inasema: “Hapakuwepo na uhalali wa kutumia Bomu la Kishindo kwani lengo la ulipuaji wake ni ili watu waogope na kukimbia.” Aidha, Kamati hiyo inakiri kwamba “hapakuwepo umuhimu wa kutumia Bomu la Kishindo kwa sababu hata ingekuwa ukamataji tayari askari polisi wapatao sita walikuwepo eneo la tukio.” Kwa misingi hiyo, “… Kamati imeona kwamba … tukio la kuuawa Bw. Daudi Mwangosi na kuumizwa baadhi ya askari polisi halikustahili kabisa.”
Mheshimiwa Spika,
Kuna uthibitisho mkubwa kwamba Serikali hii ya CCM na Jeshi la Polisi wamekuwa wanawalenga kuwaua au kuwaumiza waandishi wa habari wanaoandika zisizowapendeza viongozi wa Serikali au Jeshi la Polisi. Kwa mfano, Ripoti ya MCT/TEF inaashiria kuwa sababu ya Marehemu Mwangosi kuuawa ni kwamba yeye “... ndiye mwandishi pekee aliyemuuliza RPC (Kamuhanda) ‘maswali magumu’ kiasi cha kumkera kiongozi huyo wa jeshi la polisi.” Ripoti hiyo inafafanua kwamba “baada ya mkutano huo na waandishi, ... baadhi ya polisi ... waliwaonya wasiende Nyololo kwa ajili ya kukusanya habari za shughuli za kisiasa za CHADEMA kutokana na uwezekano wa kutokea kwa hali hatarishi.” Aidha, “baada ya mkutano wa waandishi wa habari wa asubuhi katika ofisi za RPC (Kamuhanda), ... askari mmoja mpelelezi alimfuata Mwangosi na kumwambia: ‘Ina maana gani kwenda Nyololo kuandika habari za Chadema ambazo zinaweza kuishia na kifo chako?’” Vile vile, Ripoti ya MCT/TEF inabainisha, ni “... wazi kwamba Polisi walikuwa wanawawinda waandishi wa Iringa ambao walikuwa wakiwajua.”
Mheshimiwa Spika,
Siku tatu baada ya mauaji ya Daudi Mwangosi, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai katika Jeshi la Polisi Robert Manumba alitoa kauli kwa vyombo vya habari kuhusu matukio ya kuuawa kwa waandishi wa habari ambapo alisema “….matukio ya aina hii yapo na yataendelea kuwepo.” Katika kuthibitisha kwamba Serikali hii ya CCM ina sera isiyo rasmi ya kulenga kuwadhuru waandishi wa habari wanaowaandika watawala vibaya na hata kuwaua, kauli ya DCI Manumba imerudiwa tena na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Magessa Mulongo wakati wa sherehe za Mei Mosi mwaka huu jijini Arusha. Kwa mujibu wa vyombo vya habari, Mkuu huyo wa Mkoa aliwatahadharisha waandishi kwa kuwaambia kwamba “unapoingia katika mkakati wa kumdhalilisha kiongozi wa Serikali unaiweka roho yako rehani…. Kuweni makini.”
Mheshimiwa Spika,
Katika Maoni yake kwenye mjadala wa Wizara ya Katiba na Sheria, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni iliyaita matamshi ya DCI Manumba na Mkuu wa Mkoa Mulongo kuwa ni ‘matendo ya kigaidi’ kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia Ugaidi, 2002, ambayo inafafanua ‘matendo ya kigaidi’ kuwa ni pamoja na vitisho vinavyohusu mtu kusababishiwa maumivu au majeraha makubwa kimwili, kuhatarisha maisha ya mtu na vinavyohusu usalama wa umma ambavyo vimelengwa au ambavyo kwa hulka au muktadha wake vinaonekana vimelengwa kutishia umma au sehemu ya umma.
Kwa mara nyingine tena Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa kauli rasmi mbele ya Bunge hili tukufu kama tafsiri hiyo ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi ni sahihi au la. Na kama ni sahihi, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kujua ni kwa nini DCI Manumba na Mkuu wa Mkoa Mulongo bado hawajakamatwa na kufunguliwa mashtaka ya ugaidi hadi sasa? Kama tafsiri hiyo sio sahihi, basi Serikali hii ya CCM itamke mbele ya Bunge lako tukufu kwamba ni sera yake rasmi kwamba waandishi wa habari wanaoiandika Serikali au viongozi wake vibaya ‘wanaweka roho zao rehani’!
Mheshimiwa Spika,
Kauli ambazo zimetolewa na Serikali hii ya CCM ndani ya Bunge lako tukufu zinathibitisha kuhusika kwa Serikali katika, kama sio kupanga basi angalau kubariki, mauaji yanayofanywa na vyombo vya usalama vya Serikali kwa waandishi. Na moja ya kauli za Serikali ambazo zimeifadhaisha na kuisikitisha sana Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ni ile iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Serikali na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Uratibu na Bunge, Mh. William Lukuvi pale alipomsifu Kamanda Kamuhanda wakati wa mjadala wa Wizara ya Mambo ya Ndani: “Katika kitabu hiki cha Kambi ya Upinzani, wamekutaja sana (Kamuhanda), hawawezi kukupongeza. Huko Iringa Kamanda unafanya kazi nzuri sana, usitetereke na makamanda wako wa huko Iringa.”
Ikumbukwe, Mheshimiwa Spika, kwamba mtu anayesifiwa kwa ‘kufanya kazi nzuri sana kule Iringa’ ni yule yule ambaye aliyelaumiwa na Tume ya Haki za Binadamu – ambayo Makamishna wake wote ni wateule wa Rais kwa mujibu wa Katiba – kuwa alikiuka sheria za nchi yetu na misingi ya utawala bora kufuatia tukio la mauaji ya Marehemu Mwangosi! Mtu anayeshauriwa na Waziri Lukuvi kwamba ‘asitetereke’ ni yule yule ambaye MCT/TEF imemhusisha na usimamizi wa moja kwa moja wa mauaji ya Mwangosi. Needless to say, mtu huyu bado yuko huru na hajachukuliwa hatua yoyote licha ya mshangao mkubwa kitaifa na kimataifa!
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa kauli rasmi mbele ya Bunge lako tukufu kama kauli ya Mheshimiwa Lukuvi kuhusu kuhusika kwa Kamanda Kamuhanda na Jeshi la Polisi katika mauaji ya Marehemu Mwangosi ndio msimamo rasmi wa Serikali hii ya CCM. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM kuliambia Bunge lako tukufu ni nini msimamo wake rasmi juu ya Taarifa ya Tume ya Haki za Binadamu na Ripoti ya MCT/TEF kuhusu kuhusika kwa Jeshi la Polisi na Kamanda Kamuhanda katika mauaji ya Marehemu Mwangosi. Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, kimya cha Serikali hii ya CCM juu ya maswali haya muhimu ni ushahidi dhahiri kuwa mauaji haya ni sehemu ya mkakati ulioasisiwa na Serikali hii ya CCM wa kuwanyamazisha waandishi wa habari kwa nia moja tu: kufifisha uhuru wa kupata na kutoa habari muhimu zinazohusika kashfa za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka serikalini.
Mheshimiwa Spika,
Miezi sita baada ya Jeshi la Polisi kumuua Daudi Mwangosi, mwandishi mwingine mwandamizi na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, alitekwa nyara na kuteswa vibaya nje ya nyumba yake baada ya nyendo zake kufuatiliwa na polisi na watu wengine wanaodhaniwa kuwa watumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa na Ujasusi (TISS). Badala ya kuchukua hatua za dhati kuwachunguza na kuwakamata wale wote waliohusika na tukio hilo la kigaidi, Jeshi la Polisi likishirikiana na Idara ya Usalama wa Taifa, maafisa waandamizi katika Ofisi ya Rais Ikulu na viongozi waandamizi wa CCM chini ya Naibu Katibu Mkuu wake Mheshimiwa Mwigulu Nchemba na baadhi ya waandishi habari maslahi, walianzisha kampeni kubwa ya kuipakazia CHADEMA na Mkurugenzi wake wa Ulinzi na Usalama Wilfred Lwakatare kwa madai ya kuhusika na ugaidi kutokana na ushahidi wa kutunga!
Mheshimiwa Spika,
Kwa vile njama dhidi ya CHADEMA na Bw. Lwakatare zimegonga mwamba baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania kuyatupilia mbali mashtaka ya ugaidi dhidi yake, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM kutoa taarifa rasmi mbele ya Bunge lako tukufu juu ya waliohusika na jaribio la kumuua Bw. Kibanda. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM itoe kauli rasmi mbele ya Bunge lako tukufu juu ya kuhusika kwa Jeshi la Polisi, Idara ya Usalama wa Taifa, Ikulu na CCM katika kutengeneza ushahidi wa uongo dhidi ya CHADEMA na Bw. Lwakatare ili kuwapumbaza Watanzania wasihoji shambulio la kigaidi dhidi ya Bw. Kibanda.
Kutoa taarifa ya uongo kwa lengo la kuanzisha mashtaka ya jinai mahakamani au kutengeneza ushahidi wa uongo kwa lengo la kuipotosha mahakama ni makosa ya jinai yenye adhabu ya kifungo cha miaka saba kwa mujibu wa Sheria ya Adhabu ya Tanzania. Ni muhimu kwa ukweli wa jambo hili kujulikana sio tu kwa ajili ya kuwawajibisha kijinai wahusika, bali pia kwa lengo la kulinda demokrasia na utawala wa sheria katika nchi yetu. Kama alivyosema Chris Conybeare, Katibu Mkuu wa Chama cha Mabaraza ya Habari Duniani (WAPC) katika ujumbe wake kwa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Dk. Fenella Mukangara juu ya mauaji ya Marehemu Mwangosi: “Waandishi wa habari wanapouawa demokrasia pia inakufa.”
3. MAELEZO NA UHURU WA HABARI
Mheshimiwa Spika,
Idara ya Habari (MAELEZO) ilikasimiwa majukumu na mali za lililokuwa Shirika la Habari Tanzania (SHIHATA) na Sheria ya Kufuta Shirika la Habari la Tanzania, Na. 7 ya mwaka 2000. Wakati SHIHATA ilikuwa na ukiritimba wa kukusanya habari pamoja na mamlaka ya kusajili waandishi wa habari, ukiritimba huo na mamlaka ya usajili wa waandishi wa habari yalifutwa kabisa kama sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Rais ya Mfumo wa Chama Kimoja au Vyama Vingi vya Siasa Tanzania, 1991 (‘Tume ya Nyalali’), iliyobaini kwamba Sheria ya SHIHATA ilikuwa inakiuka misingi ya uhuru wa mawazo na uhuru wa habari.
Kwa sababu hiyo, majukumu mapya ya Idara ya Habari, kama yalivyofafanuliwa katika kifungu cha 4(2) cha Sheria ya Kufuta SHIHATA, ni pamoja na kutoa, kuendeleza na kuhamasisha uanzishwaji na uendeshaji wa za kukusanyia na kusambaza habari; kukusanya na kusambaza habari na kuishauri Serikali juu ya masuala yanayohusu usambazaji habari na utendaji wa mashirika ya habari. Idara ina ofisi katika baadhi ya mikoa ya Tanzania Bara.
Mheshimiwa Spika,
Tofauti na SHIHATA, Idara ya Habari haina na haijawahi kupewa jukumu la kisheria la kuwa msimamizi wa vyombo vya habari na wanahabari nchini. Hata hivyo, kama ilivyokuwa kwa SHIHATA, Idara hii imekuwa inawauzia waandishi wa habari vitambulisho (press cards) ambavyo vimekuwa vinatumika kama vitambulisho cha kazi kwa waandishi wa habari hapa nchini. Vitambulisho hivyo vimekuwa vinauzwa kwa shilingi za Tanzania elfu ishirini, lakini Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ina taarifa kwamba bei ya vitambulisho hivyo imepanda mwaka huu hadi kufikia shilingi elfu thelathini. Aidha, vitambulisho hivyo hutolewa kila mwaka katika Ofisi za MAELEZO Dar es Salaam na hivyo kusababisha gharama na usumbufu mkubwa kwa waandishi wa habari walioko mikoani.
Mheshimiwa Spika,
Vitendo hivi vya Idara ya Habari ni kinyume cha Sheria ya Kufuta SHIHATA. Kwa sababu hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM itoe kauli rasmi mbele ya Bunge lako tukufu Idara ya Habari imetoa wapi mamlaka ya kusajili waandishi wa habari kwa kuwalazimisha kununua vitambulisho vya uandishi habari. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka Serikali itoe kauli rasmi mbele ya Bunge lako tukufu kama kuna masharti yoyote ya kisheria yanayolazimu waandishi wa habari wasajiliwe na MAELEZO kwa kupatiwa vitambulisho vya kazi na Idara hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Sio tu kwamba Idara ya Habari imejitwalia mamlaka ya kusajili waandishi wa habari kwa kuwalazimisha kununua vitambulisho vya taaluma yao, lakini pia imeendelea kuwa kikwazo kikubwa kwa kupanuka kwa demokrasia na uhuru wa habari katika nchi yetu. Historia yake inaanzia miaka ya mwanzo ya utawala wa kikoloni wa Kiingereza wakati walipotunga Sheria ya Magazeti ya 1928. Chini ya Sheria hiyo, wakoloni walidhibiti ukuaji wa vyombo vya habari vya wenyeji wa Kiafrika kwa kuviwekea masharti ya kusajiliwa baada ya kutoa dhamana ya fedha taslimu.
Marekebisho ya Sheria hiyo yaliyofanywa mwaka 1952 yaliweka masharti magumu zaidi ya usajili wa magazeti pamoja na kuongeza kiwango cha dhamana kutoka pauni za Kiingereza 160 hadi pauni 520. Kwa mujibu wa Martin Sturmer katika kitabu chake The Media History of Tanzania, wakati magazeti ya Wamisionari na yale yaliyokuwa yanaunga mkono sera za utawala wa kikoloni katika Tanganyika hayakudaiwa kulipa dhamana, magazeti yaliyokuwa na mrengo wa upinzani wa sera za dola ya kikoloni yalilazimika kulipa dhamana hiyo.
Baadae mwaka 1955 dola ya kikoloni iliongeza udhibiti zaidi wa vyombo vya habari kwa kuingiza katika Sheria ya Adhabu vifungu vipya vilivyokataza uchapishaji wa jambo au taarifa yoyote lenye uwezo wa kuleta chuki dhidi ya serikali ya kikoloni au watendaji wake. Kama anavyosema Sturmer, kutokea hapo sheria hiyo ya uchochezi ndio imekuwa kizingiti kikubwa kwa uhuru wa magazeti katika Tanzania. Haiwezi kuwa ajabu kwamba wahanga wa kwanza wa sheria hiyo ya uchochezi walikuwa mabwana Kheri Rashidi Baghdelleh na Robert Moses Makange waliokuwa wahariri wa gazeti la Mwafrika; na mhariri wa gazeti la Sauti ya TANU aliyejulikana kama Julius Kambarage Nyerere!
Mheshimiwa Spika,
Kitu cha ajabu ni kwamba sheria iliyotungwa na wakoloni wa Kiingereza kwa lengo la kuwadhibiti wenyeji wa Kiafrika wasidai uhuru au kuanika uchafu na uonevu wa dola ya kikoloni haikufutwa mara baada ya uhuru. Badala yake, sera za habari za dola ya uhuru sio tu zilipokea na kuzidisha masharti ya kisheria dhidi ya uhuru wa habari kwa kutunga Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 iliyoongeza makali ya sheria ya uchochezi, bali pia zilitaifisha magazeti na vyombo vingine vya habari binafsi vilivyokuwepo wakati wa uhuru.
Hivyo, kwa mfano, Shirika la Utangazaji la Tanganyika (TBC) lilitaifishwa kwa Sheria ya Bunge ya tarehe 16 Machi 1965 na kubatizwa jina jipya la Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD). Aidha, tarehe 5 Februari, 1970, gazeti binafsi la The Standard lilitaifishwa na Serikali. Na ilipofika tarehe 26 Aprili, 1972, The Daily News, gazeti jipya la Serikali lilianzishwa kwa kuunganisha The Standard na gazeti la The Nationalist lililokuwa linamilikiwa na TANU. Hivyo basi, kama anavyosema Sturmer katika historia yake ya vyombo vya habari Tanzania, “kufikia mwaka 1976 Serikali ya Nyerere ilishafanikisha lengo lake kuu la sera ya habari – kuwa na udhibiti juu ya vyombo vyote vikuu vya habari....”
Mheshimiwa Spika,
Utaratibu huu wa udhibiti juu ya vyombo vya habari kwa kutumia Sheria ya Magazeti ulishambuliwa na Tume ya Nyalali kwa kukiuka matakwa ya ibara ya 18 ya Katiba inayotoa uhuru wa mawazo na uhuru wa habari. Kwa maneno ya Tume hiyo, Serikali inakiuka uhuru wa mawazo na wa habari “... kwa kujihusisha na kuchuja habari zinazotolewa kwa wananchi.” Tume ilipendekeza marekebisho makubwa katika Sheria ya Magazeti “... ili kuruhusu uhuru mkubwa zaidi wa habari na wa mawazo na kulegeza uchujaji wa habari.” Mapendekezo haya ya Tume ya Nyalali hayajatekelezwa hadi leo hii, zaidi ya miaka ishirini na mbili tangu Tume hiyo iwasilishe Taarifa yake kwa Rais Ali Hassan Mwinyi.
Mheshimiwa Spika,
Wakati Tanzania imebakia mateka wa sera za habari za kikoloni na za utawala wa kiimla wa chama kimoja, jirani zetu wa Kenya na marafiki zetu wa Zimbabwe wamepiga hatua kubwa katika kupanua uhuru wa habari. Hivyo, kwa mfano, Katiba Mpya ya Jamhuri ya Zimbabwe iliyopitishwa kwa kura ya maoni ya wananchi wa nchi hiyo mwezi Februari mwaka huu inatoa uhuru wa mawazo ambao unajumuisha uhuru wa kutafuta, kupokea na kusambaza mawazo na habari nyingine; uhuru wa mawazo ya kisanii na wa utafiti wa kisayansi na uhuru wa taaluma.
Aidha, Katiba hiyo inatoa uhuru wa habari ambao ni pamoja na ulinzi wa vyanzo vya habari vya waandishi wa habari; na uhuru wa uanzishaji wa vyombo vya utangazaji ambavyo havitakiwi kuwa chini ya udhibiti wa serikali au maslahi ya kisiasa au kibishara. Vile vile, Katiba Mpya ya Zimbabwe inavilazimu vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Serikali kuwa huru kuamua mambo gani ya kutangaza; kutokupendelea na kutoa fursa sawa kwa ajili ya kutangaza maoni tofauti na mawazo yanayokinzana.
Mheshimiwa Spika,
Katiba Mpya ya Zimbabwe inatoa pia uhuru wa taarifa (access to information). Hivyo, kwa mfano, kila raia au mkazi wa kudumu wa Zimbabwe, ikiwa ni pamoja na makampuni na vyombo vya habari, ana haki ya kupatiwa taarifa yoyote inayodhikiliwa na Serikali au na taasisi au shirika lolote la serikali katika ngazi zote, kama taarifa hiyo inahitajika kwa ajili ya maslahi ya uwajibikaji kwa umma. Zaidi ya hayo, kila mtu, ikiwa ni pamoja na vyombo vya habari vya Zimbabwe, ana haki ya kupatiwa taarifa inayoshikiliwa na mtu yeyote, pamoja na Serikali, kama taarifa hiyo inahitajika kwa ajili ya kufurahia au kulinda haki yake. Kama ilivyo kwa Zimbabwe, Katiba Mpya ya Kenya nayo pia imetoa uhuru mpana wa habari kwa wananchi wa Kenya.
Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, ni fedheha kwamba nchi yetu iliyokuwa ya kwanza kupata uhuru katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini inaelekea kuwa ya mwisho katika masuala ya uhuru wa habari kwa watu wake. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM kulieleza Bunge lako tukufu ni lini italeta muswada wa sheria kwa lengo la kufuta urithi huu wa fedheha wa sheria za kikoloni ili Tanzania iendane na karne mpya ya uhuru wa habari na wa mawasiliano.
Mheshimiwa Spika,
Kwa sasa vyombo vya habari vya Serikali yaani, Radio na Television za Taifa ndio vinatoa matangazo kwa wananchi kuhusu kile kinachoendelea Bungeni. Kwa bahati mbaya ni kwamba Radio ya Taifa ambayo inasikilizwa na watanzania wengi wa hali ya chini na kati katika maeneo mengi ya mijini na vijijini wanashindwa kusikiliza mijadala inayoendelea Bungeni, kwani matangazo yanakatishwa pindi kipindi cha maswali na majibu kinapomalizika. Matangazo ya mjadala wa Bunge yanaendelea kurushwa kwenye Television ya Taifa hadi Bunge linapoahirisha shughuli zake kwa siku.
Mheshimiwa Spika,
Huku ni kutowatendea haki watanzania wengi kwa kuwapa fursa kusikiliza nini wawakilishi wao wanachokiongea katika mijadala mbalimbali Bungeni. Kambi Rasmi ya Upinzani inaona sasa ni muda mwafaka kwa sekta binafsi nazo kufanyakazi hiyo ambayo inaonyesha imevielemea vyombo hivyo vya serikali na kuondoa ukiritimba uliopo wa kurusha matangazo ya Bunge.
3.2  Matangazo ya serikali kwenye vyombo vya habari
Mheshimiwa Spika,
Suala la matangazo ya serikali katika vyombo vya habari si kwamba limekuwa likitumika kuminya uhuru wa habari katika baadhi ya vyombo vya habari hususan vinavyoonekana kuwa vinafanya utafiti katika habari zake kwa masuala mbalimbali ya kisiasa, kijamii na kiuchumi na hivyo kuweka hadharani mapungufu na uchafu wa Viongozi waliopewa dhamana na wananchi.
Mheshimiwa Spika,
Suala hilo la matangazo badala ya kuviimarisha vyombo vya habari ili viweze kusimama na kufanyakazi bila ya kuingiliwa, sasa linatumika kama njia ya kufifisha uhuru wa kutafuta na kutoa habari na kuvifanya vyombo vya habari kuachana na uhandishi wa uchunguzi na hivyo kukiuka haki za walaji za kupata taarifa kwa mujibu wa Ibara ya katiba ya 18 (d).  
Mheshimiwa Spika,
Sasa kumezuka mtindo mwingine wa kuhamishia raslimali za Serikali kwenye chama kwa ajili ya kuiokoa CCM na wanasiasa wengine. Tutatoa mfano hai wa hivi karibuni kabisa.  Kwa wafuatiliaji wa habari katika vyombo vya habari, bila shaka watakumbuka kuwa siku ya Mei Mosi, Gazeti la CCM linaloitwa Uhuru, lilikuwa na kurasa 79, ikiwa ni ongezeko la karibu mara tatu ya gazeti hilo linavyotoka kwa siku za kawaida kama halina matangazo.
Kinachoweza kuwa kimewasikitisha wafuatiliaji makini wa masuala ya habari ni kwamba matangazo hayo hayakuwa ya watu au kampuni binafsi yalikuwa ni matangazo ya serikali na taasisi zake, kwa maana ya kwamba yaligharimu mamilioni ya shilingi za walipa kodi wa Tanzania, ambayo kimsingi yalipotumika ‘hovyo’ kama tutakavyoonesha kwa hoja hapa;
Mheshimiwa Spika,
Tatizo hapa si tu kwamba gazeti hili ni la CCM, bali pia kuna masuala ya msingi kadhaa ambayo kwa kweli mtu yeyote makini, anayejua biashara ya matangazo, hasa kutangaza kupitia vyombo vya habari, anapaswa kuzingatia mara zote kabla hajaamua kutumbukiza mamilioni kwa ajili ya kujitangaza;
Kwanza, kama chombo hicho ni gazeti, basi linapaswa kuwa na wasomaji wengi na pia mzunguko mkubwa sokoni kwa maana ya kuwafikia watu wengi kutokana na kusambaa maeneo mengi ndani (na nje ikibidi) ya nchi. Mfuatiliaji yeyote makini wa vyombo vya habari anajua wazi kuwa gazeti hilo la CCM, halina sifa hizo.
Kama serikali na taasisi zilizotumia gazeti hilo la CCM kama njia ya kujitangaza zingekuwa makini na matumizi halali ya fedha za Watanzania, lazima zingezingatia kanuni za kawaida kabisa; yaani kuhakikisha wanapata wasomaji na soko kubwa katika bidhaa na huduma zao wanazotangaza, hivyo wangepaswa kutangaza katika magazeti yanayosomwa na yenye mzunguko mkubwa.
Mheshimiwa Spika,
Kinachoonekana hapa ni kwamba, baada ya njia nyingine za kifisadi za kupata fedha kuisaidia CCM kushtukiwa, sasa zimebuniwa mbinu nyingine za kifisadi za kusaka fedha kwa ajili ya chama hicho, mojawapo ikiwa ni hii ya utoaji wa matangazo kwa vyombo vya habari vya CCM, visivyokuwa na sifa stahili. Haya ni matumizi mabaya ya matangazo yenyewe na fedha za umma!
Ni namna ile ile ya kutoa zabuni kwa Kampuni ya CCM, ifanye upanuzi wa eneo la bandari kwenye eneo la CCM, bila makampuni yenye uwezo kushindanishwa ili kupata moja iliyo makini na yenye vigezo vya kufanya kazi husika.
3.3 TCRA NA UANGALIZI WA VYOMBO VYA HABARI VYA KIELEKTRONIKI
Mheshimiwa Spika, TCRA ndiyo yenye mamlaka ya kusimamia vyombo vya elkroniki kama Radio na Televisdion, lakini imeshindwa kabisa kusimamia vyombo hivyo walivyovipatia leseni ya kufanyakazi, kwani  baadhi ya vituo ukisikiliza vinafanya uchochezi wa kisiasa, kidini, ukabila  wa  wazi lakini vimeachwa  hadi matatizo ya udini yaliposhika kasi ndio  Serikali ikaanza kukimbia kuchukua hatua.
Mheshimiwa Spika, Hivi sasa intaneti haitawaliwi na sheria yoyote nchini, baadhi ya vipindi vya redio na televisheni havizingatii maadili ya Kitanzania, maeneo mengi ya vijijini hayana huduma ya televisheni. Kambi Rasmi ya Upinzani inasema kuwa huu ni udhaifu wa wazi kwa mamlaka hiyo iliyopewa jukumu la kusimamia. Hivyo basi tunaitaka Serikali itoe kauli kuhusiana na udhibiti wa TCRA katika suala hilo.
ka 2013)

3.4 SHIRIKA LA UTANGAZAJI TANZANIA (TBC)
3.4.1 TBC na matukio muhimu ya Kitaifa
Mheshimiwa Spika,Ikiwa imepita takribani miaka mitano tangu Mhe. Raisi alipozindua rasmi Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) mwezi mei 2008. Kwa kuwa, pamoja na uchakavu na ukosefu wa vifaa TBC imeweza kupanua masafa yake ya utangazaji karibu nchi nzima ,na kwa kuwa hili ni shirika la umma, ni matumaini makubwa kwa watanzania kuwa TBC ingekua mstari wa mbele katika kuripoti na kutangaza matukio muhimu yanayoendelea katika nchi yetu.
 Mheshimiwa Spika, Kwa masikitiko makubwa TBC imekua nyuma katika kuripoti matukio muhimu na badala yake imekua ikiweka vipindi visivyoendana na matukio yanayolikabili taifa. Hii ni dharau kwa watanzania wengi hasa ukizingatia kuwa hili ni shirika la umma na si la mtu binafsi hivyo wajibu wake mkubwa ni kumpa taarifa mtanzania kwa wakati hata pale inaposhindwa kutoa taarifa ama kuwepo eneo la tukio basi lazima programu zake ziendane na hali halisi.
Mheshimiwa Spika, Kwa masikitiko makubwa wakati wa ajali ya meli ya MV Skagkit iliyotokea mwaka jana, 2012, wakati kuna taarifa za awali za ajali, TBC ilikua ikiweka na kupiga muziki wa taarabu bila ya kuzingatia uzito wa ajali ile, hata siku iliyofuata kwa ajili ya shughuli za uokoaji TBC iliendelea kuweka programu ambazo hazikuendana na uzito wa tukio lile licha ya kuwa mamia ya watanzania walipoteza maisha na huku tafrani ikizuka kwa baadhi ya watanzania ambao ndugu zao walikua katika tukio lile.
Mheshimiwa Spika,Katika kuonesha kuwa TBC haijifunzi kutokana na makosa, ama labda imekosa uongozi wenye weledi na umakini tangu kuisha kwa ajira ya mkurugenzi wao makini Tido Muhando, mwezi wa April 2013 ambako kulikua na mlipuko wa bomu Arusha,tukio ambalo lilikuwa kubwa kwenye historia ya nchi yetu kwani ni mara ya kwanza tukio kama hilo kutokea, TBC iliendelea na urushaji wa matangazo na vipindi tofauti huku televisheni na vituo vingine vya binafsi vilikuwa vinajulisha taifa kuhusiana na tukio hilo.
Mheshimiwa Spika, Tukiwa katika mijadala ya muhimu ya mustakabali wa taifa letu, ambapo tunajadili na kupitisha bajeti kwa ajili ya watanzania, TBC hukata matangazo ya vipindi vya Bunge wakati uwasilishaji wa hoja muhimu ukiendelea. Wakati wa hotuba ya Mambo ya ndani, wakati msemaji mkuu wa kambi ya upinzani anakaribia kuanza kusoma maoni ya Kambi ya Upinzani , TBC walikata matangazo na kuweka sherehe za Mwenge.
Mheshimiwa Spika,Pamoja na hayo yote, TBC bado inaendelea na kauli mbiu yake ya 'Ukweli na Uhakika'  kauli ambayo haiendani na uhasilia wa uratibu wa vipindi vyake vya  matangazo na uwasilishaji wa taarifa kwa umma. Mara nyingi kwenye mijadala na hoja nzito ambazo Serikali inakua ina hali mbaya, matangazo ya bunge hukatwa kwa kisingizio kuwa mitambo au matatizo ya kiufundi yametokea, mbona matangazo au hitilafu za ufundi hazitokei katika sherehe za Mwenge?Ama hitilafu kwenye kuonesha ujio wa rais wa China ? TBC inatumika na imeendelea kutumiwa na Serikali ya CCM katika kuminya haki ya mtanzania ya kupata habari si kwa sababu ya ufinyu wa bajeti peke yake bali kuwaridhisha watawala. Lazima TBC ibadilike na kujua kuwa ina dhamana katika kupeleka habari na taarifa sahihi kwa umma kwa wakati na si kwa kuendeshwa kama roboti.
4.0   MASUALA YA VIJANA
4.1 UUNDAJI WA BARAZA LA VIJANA LA TAIFA
Mheshimiwa Spika, suala la mchakato wa uundwaji wa Baraza la Taifa la Vijana, sasa umekuwa si tu wimbo bali zimwi la muda mrefu linaloiandama serikali ya CCM na imeshindwa kabisa kuepukana nalo.Sera ya zamani ya maendeleo ya vijana ya mwaka 1996 ilitamka kwamba kutaanzishwa  Baraza la Vijana na suala hilo kurudiwa katika Sera mpya ya mwaka 2007; hata hivyo Serikali imekuwa ikiwepa kuhakikisha kwamba matakwa hayo ya sera tajwa yanatekelezwa pamoja na kuwa suala hilo linahusu mustakabali wa maendeleo ya vijana nchini.  Kambi Rasmi ya Upinzani inatambua kwamba katika ilani za uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 vyama mbalimbali viliahidi kuhakikisha kwamba Baraza la Vijana la Taifa linaundwa.
Mathalani, CHADEMA katika Ilani yake 2010-2015 kipengele  6.4.1 (viii) ilitamka “Kwa kuwa vijana ndio kundi kubwa hapa nchini, na kwa kuwa uhai wa muda mrefu wa taifa letu upo mikononi mwa vijana, Serikali ya CHADEMA itawezesha vijana kuunda Baraza la Vijana (BAVITA) ambalo limekwamishwa na Serikali ya CCM kwa muda mrefu”.
CCM nayo kupitia ilani yake ya katika kipengele 80 (k) “Kuhamasisha ushiriki wa vijana katika ngazi mbalimbali za maamuzi ikiwa ni pamoja na kukamilisha uanzishaji wa Baraza la Vijana”.Hivyo, Kambi Rasmi ya Upinzani inatarajia kwamba wabunge wa pande zote katika suala hili la kuanzishwa kwa Baraza la Vijana la Taifa kuungana kuwa kitu kimoja kuisimamia Serikali itekeleze Sera na ahadi badala ya kuitetea kwa udhaifu iliyouonyesha.
Mheshimiwa Spika; Katika  Hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo juu ya mapitio ya utekekelezaji kwa mwaka 2010/2011 na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2011/2012 tulihoji ni lini hasa Serikali ingewezesha kuanzishwa kwa Baraza la Vijana la Taifa. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani ilirudia tena kuhoji suala hili wakati wa mjadala wa mapitio ya utekelezaji kwa mwaka 2011/2012 na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2012/2013. Hata hivyo, kwa nyakati zote hizo Serikali katika majumuisho imekuwa irudia tena ambayo imekuwa ikitolewa kwa miaka zaidi ya miaka 17 ya kukamilisha mchakato wa kuanzishwa kwa baraza  la Vijana la Taifa; bila utekelezaji kamili na wa haraka.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inayo taarifa kwamba kufuatia hali hiyo mwezi Januari 2013 mbunge wa Ubungo, Mheshimiwa  John Mnyika aliwasilisha kwa  Katibu wa Bunge muswada binafsi wa sheria kuwezesha kuundwa kwa Baraza la Taifa la Vijana.  Katika Hotuba yake juu ya mapitio ya utekelezaji kwa mwaka 2012/2013 na makadirio ya mapato na matumizi ya mwaka 2013/2014 ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Mheshimiwa Freeman Mbowe alihoji ni lini Serikali itawasilisha bungeni miswada binafsi ya wabunge ukiwemo muswada huo.
Mheshimiwa Spika; kwa mujibu wa Kitabu cha hoja za wabunge na majibu ya Serikali kuhusu Hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2013/2014 juu ya muswada huo “Ofisi ya Katibu wa Bunge imemwandikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupata ufafanuzi kama Muswada unaohusu uanzishwaji wa Baraza la Vijana la Taifa hautakuwa na athari zozote za kiwango cha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina kama ilivyoanishwa katika Kanuni ya 95 ya Kanuni za Kudumu za Bunge toleo la mwaka 2007”.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inayo taarifa kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali ametoa ushauri kuwa muswada huo hauwezi kuchapishwa katika gazeti la Serikali kwa kuwa umekiuka masharti ya ibara ya 99 ya Katiba ya Nchi. Kambi Rasmi ya Upinzani ina taarifa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ametoa ushauri huo kwa kuwa muswada unalenga pamoja na mambo mengine kupitia kifungu cha 31 kipengele cha kwanza kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa madhumuni ya kugharamia shughuli za baraza la vijana la taifa, mipango ya baraza na kutekeleza miradi ya vijana kwa ajili ya maendeleo ya vijana.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza iwapo katika kutoa ushauri huo ilizingatia kwamba kifungu cha 31 kipengele cha pili cha muswada huo kinataja vyanzo mbalimbali vya fedha za mfuko ikiwemo kutaja kuwa  fedha za mfuko zitatokana na fedha zilizotengwa na Serikali na Bunge kwa ajili ya Baraza kwa mujibu wa Ibara ya 135 kifungu cha pili cha katiba ya Nchi.
Mheshimiwa Spika; Ibara ya 135 (2) ya Katiba ya Nchi inatamka  kuwa “fedha ambazo hazitawekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ni zile zote ambazo zimetajwa na sheria ya kwamba zitumike kwa shughuli maalum au ziwekwe kwenye mfuko mwingine kwa ajili ya matumizi maalum”.
Kambi Rasmi ya Upinzani inataka ufafanuzi kutoka kwa Serikali ni kwanini haikutoa ushauri wa kufanya ibara hiyo ya Katiba ya Nchi kutumika kuwezesha kuanzishwa kwa Baraza la Vijana na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana bila kufungwa na Ibara ya 99 ya Katiba kifungu cha kwanza ambacho kimeweka masharti kuwa “Bunge halitashughulikia jambo lolote kati ya mambo yanayohusika na ibara hii isipokuwa kama Rais amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na Bunge na pendekezo hilo la Rais liwe limewasilishwa kwenye Bunge na Rais.”
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inatambua kuwa Kifungu cha pili kinataja mambo yanayohusika na ibara hiyo ya 99 ni pamoja na muswada wa sheria kwa ajili ya “kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali au mfuko mwingine wowote au kubadilisha kiwango hicho kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza”. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka 17 maraisi na mawaziri wenye dhamana wamekuwa wakiacha kutumia madaraka hayo ya kikatiba kuleta muswada bungeni wa kuwezesha kuundwa kwa Baraza la Vijana la Taifa; hivyo kitendo cha Serikali kupitia kwa Mwanasheria Mkuu kuendeleza vikwazo hata kwa muswada binafsi wa mbunge kuhusu suala hilo kunaashiria ukosefu wa nia njema kwa upande wa Serikali katika mchakato wa kuundwa kwa Baraza la Vijana la Taifa.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa mwito kwa Serikali na Uongozi wa Bunge kuwezesha muswada wa Baraza la Taifa la Vijana kuwasilishwa kwenye mkutano huu wa kumi na moja wa Bunge unaoendelea iwe ni kupitia muswada binafsi, muswada wa kamati au muswada wa Serikali kwa kuwa tayari maoni yameshakusanywa kwa miaka mingi kinachohitajika sasa ni utekelezaji wa Sera na ahadi.
Kambi rasmi ya upinzani, Tunataka kujua msimamo wa Serikali katika bunge hili, ituambie muda mahsusi (time frame) lini hasa mchakato wa uundwaji wa baraza hilo utakamilika na hatimaye kuanza kufanya kazi kwa Baraza la Vijana la Taifa kwa ajili ya maslahi ya vijana wa nchi hii. Iwapo Serikali ya CCM itaendelea kupiga dana dana muswada wa sheria wa kuundwa kwa chombo hiki muhimu kwa maendeleo ya vijana; Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni inayoongozwa na CHADEMA itawahamasisha vijana nchi nzima kuelekeza nguvu na uwingi wao katika kuishinikiza Serikali sikivu ya CCM, kufanya mabadiliko yenye kuwezesha matakwa ya vijana kutekelezwa kwa wakati.
4.2 Sekta ya maendeleo ya vijana
Mathalani katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka jana, kazi pekee ambazo zimekuwa zikipewa kipaumbele na sekta hii ni kukimbiza mbio za mwenge na kuratibu maadhimisho ya wiki ya vijana kitaifa.
Aidha kwa mwaka jana, sekta hii, kwa mujibu wa maelezo ya wizara, ilifanya uratibu wa mafunzo ya kuwawezesha vijana kuwa na mawazo ya kimkakati ya ubunifu na ujasiriamali katika mikoa ya Mbeya, Mwanza, Mara, Morogoro, Geita, Njombe, Kigoma na Arusha!
Kambi ya Upinzani Bungeni inaitaka wizara kulieleza bunge lako hili kwa takwimu na maelezo ya kina ni kiasi gani mbio za Mwenge ambazo zimekuwa zikitumia mabilioni ya fedha ‘kuingiza’ mamilioni ya fedha, zimeweza kuwasaidia vijana wa Tanzania kupambana na tatizo kubwa linalowakabili la ukosefu wa ajira na ujira wenye staha.
Je, wizara inaweza kutoa takwimu hapa kuonesha namna ambavyo mabilioni ya fedha waliyotengewa mwaka jana kwa ajili ya uratibu wa mafunzo ya ubunifu na ujasiriamali, wameweza kufundisha vijana wangapi na katika maeneo yapi hasa ya utaalamu na taaluma, kwa kiwango gani ili kuweza kuwajengea uwezo wa kuajiriwa na kujiajiri kwa ajili ya kupata ujira wenye staha.
4.3 Mikataba, mipango, sera na utekelezaji
Mheshimiwa Spika, Mwaka mzima baada ya serikali kusimama hapa bungeni na kulipatia bunge lako matumaini na kutoa ahadi kemkem wakati wa kupitisha Azimio la Mkataba wa Kimataifa wa Vijana wa Afrika, hadi sasa wizara hii imeendelea kusuasua na kuzidi kutoa ahadi juu ya ahadi kuhusu kuweka utaratibu wa kisheria wa utekelezaji wa mkataba huo.
Mheshimiwa Spika, Baada ya bunge hili katika mkutano wake wa mwezi Februari mwaka jana kupitisha azimio hilo, katika hotuba ya bajeti mwaka jana, wizara hii ilisema kuwa, kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeanza kuchukua hatua za kuandaa muswada wa sheria ya utekelezaji wa mkataba huo.
Mheshimiwa Spika, Lakini katika kuonesha kuwa serikali hii haikuwa wala haina nia ya dhati kuweka utaratibu wa kisheria ili kusaidia utekelezaji wa azimio hilo, katika malengo yake ya utekelezaji wa mpango wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2013/14, imeshindwa kabisa kuzungumza chochote juu ya suala hilo.
Kambi rasmi ya Upinzani, inaona kuwa huu ni mwendelezo tu wa serikali hii ya CCM kuendelea na utamaduni wake wa kuwatelekeza,kuwapuuza na kuwadharau vijana wa nchi hii.Aidha , tunataka kujua ni lini wizara italeta mswada huo hapa Bungeni kwa ajili ya kupitishwa na Bunge na kuwa sheria.
4.4  Mbio za Mwenge wa Uhuru
Mheshimiwa Spika,mara kadhaa sasa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni imekuwa ikihoji maswali anuai kuhusu jambo hili lakini bahati mbaya yamekuwa yakitolea majibu yasiyokidhi haja. Nasi kwa ajili ya kutimiza wajibu wetu wa kuwasemea Watanzania wasiokuwa na sauti ndani ya mhimili huu, tutaendelea kukumbushia na kuhoji hadi majibu mujarabu yakakapotolewa.
Mathalani, katika moja ya malengo ya utekelezaji wa mpango wa bajeti wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ni ukimbizaji wa Mwenge wa Uhuru. Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, si tu kwamba imekuwa ikihoji maana nzima ya kuendelea kutumia mabilioni ya walipa kodi maskini kwenye mbio za mwenge, badala ya kuuweka makumbusho na kuufanya kuwa moja ya vivutio vya kiutamaduni.
Mheshimiwa Spika, mtu yeyote makini hawezi kuona mantiki ya mbio za mwenge ambazo zimekuwa zikitumia mabilioni ya fedha kuzunguka nchi nzima kuzindua miradi ya mamilioni ya watu binafsi! Kama vile bar, nyumba za kulala wageni na mingineyo.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha tumeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukimbiza mwenge, randama ya wizara inaonyesha kuwa ,kijifungu 210319 zinaombwa shilingi 3,000,000 ‘kwa ajili ya kulipa matibabu na bima kwa wakimbiza Mwenge wa uhuru’,kijifungu 210315 zinaombwa shilingi 64,200,000 ‘kwa ajili ya kulipa posho za kujikimu kwa wakimbiza mwenge wa uhuru, kijifungu 220302 zinaombwa shilingi 57,750,000 ‘kwa ajili ya kununulia dizeli ya magari mawili yatakayotumika kwenye sherehe za uzinduzi na kilele cha mbio za mwenge wa uhuru’,.
Aidha, kijifungu 220604 sare, wizara inaomba kiasi cha shilingi 8,886,000 ‘kwa ajili ya sare za wakimbiza Mwenge kitaifa’, kijifungu 220708 zinaombwa shilingi 25,000,000 ‘kwa ajili ya kukodi ndege kwa shughuli za mbio za Mwenge wa uhuru’, kijifungu 220709 ,zinaombwa jumla ya shilingi 7,200,000 zinaombwa kwa ‘ajili ya ununuzi wa vifaa vya mkutano wa tathimini ya mbio za mwenge wa uhuru’,kijifungu 221005 zinaombwa shilingi 78,500,000 ‘kwa ajili ya posho ya safari za kikazi ndani ya nchi kwa wakimbiza mwenge kitaifa’ ,kijifungu 221406 zinaombwa shilingi 15,000,000 kwa ajili ya ‘...kuandaa tuzo ...wakati wa mbio za mwenge’,
Mheshimiwa Spika, Pamoja na kutengwa kwa fedha zote hizi kiasi cha shilingi 259,536,000 pesa ambazo zingewekezwa kwenye mfuko wa kuwakopesha vijana zingeweza kuwakwamua kwenye tatizo la ajira, serikali inaomba fedha hata kwa ajili ya kukodi ndege kwa ajili ya kukimbiza mwenge , mwaka huu tutashuhudia mwenge ukikimbizwa angani! bado mwenge umeendelea kupoteza mwelekeo
Mheshimiwa Spika, katika kuthibitisha kuwa Mwenge umepoteza mwelekeo katika mwaka huu wa fedha katika kijifungu 230600 ‘matengenezo ya mashine’ katika kijifungu 230605 ‘mikataba ya matengenezo kutoka nje’ randama uk.86 inasema ‘mwaka 2013/2014 sh.366,000 zinaombwa kwa ajili ya kupata wataalamu nje ya wizara kwa ajili ya kutoa huduma ya matengenezo ya chombo cha Mwenge wa uhuru’. Unaweza kuona kuwa chombo hiki kinatafutiwa mtaalamu kutoka nje ya wizara na malipo ya mtaalamu huyo ni shilingi laki tatu! Hii ni dalili ya wazi kuwa chombo hiki yafaa kikawekwa kwenye jumba letu la makumbusho.
Kambi Rasmi ya Upinzani, haikubaliani na serikali kutumia kiasi cha shilingi 259,536,000 kwa ajili ya posho za kukimbiza mwenge, tunataka fedha hizi ziingizwe kwenye programu za maendeleo ya vijana ili waweze kujiajiri na mwenge uwekwe kwenye jumba la makumbusho, kwani umekuwa ni kero kwa wananchi vijijini kuchangishwa fedha za mwenge bila hata kujua zinaenda kufanya nini.

5.0 USIMAMIZI WA MICHEZO NA MUSTAKABALI WAKE KWA TAIFA
Mheshimiwa Spika, Pamoja na hazina ya wanamichezo nchini, lakini michezo mingi nchini haipewi kipaumbele na serikali.Mara kadhaa vyombo vya habari vimekua vikiupa kipaumbele mchezo wa soka kana kwamba michezo mingine haina tija kwa taifa. Leo hii kuna michezo ambayo kama ikipewa uzito wa kutosha italeta taifa hili heshima katika medani za kimataifa.
Mheshimiwa Spika,Labda kwa kuwa tumeshindwa kuwekeza kwenye michezo mingine kwa vipaumbele ambavyo vinaweza kuiweka Tanzania katika ramani ya michezo, hii imefanya michezo hiyo kufa na hazina ya taifa ya vipaji mbalimbali nayo kufa bila kutumika. Mfano katika michezo ya 30 ya Olimpiki iliyofanyika jijini London, Uingereza Julai mwaka 2012, Tanzania ilipeleka jumla ya wanamichezo 7 ambao hawakuambulia medani yoyote .
Mheshimiwa Spika,Wakati Afrika ya Kusini ilipeleka wanamichezo 125 kwa jumla ya michezo 17,sisi tulipeleka 7 tu. Kuna jambo kuu la kujifunza kutokana  na jinsi ambavyo Serikali, sikivu , ya CCM inaendesha nchi yetu. Jambo ambalo linastaajabisha na lenye maswali mengi yasiyo na majibu, Je Wizara hii ina kazi gani? Ina mikakati gani ya jumla katika kusimamia vyama vya michezo nchini ili viwe na tija? Je wizara hii ina uchungu na fedha za kodi za wananchi hii kwa matumizi yasiyo na tija katika sekta ya michezo? Je taifa hili limekosa kutumia michezo kama njia mojawapo ya kutangaza jina la Tanzania na kuliweka katika ramani ya dunia kwa kuwa na wanamichezo bora na si bora wanamichezo?
Kambi rasmi ya Upinzani, inapendekeza kwa msisitizo mkubwa kuwa katika kipindi hiki ambacho taifa letu lipo katika mpasuko na mgawanyiko wa masuala mbalimbali kuanzia udini,mchakato wa katiba nk , katika kipindi hiki ambacho mshikamano na umoja wetu kama taifa upo katika hatari ya kusambaratika, jambo ambalo linaweza kutuunganisha kama taifa moja lililobakia ni michezo .
Hivyo basi tuhakikishe kwamba timu ya taifa ya mpira wa miguu inaandaliwa vya kutosha na tuweze kuingia kwenye fainali za kombe la dunia ifikapo 2014, tuna kazi ndogo ya kuifunga Morocco kwao, tunatakiwa kuifunga Ivory coast hapa kwetu, tunaamini inawezekana kama mipango madhubuti ikiwekwa sasa.
5.1 Chama cha Riadha Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Mwaka 2012, katika mashindano ya taifa ya riadha kulikua na changamoto kubwa ya wanariadha kushiriki katika mashindano ya taifa bila ya maandalizi ya kutosha, huku baadhi ya wanariadha wakishiriki katika mashindano bila ya kuwa na viatu. Haya ni mashindano ya taifa, Chama cha Riadha (RT)nchini, kimeyandaa bila ya kuwa na mikakati ya kitaifa ya kuhakikisha kuwa  vigezo na viwango vimefuatwa.
Aidha , chama hiki kimekuwa kikilalamikiwa sana na wadau wake kutokana na hisia kwamba kunakuwa na upendeleo katika kutuma wanariadha ambao wamekuwa wakiwakilisha taifa letu katika michezo mbalimbali ya kimataifa.
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kujua serikali imechukua hatua gani dhidi ya viongozi wa chama hiki ambao badala ya kusimamia riadha wamekuwa hawafanyi hivyo , aidha kuna mikakati na mipango gani ya kuinua kiwango cha riadha hapa nchini ili kurudhisha heshima ya taifa kwenye mchezo huu maarufu duniani kote?
5.2 Mapato ya viwanja vya Taifa.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa randama uk 102 katika mapato kuna kifungu 140259 ambacho kinahusu mapato ya viwanja vya michezo (uhuru na Taifa) makadirio yalikuwa kukusanya shilingi 400,000,000 kwa mwaka 2012/2013 ila mapato halisi yaliyokusanywa kutokana na asilimia 15 ya mapato yote yanayokusanywa kutokana na kutumika kwa kiwanja hicho mpaka februari 2013 yalikuwa 329,814,400 tu.
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kujua mapato hayo yalikusanywa kutokana na michezo mingapi na fedha hizo zilitumika katika kufanya kazi gani za kuendeleza michezo hapa nchini.



5.3 Malipo kwa makocha wa kigeni.

Mheshimiwa spika, katika mwaka huu wa fedha serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.230 katika kifungu 6004-280518 (Baraza la Michezo la Taifa –Makocha)(chanzo:randama, jedwali namba 8) kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC),Aidha kwenye fungu hilo hilo 6004 kwenye matumizi ya kawaida (chanzo randama ;jedwali namba 6) zimetengwa jumla ya shilingi milioni 586,079,000 kwa ajili ya mishahara na matumizi mengineyo zimetengwa shilingi 1,917,960,000

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa randama ya wizara uk.93 kijifungu 270800 ‘ruzuku kwa asasi na vituo’ zimetengwa jumla ya shilingi 1,564,382,000 na katika kijifungu kidogo cha 270813 ‘Baraza la Michezo la Taifa’ zimetengwa shilingi 1,524,382,000 kwa ajili ya ‘mishahara ya Makocha wa Kigeni’ na matumizi ya Baraza la michezo la Taifa. Aidha katika mwaka wa fedha 2012/2013 kwenye kijifungu hiki zilitengwa jumla ya shilingi 823,546,000 tu kwa ajili ya mishahara kwa makocha wa kigeni.
Wakati kichwa cha habari cha kasma hii na kijifungu hiki kikisema ni ‘ruzuku kwa asasi na vituo’ , ruzuku inayokwenda kutolewa ni kiasi cha shilingi milioni 40 tu kama ambavyo inaonekana kwenye kijifungu 270839 kituo cha michezo Arusha shilingi milioni 20 na kijifungu 270840 kituo cha michezo Songea shilingi milioni 20.

Kambi rasmi ya upinzani, inaona kuwa fedha hizi ni nyingi sana kwa ajili ya mishahara na marupurupu ya makocha wa kigeni, hivyo basi tunataka kujua yafuatayo;
i.                    Ni makocha wangapi watalipwa na ni wa michezo gani?
ii.                  Wanapewa marupurupu gani kama stahili zao?
iii.                Kwanini serikali na wizara hii isiwapeleke makocha wa kitanzania mafunzoni nje ya nchi ili waweze kutumikia taifa lao pindi wakimaliza masomo yao?

6.0 BARAZA LA KISWAHILI TANZANIA
Mheshimiwa Spika,Wizara inao wajibu wa kuimarisha, kukuza na kuendeleza lugha yetu ya Kiswahili kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano ikiwa ni pamoja na uratibu na kuhakikisha ustawi na maendeleo ya utumiaji wa Kiswahili kwa kushirikiana na asasi zile ambazo zinahusika na uendelezaji wa lugha hii hapa nchini.  Baraza lina wajibu wa kuhakikisha kuwa matumizi ya Kiswahili yanapewa kipaumbele katika maisha ya kila siku ya mtanzania, ikiwemo katika shughuli za kitaifa na kimataifa ambazo viongozi wa taifa letu wanahudhuria.
Mheshimiwa Spika, Pamoja na nyimbo ambazo Serikali ya CCM imekua ikiziimba mara kwa mara kuwa inataka kukuza lugha ya Kiswahili ili kuutangaza utamaduni wa Tanzania katika jumuia ya kimataifa ni aibu kubwa kwa taifa letu pale ambapo viongozi wake waandamizi wanapokuwa watumwa wa lugha za nchi za Magharibi!
Mheshimiwa Spika, Kwa kuwa Serikali ya CCM imeamua kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na nchi ya China, ni kitendo cha kusikitisha na aibu kuona kuwa wakati wa ziara yake nchini, Raisi wa China, alihutubia na kuzungumza kwa ufasaha lugha ya taifa lake wakati Rais wa Tanzania na Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa wakitumia lugha ya Kiingereza. Swali la kujiuliza, kama Raisi wa nchi pamoja na waziri wake wanaona ugumu kutumia lugha ya taifa wakati mgeni wao ametumia lugha ya taifa lake wakati walengwa wa ujio ule na wageni wengi waliokuwa katika uzinduzi wa Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere wengi walikua ni watanzania, je itakuaje kwa mwananchi wa kawaida leo? Lugha ya Kiswahili haiwezi kukua wala kupewa umuhimu na mataifa mengine ikiwa viongozi wa Serikali wanaonesha hadharani utumwa wa utamaduni wa nchi za magharibi, lazima kwa nguvu zote Bunge na taifa tukatae aina hii ya utumwa kwa maana kuwa hata Serikali inayotakiwa kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili na kukitangaza, wamekua mstari wa mbele kutumia lugha ya Kiingereza.
Mheshimiwa Spika, kambi rasmi ya upinzani tunajiuliza hivi, Hata kama Serikali ya CCM imeshindwa kulinda tembo wetu basi hata Kiswahili mshindwe kukilinda? Tunarudia tena, huu ni utumwa! Haukubaliki! Tutumie na kukitangaza Kiswahili kwenye dhifa na hafla za kimataifa, kwa kuwa Kiswahili ndiyo urithi wetu.


7.0 USIMAMIZI WA HAKI ZA WASANII NA USHIRIKI WA SERIKALI KATIKA UTEKELEZAJI
Mheshimiwa Spika, Sheria ya hakimiliki inayotumika sasa katika kusimamia hakimiliki na hakishiriki za wasanii , ni sheria iliyopitishwa na Bunge inayojulikana kama Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki namba 7 ya 1999. Hii iliiondoa sheria ya awali Sheria ya Hakimiliki namba 61 ya 1966. Sheria hii imeendelea kutumika baada ya kutungwa kanuni mbalimbali mwaka 2000 na kuanza kutumika zikiwemo sheria iliyounda COSOTA. COSOTA ilianza kwa kuwa na bodi iliyokuwa mchanganyiko wa wajumbe waliochaguliwa na wasanii na wajumbe walioteuliwa na Waziri wa Viwanda na Biashara. Na hali hii ya kuwa na wawakilishi wasanii katika COSOTA iliendelea mpaka baada ya uchaguzi mkuu wa chama hicho 2007, ambapo Waziri hakuweza kuteua Mwenyekiti wa bodi ya chombo hicho na hivyo kuzuia Bodi kuweko.
Mheshimiwa Spika,hata alipoulizwa na Mh. Martha Mlata kwenye bunge la bajeti 2008 aliahidi kushughulikia na hakufanya hivyo hata akaulizwa tena bunge la bajeti 2009. Hivyo hatimaye  2011 ikateuliwa Bodi ambayo haikuwa na muwakilishi kutoka wasanii japokuwa COSOTA iliendelea kukusanya mirabaha ‘kwa niaba ya wasanii’.
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kujua ni kwanini bodi hii haina mwakilishi wa wasanii kama sheria inavyotaka? Lini mwakilishi huyo atateuliwa na wizara?

7.1 Kulinda kazi za wasanii
Mheshimiwa Spika, Mwaka 2001, ilitengenezwa kamati iliyoitwa National Anti Piracy Committee ikiongozwa na Mwenyekiti John Kitime, iliyokuwa chini ya COSOTA, kazi yake kubwa ni kuwezesha kutengeneza sheria na kanuni za kuwezesha kazi za audio na video kuwa na stika za mapato. Kazi hii ilifanyika na kukamilika na kanuni hizo zilipita kwa usimamizi wa Waziri Mh. Juma Ngasongwa kabla tu ya uchaguzi wa mwaka 2005, lengo likiwa ni kupata sapoti ya wasanii.
Mheshimiwa Spika, Baada ya jitihada za hapa na pale, Serikali kwa kupitia TRA wameleta stika mpya, ambazo  Tatizo moja tu hapa ni kuwa TRA kazi yao ni kukusanya kodi tu na sio kulinda hakimiliki, hivyo stika ya TRA ni stika ya kukusanya kodi na italeta mkanganyiko katika utekelezaji wa taratibu za hakimiliki. Je, wizara imepanga mikakati gani kuhakikisha kuwa kazi za sanaa hazidurufiwi, kuuzwa na kusambazwa bila ya ridhaa za wasanii nchini? Kambi rasmi ya upinzani bungeni inarudia kuitaka Serikali kuifumua COSOTA na kuunda chombo kipya kitachokuwa na uwezo wa kusimamia kazi za sanaa.
7.2 Nyimbo za wasanii na Mapato kwao.
Mheshimiwa Spika, Mwaka 2003 zilipitishwa kanuni zilizoagiza wenye vyombo vya utangazaji nchini ziwalipe wanamuziki kutokana na matumizi ya nyimbo zao mbalimbali ambazo wanazitumia kwenye vipindi mbalimbali. Ni jambo la kushangaza kuona kuwa Serikali ya CCM inayojitapa kuwa na utawala wa sheria inashindwa kudhibiti vyombo vya habari na utangazaji ambavyo vimeendelea kutumia kila aina ya ubabe na njia za kiunyonyaji ili visilipe fedha hizi kwa wasanii. Leo hii wasanii wanalazimishwa kuandika barua kuwa wametoa nyimbo zao kwa vyombo hivyo zipigwe bila kulipia na kutokana na mazingira yaliyotengenezwa, wanamuziki wanajikuta ni lazima wahonge! ili nyimbo zao zipigwe ili waweze kupata soko la kazi zao.
Mheshimiwa Spika,Wizara hii ambayo inasimamia TBC, televisheni na redio ya Taifa, imeshindwa kuvichukulia hatua za kisheria vyombo vyake ambavyo vimekua moja wapo ya wakiukaji wa sheria hii. Ni kejeli kwa taifa, ni kejeli kwa wasanii wanaopata shida kujikwamua kimaisha. TBC leo inapiga na kucheza nyimbo za wasanii bila kuwalipa, huku wizara inayotakiwa kusimamia vyombo hivi inashuhudia sheria zilizopitishwa na bunge hili zinavunjwa.
Mbaya zaidi TBC inauza CD na kanda za nyimbo zilizoko katika maktaba yake bila kutoa hata senti kwa wanamuziki waliorekodi nyimbo hizo, iko wapi tofauti yao na maharamia wengine? Leo hii wizara inawezaje kusema kuwa wao ni wasafi? Ni aibu kwa wizara, ni aibu kwa watendaji wake, ni aibu kwa serikali , sikivu, ya CCM!
7.2 Harakati za kudai haki za wasanii.
Mheshimiwa Spika, sanaa imeendelea kufanywa mtaji wa biashara na watu wachache ambao wanatumia nguvu waliyo nayo katika jamii na uwezo wao wa kifedha katika kukandamiza maslahi ya wasanii hapa nchini. Katika harakati za kutafuta haki za wasanii hapa nchini, mimi binafsi pamoja na wasanii wengine wachache, tulianzisha  harakati za kudai haki kwa kupitia programu maarufu iliyojulikana kama 'Anti Virus' chini ya 'Vinega' ikiwa na lengo na juhudi za kudai haki za wasanii dhidi ya ukandamizaji unaofanywa na wajanja wachache kwenye muziki, ambao wametumia nafasi kama njia ya kutumia mitaji yao ya fedha kuwaendesha wasanii jinsi wanavyotaka wao.
Mheshimiwa Spika, Kama ilivyo kawaida, wasanii wengi walidharau jitihada zetu na kutotuunga mkono. Leo hii katika tasnia ya muziki, kuna mgogoro mkubwa uliofuka moto kati ya msanii maarufu Lady Jaydee dhidi ya wamiliki wa radio ya Clouds FM hatua iliyosababisha  nyimbo za wanamuziki wa kizazi kipya maarufu kama 'Bongo Flavour' kutopigwa kwa siku moja katika kituo hicho. Sasa, ukiangalia kilio cha Lady Jaydee ni kilio kilekile kilichopelekea VINEGA kuingia vitani.
Mheshimiwa Spika, kama msemaji mkuu wa kambi ya upinzani bungeni, na mwenye dhamana na uchungu na tasnia ya sanaa nchini, niweke wazi kwa umma wa watanzania kuwa, tumefikia hapa tulipo si kwa kuwa na sheria kandamizi tu bali pia kwa kukosekana kwa umoja wa wasanii nchini. Wakati tukiwa na juhudi za kutetea maslahi ya watanzania kupitia Anti Virus, ni wasanii wachache ambao walituunga mkono na wengi wao wakibeza jitihada zetu, wakiwemo hawa ambao leo wanalalamika kuwa wananyonywa haki zao. Wengine walifikia hatua ya kusema kuwa tumepewa fedha ili kuzima harakati tulizozianzisha.
Mheshimiwa Spika, Umoja wa wasanii hasa wa muziki wa kizazi kipya nchini, unasimamiwa na chombo halali kinachojulikana TUMA-‘Tanzania Urban Music Association’, lakini kutokana na ujanja wa watu wachache, waliudhoofisha umoja huu kwa kuanzisha kampuni iliyosajiliwa kama TFU- ‘Tanzania Flavour Unit’ iliyowalaghai wasanii kuwa ni muungano wa wanamuziki wa Bongo Fleva na kuhodhi majukumu ya TUMA ambacho ni chama halali cha kusimamia wanamuziki wa Bongo Fleva. Mpaka tunapoongea leo hii, hata Studio iliyotolewa na Mheshimiwa Raisi, bado ipo katika mikono ya TFU pamoja na Serikali kuamuru irudishwe katika mikono ya Serikali ili ikabidhiwe kwa wasanii wote chini ya chama halali cha TUMA. Sasa tunataka wasanii wote nchini waache uoga na unafiki na wajiunge na vyama vyao halali ili viwatete haki zao.
Mheshimiwa Spika,Kumekuwa na upotoshaji mkubwa wa utetezi wa  haki za wasanii kwa kuwa wanaotuhumiwa kunyonya haki za wasanii wameweza kutajirika na kuneemeka kwa kupitia jasho na mgongo wa wasanii. Hawa hawa wanaotuhumiwa kuhujumu wasanii ndio wanatumia nafasi yao kuupotosha ukweli wa tuhuma dhidi yao. Wanatumia fedha na rasilimali walizo nazo katika kunyanyasa wasanii, kuwakandamiza, kuwapokonya haki zao na kuwadhalilisha kuwa bila wao, wasanii wasingekua kitu.
Mheshimiwa Spika, Leo hii wasanii wanaishi kwenye hali ngumu, umasikini mkubwa lakini bado wanatolewa maneno ya kashfa na dharau na Serikali imeendelea kukaa kimya. Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inaitaka Serikali kuacha siasa kwenye kutatua migogoro ya taifa hili. Siasa zimetumika sana katika kuzima jitihada za wanyonge kwenye taifa hili, leo hii wananchi hawana imani na Serikali kwa kuwa imeonesha wazi imeshindwa! Kushindwa kwa Serikali katika kutatua migogoro ya wasanii kwa kutotekeleza makubaliano mbalimbali yanayoafikiwa kati yake na wasanii, yameshusha hadhi yake kwa wasanii. Swali kubwa kwa Serikali sikivu ya CCM, Je mnasubiri migogoro mingapi ili mjue kuwa wasanii hawatendewi haki? Je mnasubiri vikao vingapi vya upatanishi  na usuluhihishi ili mjue kuna tatizo? Ama mnataka wasanii wagombane, wapigane, wauane ili mjue kuwa kuna tatizo?
Mheshimiwa Spika,Leo hii, Serikali bila ya kukaa na wadau wa muziki wa dansi, taarabu, bongo fleva, hip hop, mnanda na mahadhi mengine na kuwasikiliza kwa makini wamejikuta wanajihusisha na mambo ambayo hawajui. Watendaji wa Serikali wameendelea kuwaingiza mkenge viongozi wa Serikali katika masuala ya sanaa nchini. Hivi karibuni,hapa Dodoma, bila ya kuwa na taarifa muhimu juu ya unyonyaji wa haki za wasanii, waziri Mkuu Mh. Mizengo Pinda, alishiriki katika tamasha la kudai haki za wasanii ambalo liliandaliwa na baadhi ya watu ambao kwa muda mrefu wamekua wakituhumiwa kuwa ni wanyonyaji wa kazi za wasanii. Kiongozi mkuu wa Serikali, unashiriki katika kupiga mihuri na kuhalalisha mikakati ya kimafia ya kuua umoja wa wasanii bila ya kuwa na taarifa sahihi. Je, waziri mkuu ana taarifa kuwa walioandaa tamasha la kudai haki za wasanii ndio walalamikiwa namba moja nchini dhidi ya haki za wasanii hasa wa muziki? Tuinataka Serikali na wanasiasa wote kuacha kutumia wasanii  kwa faida zao binafsi bali wasaidie kutatua matatizo halisi ya wasanii ili waondokane na umasikini.
8.0 UTAMADUNI NA MALIKALE NCHINI
Mheshimiwa Spika,Zipo njia mbalimbali ambazo zinatambulisha utamaduni wa mtanzania kwa mataifa mengine. Utamaduni wetu unatambuliwa kwa kupitia lugha, mavazi, vyakula, sanaa, maadili na malikale za taifa letu. Leo hii ukiangalia makumbusho ya taifa, haina vitu vya msingi vya kufanya makumbusho kuwa chanzo cha kuliingizia taifa fedha za kigeni kwa njia ya utalii. Sehemu nyingi nchini ambazo zinaelezea utamaduni wetu na asili ya taifa letu, kama Bagamoyo, Kilwa Masoko, Kilwa Kivinje, Isimila, Zanzibar haziwekwi katika mazingira ya kuyatunza kwa ajili ya kuelezea asili ya taifa letu.
Leo hii , Serikali ya CCM ikijitetea kuhusu kuboresha ama kutunza malikale za taifa letu ikiwemo majengo ya kale, itajigamba kuwa imeyapaka rangi. Lakini ni maajabu kuona majengo yale, yamepakwa rangi nyeupe, chokaa hali inayoyafanya majengo haya kuwa na rangi za kijani zenye ukungu inapokuja suala la ukarabati wake. Ukiangalia marekebisho ya majengo hayo, yamefanyika na kuondoa uasilia wa majengo hayo kama yalivyokua zamani,.
Kambi rasmi ya Upinzani, inaiuliza Serikali je,imeshindwa kutafuta wataalamu wa majengo wenye kuweza kurekebisha na kuyatunza majengo katika hali ilokuwa  bila ya kuyaharibu zaidi? Ni mikakati ipi ambayo Serikali imejiwekea kwa mwaka huu wa fedha wa 2013/2014 katika kuyatunza na kuyatengeneza  majengo ya kale ili kutunza utamaduni wa taifa letu?
10.0 UCHONGAJI WA VINYAGO NA THAMANI YAKE KWA TAIFA
Mheshimiwa Spika,Kama kawaida Serikali ya CCM imeendelea kutawala huku kukiwa hakuna utaratibu mzuri wa kusimamia maslahi ya wachongaji wa vinyago hapa nchini. Wachongaji wa vinyago ambao wamesaidia kwa kiasi kikubwa kutangaza utamaduni wa taifa letu kwa kutumia kazi zao za sanaa hapa nchini hasa katika kutangaza utalii.
Kwa taarifa tulizonazo kutoka kwa wachongaji vinyago ni malalamiko ya kazi zao za sanaa kununuliwa na kisha kusafirishwa kuelekea nchi za nje ambapo huko hupigwa mihuri kuwa imetoka katika nchi za jirani. Hii imeua soko la vinyago hapo nchini na kukandamiza maslahi ya wachongaji hawa ambao ni hazina kwa taifa letu. Wachongaji vinyago wana umuhimu mkubwa katika kulinda utamaduni wa nchi yetu kwa kuwa ni urithi tuliopewa na ni lazima Serikali iweke mikakati ya kuhakikisha kuwa soko la vinyago ndani na nje ya nchi linamufaisha mchongaji kimapato.
Kambi rasmi ya upinzani bungeni, inaitaka Serikali kutoa kauli hapa bungeni ina mkakati gani uliowekwa kwa mwaka huu wa fedha katika kuhakikisha kuwa wachongaji vinyago wananufaika kwa kazi zao hasa ukizingatia kuwa, soko la ndani la vinyago halina faida ya kutosha na usimamizi wa kina. Vinyago ambavyo vinachongwa Tanzania vimeendelea kuuzwa nje ya nchi na kuzipatia nchi hizo mapato makubwa na baadhi ya kazi hizo hazitambuliwi kuwa zinatoka nchini.  
11.0 USIMAMIZI WA HAKI ZA WASANII KATIKA UUZAJI WA MIITO YA SIMU
Mheshimiwa Spika,Biashara ya miito ya simu, inayofanywa na makampuni ya simu nchini ni biashara ya siri ya kimafia inayohitaji kuwekwa wazi kwani kuna ukwepaji mkubwa wa kodi na haki za wasanii, ambapo pamoja na waliojiunga kihalali kutopata haki yao wako wale wanaokuta nyimbo zao zinatumika bila kujua zimepelekwa huko na nani na kwa mikataba ipi. Leo vyombo vyote vya Serikali vinavyotakiwa kusimamia sheria na kanuni za hakimiliki zinakaa kimya huku wasanii wakipokwa haki zao, taifa likipoteza mapato na kuubariki wizi huu wazi wazi.
Mheshimiwa Spika,Hivi karibuni tumeshuhudia Serikali ya CCM kupitia wizara yake yenye dhamana ya kufuatilia biashara ya miito ya simu, wizara ya mawasiliano, sayansi na teknolojia imeshindwa kutoa majibu ya ufuatiliaji wa tozo na mapato ya miito ya simu, Mmeshindwa kutimiza wajibu wenu kwa wananchi lakini pia mmeshindwa kutimiza wajibu wenu katika kutekeleza matakwa ya katiba ya nchi hii, kuulinda uhuru na haki za wananchi wake kama ambavyo muasisi wa taifa hili alijitahidi kufanya.
12.0 TASNIA YA FILAMU NA MCHANGO WAKE KATIKA KUKUZA UCHUMI NCHINI
Mheshimiwa Spika,Tasnia ya filamu nchini imeendelea kukua kila siku huku kukiwa na usimamizi mdogo wa Serikali katika kuhakikisha kuwa sekta hii inatumika vizuri kama chanzo cha kukuza ajira nchini lakini pia kama moja ya njia ya kuwaongezea wananchi kipato na Serikali kukuza uchumi kwa kupitia kodi mbalimbali. Leo hii, soko la filamu nchini Nigeria limeweza kuingiza takribani kiasi cha dola 250 milioni kwa mwaka kama mapato ya filamu zinazotengenezwa kwa soko lao la Nollywood, je Serikali kupitia wizara hii imefanya tathmini gani kwa kupitia mamlaka za mapato na kujua soko la filamu kwa mwaka linaingiza kiasi gani hapa nchini? Kambi rasmi ya Upinzani, inaitaka Serikali ya CCM kuacha kufanya kazi kwa mazoea sasa na badala yake ivisimamie vyombo husika kuhakikisha kuwa sekta ya filamu inapewa kipaumbele pia na thamani ili kuweza kukusanya kodi na kupunguza umasikini nchini. Tasnia ya filamu si tu inaweza kuliingizia soko hili fedha bali pia ikipewa thamani inauwezo mkubwa kwa kutatua tatizo la ajira hapa nchini. Kwa kuwa mpaka sasa, Tanzania imeshatoa filamu nyingi na soko lake kupanuka katika nchi za Afrika Mashariki na kati, je tasnia hii mpaka sasa imeweza kuzalisha ajira ngapi? Kambi rasmi ya upinzani, inaitaka wizara kuja na takwimu rasmi za ajira zilizotokana na tasnia hii kufikia mwezi Machi mwaka huu.
Mheshimiwa Spika,Tanzania ambayo imebarikiwa kwa kuwa na vivutio mbalimbali vya utalii, ikiwemo Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama za Serengeti, Ngorongoro, Manyara, Mikumi pamoja na hifadhi za wanyama kama Selous, Tarangire, maziwa makubwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa, sehemu zenye asili ya utumwa kama Bagamoyo, Zanzibar, Kilwa Masoko, misitu mikubwa, mito na vivutio mbalimbali; ina nafasi kubwa ya kutumika kama moja ya 'film destinations' duniani kama ambavyo nchi nyengine imewekeza.
Mheshimiwa Spika,Nchi mbalimbali zimeweza kujiingizia fedha za kigeni kila mwaka kutokana na kutumia vivutio walivyo navyo na mandhari ya nchi zao kupitia tasnia ya filamu. Nchini Afrika Kusini, tasnia ya filamu ina thamani ya kiasi cha takribani randi 12 bilioni sawa na shilingi trilioni 2.17 za kitanzania huku ikichangia kiasi cha shilingi 1.4 bilioni kwenye uchumi wa taifa na ongezeko la kiasi cha shilingi milioni 400 kwa mwaka katika kipindi cha miaka minne toka mwaka 2008 walipoamua kufanya mabadiliko ya tasnia ya filamu. Zaidi , tasnia ya filamu imeweza kuongeza soko la ajira kwa kutoa karibu ajira 30,000.[1]Afrika kusini imeweza kutumia sekta hii kwa kwa kutumia mandhari waliyo nayo ambayo inafanana na mandhari za takribani nchi 57 ulimwenguni na kutumika kutengeneza filamu zenye mafanikio Hollywood. Ipo haja ya wizara hii kwa kushirikiana na wizara ya maliasili na utalii kufanya tathmini ya kina na kutengeneza mazingira ya kutumia vivutio tulivyo navyo ili kuifanya Tanzania sehemu bora zaidi Afrika kwa ajili ya kutengeneza filamu kwa kupitia mandhari zake. Lazima Serikali itengeneze mkakati endelevu wa kuendeleza sekta ya filamu nchini kwa kuitangaza Tanzania katika anga za kimataifa kama 'film destination' bora zaidi Afrika.
13.0 MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI 2013/2014
Mheshimiwa Spika, katika makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hii kwa mwaka wa fedha 2013/14, jumla ya shilingi 21, 328,045,000, zimeombwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na miradi ya maendeleo.
Aidha, kama ilivyo ada ya miaka yote kwa bajeti za serikali hii ya CCM, katika wizara zote, fedha za matumizi ya kawaida ni nyingi kuliko fedha ambazo zinatarajiwa kutumika katika miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Suala linaloweza kumuumiza mdau yeyote ambaye angependa kuona wizara hii ikisonga mbele ni pale ambapo miradi ya maendeleo imetengewa sh. 600,000,000 pekee, wakati kuna kiasi cha takriban bilioni 10 zimetengwa kwa ajili ya kitu kinachoitwa ‘matumizi mengineyo’.
Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inahoji hayo matumizi mengineyo yasiyojulikana au kuelezwa hapa mbele ya bunge lako lakini yanatengewa karibu nusu yote ya bajeti ya matumizi ya kawaida, ni nini na yapi?
Mheshimiwa Spika, Baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, naomba kuwasilisha.

.......................................
Joseph Osmund Mbilinyi (Mb)
Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani-Wizara ya Habari,Vijana, Utamaduni na Michezo.
20.05.2013